<?xml version="1.0" encoding="utf-8"?><?xml-stylesheet href="http://www.habaritanzania.com/templates/Default/RssDisplay.xslt" type="text/xsl"?>
				<rss version="2.0">
				  <channel>
						<title>Habari Tanzania - Blogs</title>
						<link>http://www.habaritanzania.com</link>
						<description />
						<language>en-us</language>
						<copyright>http://www.habaritanzania.com</copyright>
						<generator>N/A</generator>
						<webMaster>info@habaritanzania.com</webMaster>
						<lastBuildDate>Thu, 20 Nov 2008 15:02:46 EAT</lastBuildDate>
						<ttl>20</ttl>

					<item>
					  <title>Ziara za mawaziri mikoani ni ufujaji wa fedha</title>
					  <link>http://www.habaritanzania.com/blogs/44/Ziara-za-mawaziri-mikoani-ni-ufujaji-wa-fedha</link>
					  <description>MAPEMA wiki hii serikali iliwatawanya mawaziri na manaibu mawaziri na makada wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) mikoani, kwa maelezo ya kwenda kuelezea wananchi ubora wa bajeti ya mwaka 2007/2008.  Uamuzi huo wa serikali kuwapeleka viongozi hao mikoani, umezua mjadala mpya hapa nchini, kwani wananchi wa kada mbalimbali wamekuwa wakihoji manufaa ya ziara hizo kwa umma, kwa kuwa zinatumia fedha za walipa kodi, ambao wengi wao ni walalahoi.  Baadhi ya wananchi wamesikika wakieleza kuwa ziara hizo zimedhihirisha ni jinsi gani serikali ilivyokumbwa na kiwewe kutokana na sumu iliyomwagwa na wapinzani waliofanya ziara katika mikoa mbalimbali nchini.  Kwa upande wetu tunapingana na hatua ya serikali kuamua kuwatawanya mawaziri mikoani kuelezea uzuri wa bajeti, kitendo hicho ni ufujaji wa fedha za walipa kodi.  Hatuna hakika kama ziara hizo zina lengo la kueleza uzuri wa bajeti ya mwaka huu, kwani kuna taarifa zinazodai kuwa ni njia mojawapo ya kujipigia kampeni kwa ajili ya uchaguzi wa ujumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa ndani ya chama hicho (NEC) unaotarajiwa kufanyika Novemba mwaka huu.  Kama ni uzuri na ubaya wa bajeti, tayari wananchi wameishaujua tangu ilipopitishwa bungeni Julai mwaka huu, kwani ni dhahiri kwamba baada ya kupitishwa kwa bajeti hiyo gharama za maisha zimepanda na hali ya maisha kuwa ya juu.  Hatuelewi hawa mawaziri sasa wanakwenda kuwaeleza wananchi kitu gani wasichokifahamu, angalau ingekuwa na maana kama ziara hizo zingefanyika muda mfupi baada ya kupitishwa kwa bajeti hiyo.  Hata kama kungekuwapo ulazima wa kufanya hivyo, jukumu hilo wangeachiwa wabunge ambao si mawaziri, kwani tunaamini wana nafasi nzuri ya kuwafikia wananchi na kuwaeleza kwa kinaga ubaga.  Hapa ndipo unapoonekana umuhimu na kuwapo kwa mgawanyiko wa madaraka na si kwa kiongozi mmoja kuwa na vyeo lukuki. Hebu Watanzania tujiulize, hawa mawaziri waliotawanywa mikoani hawana majukumu mengine ya kitaifa ya kufanya katika wizara wanazoongoza?  Ni dhahiri zipo nyingi, na kwamba iwapo mawaziri hao wangetumia nafasi hizo wangesaidia kupunguza misongamano ya kazi za kila siku zinazowakabili.  Ieleweke kwamba Watanzania hivi sasa wanauelewa mkubwa, hivyo kitendo cha serikali kushindwa kutoa majibu thabiti kuhusu hoja za wapinzani, na badala yake kuamua kutumia ujanja wa kuwatuma viongozi wake kupunguza sumu ya wapinzani, kwa maelezo ya kueleza uzuri wa bajeti na kuwaponda wapinzani, ipo siku italeta madhara kwa viongozi hao.  