Padri Privatus Karugendo
INGAWA sheria za Serikali za Mitaa zilishafanyiwa marekebisho ili kuzipatia uwezo wa kuajiri na kusimamia watumishi wake, bado wizara za kisekta zinaendelea kupenda kuendelea kuwasimamia hata wale watumishi walioko kwenye halmashauri.
Hali hii inawababaisha sana watumishi. Ipo haja ya kuweka mipaka iliyo wazi ya majukumu ya Tume ya Utumishi wa Umma na yale ya halmashauri kuhusu ajira na usimamizi wa watumishi.
Haya yote yananisukuma kusema kwamba kinachohitajika si kuboresha mifumo, bali ni mapinduzi ya kina katika Serikali za mitaa na Serikali Kuu.
Sheria
Mwaka 1997 ilipitishwa sheria mpya ya Tawala za Mikoa Na. 19. Haya yalikuwa ni mazingira mazuri ya kuelekea Serikali za Mitaa.
Marekebisho ya Sheria za Serikali za Mitaa za mwaka 192 yalifanyika ili kujumuisha dhana ya kupeleka madaraka kwa Wananchi (decentralization by devolution) inayojulikana kama ‘D by D’ na kuweka mahusiano mapya kati ya Serikali Kuu na Serikali za Mitaa.
Sheria Na. 6 ya mwaka 1999 ilipitishwa ambayo ilivifanyia marekebisho baadhi ya vifungu vya sheria Na, 8,9, 10 ya 1982.Vile vile, kanuni za usimamizi wa fedha, usimamizi wa watumishi, na maadili ya madiwani na maadili ya watumishi wa halmashauri zilitungwa na kutolewa.
Kwa nyongeza ya hapo, taratibu za uchaguzi wa viongozi katika ngazi ya kijiji, mtaa na kitongoji ziliandaliwa na kutumiwa katika uchaguzi wa mwaka 1999.
Sasa hivi juhudi inayofanyika ni kuainisha sheria za kisekta ili ziendane na zile za Serikali za Mitaa kwa nia ya kuondoa migongano.
Migongano hii ilikuwa inatokea na bado inatokea kwasababu kama tulivyosema tangu mwanzo mifumo yetu ilikuwa imekaa kichwa chini miguu juu.
Na kulifanikisha hili, ingawa itayachosha masikio yetu, ni kufanya mpinduzi ya kweli na wala si kuboresha tu!
Hili ninalolisema linajitokeza katika utekelezaji wa Sheria za Serikali za Mitaa. Sheria hazifuatwi na zinavunjwa kiholela. Hili bado linafanyika pale ambapo maboresho yameanza na kufanya kazi na sehemu ambazo bado wako kwenye hatua za mwanzo.
Hii inatokana na halmashauri kutokuwa na wasimamizi wa sheria zao na wananchi kuwa na uelewa mdogo wa haki zao na madaraka yao na wajibu wao katika serikali za mitaa.
Kukosekana kwa huduma za polisi na mahakama huko vijijini kunatoa mwanya kwa baadhi ya watendaji katika ngazi za chini kuwa ‘miungu wadogo’ na kutenda vitendo viovu, hali ambayo inaweza kusababisha kuvunjika kwa amani.
Watendaji wa vijiji na kata wanafanya kazi ya polisi, hakimu, afisa biashara TRA n.k! Sasa hivi programu ya maboresho imeanza kuwapatia mafunzo watendaji wa vijiji mitaa na kata ili waweze kujua mipaka yao ya kazi.
Kama tulivyoona kwa upande wa wahasibu katika halmashauri, ni sawa na kwa upande wa sheria.
Kuna upungufu wa wanasheria. Hivyo ushauri wa kisheria haupatikani. Mivutano isiyokuwa ya lazima inaendelea na wakati mwingine halmashauri zinashitakiwa na kupoteza mali nyingi kwa kutokuwa na ushauri wa kisheria.
Mifano yote hii inalenga kuonyesha jinsi maboresho yanavyopaswa kuwa mapinduzi. Ni lazima halmashauri ziwe katika hali ya kuwavutia wataalamu wa kila sekta.
Lakini pia ni lazima tuwe na mfumo wa kuwaandaa wataalam wetu katika hali ya uzalendo.
Hakuna miujiza ya kutoka mbinguni na kuboresha hali ya maisha yetu. Ni lazima wawepo wa kujitoa muhanga na kuandaa mazingira bora ya baadaye.
Kwa vile programu ya maboresho itagusia pia na mfumo wa elimu, tuliachie hapa. Lakini ni lazima kuwa macho maana mfumo wa elimu wa kulifaa taifa letu hauwezi kutoka nje. Utajengwa na sisi na wala si wageni.
Usimamizi wa Mpango wa Uboreshaji
Usimamizi wa utekelezaji wa Mpango wa Uboreshaji ni jukumu la Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa. Wakati wa kuandaa programu, Serikali ilikubaliana na wabia wake iundwe timu ya wataalamu wa kuiwezesha wizara yenye dhamana ya Serikali za Mitaa kusimamaia utekelezaji wa Mpango wa Uboreshaji wa Mfumo wa Serikali za Mitaa.
Mpango wa aina hii ambao unalenga kubadili fikra, mazoea na tabia za watu unahitaji muda mrefu wa maandalizi, na ushirikishwaji ili kupata maamuzi ya pamoja na fedha nyingi zinahitajika kugharamia uboreshaji unaokusudiwa.
Kubadilisha fikra, mazoea, tabia, mifumo, si “Maboresho” bali ni mapinduzi! Labda neno maboresho lilitumika kukwepa ukali wa neno mapinduzi?
Mbona tuna Chama Cha Mapinduzi? Kama sikosei wale waliobuni jina la Chama Cha Mapinduzi, walikuwa na lengo la kupindua fikra, mazoea, tabia na mifumo iliyopitwa na wakati, ili kuunda mifumo ya kizalendo ya kuharakisha maendeleo na kulinda uhuru wa nchi yetu.