Katika akili ya kawaida mtu mwenye njaa hawezi kucheza ngoma hata kama ni ya mfalme, sembuse bendi ya TOT-Plus? Ni dhahiri wananchi hawataweza kushangilia mikutano hiyo kwakuwa tayari wameishaona hakuna dalili za maisha bora kuwafikia.  Katika kuonyesha kuwa wananchi wamechoshwa na ahadi hewa na ambazo hazitekelezeki zinazotolewa na serikali, wananchi wamefikia hatua ya kuwazomea baadhi ya viongozi wa serikali wakiwemo mawaziri walioko katika ziara hizo.  Mawaziri ambao wamo kwenye ziara hizo ni Waziri wa Chakula, Kilimo na Ushirika Stephen Wassira, Waziri wa Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana, John Chilligati na Naibu Waziri wa Usalama wa Raia, Mohamed Aboud, na baadhi ya makada wa chama hicho Shaibu Akwilombe, Tambwe Hizza na Salim Msabaha, ambao walijiunga na CCM wakitokea kambi ya upinzani.  Hakika zomeazomea kwa viongozi haileti picha nzuri kwa jamii, hivyo serikali na CCM wanapaswa kujiuliza ni kwanini wananchi wamefikia hatua hiyo ya kuwazomea viongozi hadharani?  Tunasisitiza na kutoa ushauri kwa serikali, dawa ya hoja za wapinzani si kuwatoa ofisini viongozi hao wa serikali katika ofisi zao na kwenda mikoani kuhutubia wananchi, tena kwa kutumia fedha za walipa kodi na fedha za CCM , dawa ni kujibu hoja hizo kwa vitendo na si maneno ya kila kukicha.  Ili serikali iendelee kuaminiwa na kuheshimiwa na wananchi ni lazima itimize ahadi zake kwa vitendo na si maneno, kwani hayawasaidii kuleta maendeleo kwa wananchi ambao wamekwisha kuanza kuonyesha kukata tamaa.</description>
					  <author>Marshy Abdu</author>
					  <pubDate>Fri, 05 Oct 2007 00:00:00 EAT</pubDate>
					  <subject />
					</item>

				

					<item>
					  <title>Njozi ya Karne: Tanzania baada ya CCM kung'olewa</title>
					  <link>http://www.habaritanzania.com/blogs/43/Njozi-ya-Karne%3A-Tanzania-baada-ya-CCM-kung%92olewa</link>
					  <description>   Samson Mwigamba     NINA njozi ninayohitaji kuishiriki na Watanzania wenzangu. Njozi ni maono ya mambo yajayo, mambo yatarajiwayo katika siku za usoni.  Natamani wanasiasa wa kambi ya ushindani (si ya upinzani), waisome njozi hii kwa makini kwa kuwa ikikubalika kwa Watanzania walio wengi, wanasiasa hawa watakuwa na jukumu la kuhakikisha njozi hii inatimia.  Katika njozi hii ninaona Watanzania katika kila kona ya nchi yetu wakilia. Kilio chao wote kikiwa ni: "Watawala (si viongozi) wametutupa. Wamejitenga nasi. Wameweka pengo kubwa kati ya walionacho na wasiokuwa nacho. Tajiri wa Tanzania anazidi kuwa tajiri wakati maskini akizidi kuwa fukara."  Naona Watanzania wakikata tamaa. Walio vijijini wanalia na kusema heri yenu mlio mijini. Wanafikiri watawala wamewekeza mijini, hivyo wanafanya bidii kuhamia mijini ili wapate hayo maisha bora wanayoyasikia kila siku kwenye vyombo vya habari.  Wanadhani ukifika tu mjini unapata kazi nzuri hata kama elimu yako ni Darasa la Saba maana mgombea urais aliyeshinda alitangaza kwamba akiingia madarakani atatoa ajira milioni moja kwa vijana (hakusema ni lazima wawe na elimu fulani).  Baada ya kupata kazi, nyumba nzuri ya umeme, kusafiri hata umbali wa kilometa mbili kwa gari, matibabu kwenye mahospitali makubwa na yenye hadhi kama Muhimbili, KCMC, Bugando, Ocean Road na raha nyingine za maisha, vinakuwa ni halali yako.  Walikuwa wamekosea. Walipofika mijini walikuta hali tofauti kabisa. Ajira milioni moja hazipo isipokuwa elfu kadhaa tu kwa vijana waliomaliza Kidato cha Sita waliopigwa msasa wa mwezi mmoja wakapelekwa kufundisha shule zinazoitwa za kata ambazo wengi wamekuwa wakiziita vituo vya kulelea watoto.  Kwa nini zisiwe vituo vya kulelea watoto ikiwa msichana niliyemfundisha twisheni mwaka 2003 akiwa Kidato cha Nne, mwaka 2006 akamaliza Kidato cha Sita. Mwaka 2007 akahudhuria hiyo voda fasta (kama wanavyoiita wao), alipomaliza akaripoti shule aliyopangiwa na wakajikuta wako walimu wawili tu tena wote ni wasichana na wote wametoka kwenye hiyo programu ya mwezi. Wakiwa wao tu na watoto wanachaguana, wewe uwe mkuu wa shule (headmistress) na mimi nitakuwa mkuu msaidizi (second mistress).  Vijana hawa kutoka vijijini wakakuta vijana wenzao wenye elimu za vyuo mbalimbali na hata vyuo vikuu wakizunguka na vyeti kila siku hadi soli za viatu zinaisha lakini kazi hawapati. Makampuni waliyotarajia yawaajiri yamebinafsishwa yote na kupunguza wafanyakazi wazalendo na kujaza wafanyakazi kutoka nje hata kwa nafasi za ngazi za chini kabisa. Hata shule za msingi zinazoitwa English medium zimejaza walimu kutoka Kenya na Uganda japo wengi wao wanachojua ni Kiingereza peke yake.  Vijana hawa wakaishia kuwa wamachinga na wapigadebe huku wakikumbana na virungu vya askari wa jiji kila uchao, kwa madai aidha ya kufanya kazi isiyotakiwa ama kufanya biashara maeneo yasiyoruhusiwa.  Wale waliojiajiri kwenye machimbo ya kokoto wakatimuliwa bila kupewa eneo mbadala au kazi mbadala. Wakaishia kuishi kwa mlo mmoja kwa siku ambao hata hivyo ni mhogo wa kukaanga (chipsi dume) na maji, na bado uhakika wa kuupata haupo.  Wakaishia kuishi kwenye nyumba za tope (mbavu za mbwa) zisizo na umeme na ambazo hata hivyo hawana pesa za kulipia kodi, hivyo ni kupanga hapa hadi mwenye nyumba amtimue kwa kutolipa kodi anahamia pale.  Ni vijana wa namna hii ndiyo ninaowaona wakiongoza na kuwa chachu ya mabadiliko. Ndiyo watakaoimba "Hakuna kulala mpaka kieleweke". Sauti zao zinapokewa na wananchi wa kawaida kuanzia na wale walio katika maeneo yenye migodi ya madini hadi kwa wananchi wa hali ya chini mijini na vijijini.  Walio katika maeneo yenye migodi wanalia kwa kuhamishwa hovyo katika maeneo yao ili kupisha wawekezaji tena bila kulipwa fidia ya kueleweka. Kibaya zaidi hadi migodi itakapofungwa hakuna chochote watakachoambulia zaidi ya umaskini ulioongezeka na kazi ya kufukia mashimo.  Wakulima wakililia gharama za pembejeo zilizo juu wakati bei ya mazao yao ikishuka mwaka hadi mwaka na serikali ikiendelea kutumia mabilioni ya pesa kuendesha 'mashangingi' ya wakubwa na kuwapeleka wakubwa nje eti kuangalia tu afya zao badala ya kutumia pesa hizo kuwapatia wakulima pembejeo bure.  Wananchi wa hali ya chini mijini wanalia na ugumu wa maisha. Umeme hawana na walio nao hawamudu tena kuulipia, bei ya mkaa imepanda mara dufu huku mafuta ya taa nayo yakipanda. Nishati gani itakuwa kimbilio kwao?  Mbali na hilo, kutokana na bajeti muflisi iliyotangazwa na serikali yao, kila bidhaa imepanda bei. Wataishije? Kando yao wapo wafanyakazi waliodanganywa kwa tume ya kuangalia upya mishahara ya watumishi wa umma lakini wakaja kuongezewa sh,12,000 tu wakati mfumko wa bei ukipanda juu?.  Wananchi hawa walidanganywa kuwa ada ya shule za msingi imefutwa wakati michango wanayotakiwa kutoa ikiongezeka mara kumi ya hiyo ada waliyokuwa wanalipa.  Waliambiwa sasa ada ya shule za sekondari za serikali imepunguzwa hadi sh 20,000 kwa shule za kutwa na 70,000 kwa shule za bweni, lakini wakajikuta wakitakiwa kuchangia majengo, chakula, vitabu, n.k, na kufanya punguzo la ada waliloambiwa liwe ni ongezeko.  Wakaambiwa serikali itajenga shule kila kata, lahaula! kumbe wajenzi walikuwa ni wao tena sehemu nyingine kwa lazima kiasi cha kufungwa kamba kama wahalifu wa makosa ya jinai hadi hapo watakapotoa huo mchango wa sh 10,000, kiasi ambacho kwa baadhi ya wananchi wa vijiji vyetu ni zaidi ya pato lao la mwaka.  Naona sauti za kilio cha wananchi hawa maskini wa Mungu kikipanda kila siku mbele ya kiti cha enzi cha Muumba wao. Kisha kwa huruma Mwenyezi Mungu akaongea na wanasiasa wa kambi inayoitwa kimakosa ya upinzani na kuwaambia, "Ondoeni ubinafsi wa kila mtu kutaka kugombea urais maana nimewatuma kuwakomboa watu wangu wa Tanzania wanaoteswa na mafarao wa kisasa"  Ghafla wazo linawajia wapinzani wote wenye nguvu za kisiasa na wanaitana. Agenda ni moja tu, kulikomboa taifa. Njia ya ukombozi ni kuzunguka nchi nzima na kuwatangazia watu wote kwamba mwisho wa mateso yenu mbele ya mafarao umewadia. Sisi ndiyo kina Musa, Haruni, Joshua na Karebu wa leo tutakaowapeleka Kaanani ya leo. Wananchi wanaitikia kwa kishindo kikuu na kushangilia ujio wa akina Musa.  Vyama hivi vinashirikiana kwa kusaini mkataba utakaowaongoza katika mapambano haya mapya. Wanaanza kwa kuanika uozo wa viongozi wa serikali na chama tawala na madhila wanayowafanyia wabunge wa upinzani kwa kutetea ukweli japo ni wachache mno bungeni.  Kamati maalum iliyosheheni wataalamu wa mambo ya uchumi, siasa, utawala na sheria inaundwa. Kazi ya kamati hii ni kuunganisha sera za vyama vyote vilivyokubali kushirikiana na kutengeza sera moja itakayoongoza ukombozi wa kiuchumi chini ya serikali mpya ya umoja wa kitaifa.  Na wakati wa uchaguzi mkuu wanadhamiria kusimamisha mgombea mmoja katika kila ngazi kuanzia urais, ubunge hadi udiwani.  Naona muda wa kampeni ukiwadia. Kwa siku kama 70 hivi, bendera ya helikopta ya upinzani inapepea kila kona ya nchi yetu ikiwa imebeba tumaini jipya kwa watanzania zaidi ya milioni 35 wakati 'mashangingi' ya CCM yakivinjari maeneo yenye upinzani mkali ili eti kukomboa majimbo!  Kila mahali inapotua helikopta hii wananchi wanaipokea kwa shangwe na vifijo na kuimba kwamba helikopta pasua anga ya CCM, ukakisambaratishe kabisa chama kilichotekwa na matajiri na mafisadi.  Tangaza Azimio la Songea na katakata kamba za CCM zilizotufunga kwenye umaskini kwa miongo kadhaa. Wanaimba, "Mwaga CCM - mwaga, ahadi hewa mwaga - mwaga maisha bora hewa - mwaga na Kikwete mwaga, Kingunge mwaga na Lowassa -mwaga"  Siku ya uchaguzi kura zinapigwa. Jitihada zote za chama tawala kupata ushindi wa halali na usio halali (kwani kama waliibiana kura wao kwa wao kwenye uchaguzi wa ndani ya chama watashindwa kuiba za wapinzani wao?) zinashindikana kutokana na kiwango cha kura za upinzani na umakini wa wananchi kulinda kura zao.  Ndipo kwa kigugumizi kikubwa mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi analazimika kumtangaza kwa mara ya kwanza mgombea asiyetoka CCM kuwa mshindi wa urais na kuwatanganza wabunge kedekede kutoka kambi ya upinzani.  Baada ya kulihutubia Bunge, rais mpya anatangaza Baraza la Mawaziri dogo kuliko yote tangu tupate uhuru, lakini lenye sura ya kitaifa na lililojaa watu wenye uchungu na nchi hii. Baraza litakuwa na mawaziri sita tu na manaibu wao wasiozidi 10.  Wizara zitakuwa ni Uchumi na Mipango, Fedha, Mambo ya Ndani, Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama na Miundombinu. Kazi kubwa itafanywa na makatibu wakuu na wakurugenzi ambao ndiyo watendaji. Hivyo wizara za sasa hata zingeunganishwa tano kuwa moja bado inaweza kuongozwa vema na waziri mmoja.  Naona Tume ya Marekebisho ya Katiba inaundwa mara moja ikihusisha wajumbe kutoka kada mbalimbali kama vijana, wazee, akina mama, wanasiasa wa chama tawala na upinzani, walemavu, wanaharakati mbalimbali, wafanyakazi, wafanyabiashara, wachumi, wanasheria, wanataaluma na wakulima.  Lakini wakati tume hii ikiendelea kukusanya maoni, serikali inaanza kuchukua hatua za haraka za kurekebisha mambo yaliyokuwa yakilitia taifa hasara na ambayo hayahitaji marekebisho ya katiba, ikiwa ni pamoja na:  Kuuza kwa mnada 'mashangingi' yote ya serikali yapatayo 6,000 na kuwanunulia magari ya kawaida viongozi wa serikali, kurudisha nyumba zote walizojiuzia vigogo wakati wa Chukua Cha-umma Mapema (CCM) na kuondokana na gharama kubwa za viongozi wa serikali kuishi kwenye mahoteli.  Kupitia upya mikataba yote ya uchimbaji madini katika nchi yetu na kufuta vipengele vinavyoliibia taifa mapato, kuweka watendaji wa serikali kwenye vitengo vyote nyeti kwenye makampuni ya madini vya uzalishaji, usafirishaji na uuzaji madini ili kuhakikisha kile kinachoripotiwa ndicho hasa kilichopatikana, kupunguza idadi ya viongozi wanaoruhusiwa kutibiwa nje na wale watakaoruhusiwa itakuwa ni kwa magonjwa machache tu au katika mazingira maalum tu na kwa utaratibu mahsusi si daktari wa mhusika kuandika tu mapendekezo na mtu anachota pesa hazina. Matibabu hewa mwisho.  Kuweka udhibiti wa hali ya juu katika mapato yatokanayo na utalii na uvunaji wa maliasili zetu kama mistu, uvuvi, n.k. kuzidisha udhibiti wa makusanyo ya kodi na kufuta mara moja misamaha holela ya kodi kwa wafanyabiashara wakubwa, kupitia orodha ya watumishi wote wa serikali kwa umakini mkubwa ili kubaini wafanyakazi hewa ambao wamekuwa wakilipwa mishahara bila kuwa kazini.  Naiona katiba mpya ya nchi ikiwa imekamilika na kuridhiwa na Bunge maalum la Katiba. Katika katiba mpya mambo yafuatayo yamezingatiwa:  Kifungu kinachompa rais mstaafu kinga ya kutoshitakiwa kwa maovu aliyoyafanya wakati akiwa rais kimefutwa, madaraka makubwa aliyokuwa nayo rais ya kuteua mawaziri, wakuu wa mikoa, wakuu wa wilaya, wakurugenzi wa majiji,manispaa, miji na wilaya, makatibu tawala wa mikoa, mabalozi wa Tanzania nchi za nje, makatibu wakuu wa wizara, wakuu wa vyuo vikuu na taasisi nyingine za serikali, yamepunguzwa sana.  Watendaji wakuu wa vyuo vikuu vya umma na wa taasisi nyeti kama TANROADS, TBS, n.k, watateuliwa na tume ya utumishi wa umma kwa taratibu maalum na kwa kipindi maalum.  Uteuzi wa mawaziri, mabalozi, Jaji Mkuu, wakuu wa majeshi, Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa hesabu za Serikali, mkuu wa taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa (TAKUKURU) na taasisi nyingine nyeti lazima uthibitishwe na Bunge na kuondolewa kwao kunalindwa na katiba, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa imekuwa huru, haiko tena chini ya ofisi yoyote ya Serikali na ni vivyo hivyo kwa Mahakama na Tume ya Uchaguzi.  Wenyeviti wote wa vyama vya upinzani vyenye wabunge wanakuwa moja kwa moja wabunge kikatiba na mwenyekiti wa chama cha upinzani chenye wabunge wengi ndiye anayekuwa kiongozi wa upinzani (safari hii atakuwa Mh. Jakaya Kikwete). Hii itaongeza demokrasia na mijadala iliyoshiba ndani ya Bunge.  Katiba imepitisha mfumo wa utawala wa majimbo na nchi imegawanywa katika majimbo yasiyozidi manane na kufanya vyeo vya ukuu wa mkoa na ukuu wa wilaya kufa kifo cha kawaida. Kila jimbo litakuwa na bunge lake na litaongozwa na gavana na timu ya watendaji.  Chini ya jimbo kuna halmashauri za wilaya, miji, manispaa na majiji yenye mabaraza yake ya madiwani na kuongozwa na wakurugenzi watendaji na timu zao.  Kila jimbo linakusanya mapato kutokana na kodi, maliasili zake na vyanzo vingine na kupangilia matumizi yao kulingana na vipaumbele vyao kama elimu, miundombinu, mawasiliano, maji, umeme, viwanda, kilimo, n.k, baada ya kutoa asilimia 20 ya mapato yake kwa serikali kuu.  Mikataba yote itakayoingiwa kati ya majimbo na wawekezaji sharti iridhiwe na mabunge ya majimbo husika. Nafasi ya waziri mmoja kutoka sehemu moja ya Tanzania kwenda nchi za nje na kusaini mkataba unaohusu maliasili ya sehemu nyingine ya Tanzania ambayo huenda hajawahi hata kufika na hajui kiwango cha maliasili iliyopo pale na maisha ya watu wa pale, haipo tena. Ni wananchi wa pale kupitia wawakilishi wao (wabunge wa jimbo) ndiyo watakaoridhia ama kukataa mkataba husika.  Baada ya hayo naona majimbo yakiongozwa na wananchi wakazi wa majimbo husika na wenye uchungu na maliasili za majimbo yao. Wanazitumia vilivyo kujiletea maendeleo kwa sapoti ya serikali kuu ambayo hutoa ruzuku kubwa kwa majimbo yenye rasilimali kidogo na ruzuku kidogo kwa majimbo yenye raslimali nyingi kutegemeana na vipaumbele vya serikali kuu.  Tena ninaona majimbo yakishindana kuleta maendeleo kila moja likitaka kupata maendeleo kama jingine na lenye maendeleo zaidi likitaka kudumu kuongoza kwa maendeleo. Magavana wa majimbo ndiyo baadaye watakuja kuaminiwa na wananchi wa nchi nzima kuongoza taifa kutokana ma mafanikio waliyoyapata majimboni mwao.  Mikakati yote hii inaliongezea taifa mapato mengi na imani kubwa kwa nchi wahisani na kuongeza misaada kwa nchi. Hili linaiwezesha serikali kuongeza kima cha chini cha mishahara hadi laki tatu na ushee kwa mwezi, kutoa matibabu bure, kutoa pembejeo za ruzuku kwa wakulima bure, kutoa ufadhili kwa wanafunzi wote wasio na uwezo kwenye elimu ya juu, kusomesha watoto wa Tanzania elimu ya msingi hadi sekondari bure.  Pia serikali inapata uwezo wa kuwekeza katika tafiti mbalimbali na uhamishaji wa teknolojia (technology transfer).  Hili linafanyika kwa kuwatuma vijana wazalendo na wenye vipaji maalum kusoma na kutafiti katika mataifa yaliyoendelea.  Wanaporudi tunawapatia nyenzo ili waweze kubuni zana bora zaidi na za kisasa za kilimo, mifumo ya kilimo cha kisasa cha umwagiliaji, mitambo ya kusafisha madini, utengenezaji wa bidhaa mbalimbali ikiwa ni pamoja na vipuri vya magari, vifaa vya umeme na elektroniki, viwanda vya kusindika mazao, n.k.  Muda si mrefu tuna viwanda vyetu vikubwa vinavyoweza kutengeneza bidhaa mbalimbali na muhimu duniani na hivyo kuongeza thamani ya bidhaa tunazouza nje.  Tukifikia hapo tayari tutakuwa katika nchi za Dunia ya Pili - Tumepaa kutoka Dunia ya Tatu.  Kwamba Mungu wa mbinguni atusaidie Watanzania kuiona vema njozi hii na kutambua mabadiliko yaliyo ndani ya uwezo wetu na hatimaye tukaamua kuyafanya na kutimiza ndoto zetu kama taifa - ndilo ombi langu, Amen. Makala hii imeandikwa na mwanaharakati wa mabadiliko anayesoma Chuo Kikuu cha Arusha.  Email: smwigamba@yahoo.comMob: 0784 815 499 au 0712 012 514</description>
					  <author>Marshy Abdu</author>
					  <pubDate>Wed, 03 Oct 2007 00:00:00 EAT</pubDate>
					  <subject />
					</item>

				

					<item>
					  <title>Msikimbilie kumshitaki Dk. Slaa</title>
					  <link>http://www.habaritanzania.com/blogs/42/Msikimbilie-kumshitaki-Dk.-Slaa</link>
					  <description>na Elishekia Isaac MWANASHERIA Mkuu wa kwanza mzalendo nchini, Jaji Mark Bomani, amewataka wanasiasa wanaotishia kwenda mahakamani kumshitaki Katibu Mkuu wa Chadema, Willibrod Slaa, kutokana na kuwashutumu kwa vitendo vya rushwa kutafakari upya iwapo kuna ulazima wa kuchukua hatua hiyo.  Bomani, mmoja wa wanasheria wanaoheshimika nchini, alitoa wito huo jana, wakati akizungumza na waandishi wa habari katika ukumbi wa mikutano wa Idara ya Habari (MAELEZO) jijini Dar es Salaam, kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu tuhuma za rushwa zilizotolewa na Dk. Slaa na viongozi wengine wa upinzani, takriban wiki mbili zilizopita.  "Kutokana na hali hii inayojitokeza, maombi yangu ni kwamba, tuwe wavumilivu wa kisiasa (political tolerance). Nawaomba ndugu zangu ambao wanatishana kushitakiana mahakamani wafikirie upya ulazima wa kufanya hivyo," aliasa Jaji Bomani.  Alisema rushwa ni tatizo kubwa katika jamii ambalo linapaswa kupigwa vita kwa nguvu zote, na kwamba malumbano ya namna yoyote yanayoweza yakayumbisha jitihada hizi za kukabiliana na rushwa hayana budi kuepukwa kwa nguvu zote.  Alionya kuhusu kuwapo kwa uwezekano mkubwa kwamba malumbano haya yanayoendelea yanaweza kukua na kufikia kiwango cha kuleta mfarakano na uhasama katika jamii iwapo yatazidi kiasi.  Aidha, mwanasheria huyo aliyepata kuchukua fomu za kugombea urais wa Tanzania kupitia CCM mwaka 1995, alikiri kuhusu kupamba moto kwa malumbano kuhusu suala zima la rushwa.  Katika hilo, alisema hali hii ya kupamba moto inachangiwa kwa kiwango kikubwa na maamuzi ya watu kupinga kuwapo kwa rushwa hapa nchini, wakati hali halisi inathibitisha pasipo shaka kwamba tatizo hilo lipo.  Bila ya kutaja majina ya watu, Bomani alizungumzia kuhusu suala zima la Dk. Slaa kutaja hadharani watu wanaotuhumiwa kwa rushwa, alisema sheria inatoa uhuru kwa mtu kutoa maoni yake ama kwa maandishi au kwa mdomo.  "Labda tu niseme kwamba litakuwa ni jambo la kushangaza kwa mtu yeyote kutoa hisia kwamba uhuru huu haupo kisheria au haufai. Uhuru huu upo na unapaswa ulindwe," alisema Bomani katika taarifa yake ya maandishi aliyoikabidhi kwa waandishi wa habari.  Kwa upande mwingine, Jaji Bomani aliwataka wananchi kuitumia Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa ya mwaka 2007 kukabiliana na vitendo hivyo kwa nguvu zote.  Akitoa mfano alisema chini ya sheria zilizopo, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) inao uwezo wa kumtaka kiongozi au mtumishi wa umma yeyote aeleze kuhusu mali zake zinazoonekana kutolingana na mapato yake halali.  Bomani anatoa kauli hiyo katika kipindi kisichozidi wiki moja tangu gazeti moja la kila wiki limkariri akisema kuwa hoja ya Dk. Slaa kuhusu tuhuma za rushwa zilikuwa ni legelege.  Katika hili, mwanasheria huyo alililaumu gazeti hilo kwa kumwekea maneno 'legelege' ambayo alisema hakuyatumia katika mahojiano yake ya maandishi aliyoyafanya na gazeti hilo linalochapishwa kila Alhamisi.  "Kwa mfano, sikumuonya Dk. Slaa na wala sikusema kuwa hoja zake ni legelege! Haya si maneno yangu, ni ya gazeti. Vilevile gazeti hilo limetaja jina la Zitto Kabwe, ambalo mimi sikulitaja katika mahojiano," alisema Bomani.  Katika taarifa yake ya maandishi aliyosema ndiyo yaliyokuwa maswali na majibu aliyoyatuma kwa gazeti hilo, inaonyesha kuwa Bomani aliandika kuwa: "Shida kubwa ninayoiona ni kwamba, baadhi ya shutuma zilizotolewa na Dk. Slaa na wenzake ni za kijumla mno."  Aidha, sehemu nyingine ya majibu yake hayo kwa gazeti hilo yanamkariri akisema kwa maandishi kuwa; Dk. Slaa na wenzake wana uhuru wa kutoa maoni yao kuhusu vitendo vya rushwa na ufisadi nchini.  Mwanasheria huyo pia amewalaumu wale wanaosema ni makosa kumtuhumu mla rushwa kabla ya kuwa na ushahidi wakati ukweli ni kwamba, sheria inasema bayana kwamba, mtu anayetuhumiwa kwa makosa hayo anahesabiwa kuwa mhalifu hadi hapo atakapojitakasa.  "Hivyo wanaosema kwamba ni makosa kumtuhumu mla rushwa mpaka kwanza ushahidi uwepo, wanaipotosha Sheria ya Kupambana na Rushwa. Sheria ya Rushwa ikitumiwa kikamilifu inaweza ikanasa wala rushwa wengi," anasema Bomani katika maandishi yake hayo, yaliyotumwa kama majibu kwa gazeti hilo.</description>
					  <author>Marshy Abdu</author>
					  <pubDate>Wed, 03 Oct 2007 00:00:00 EAT</pubDate>
					  <subject />
					</item>

				

					<item>
					  <title>Longido wataka mkataba uchimbaji madini utenguliwe</title>
					  <link>http://www.habaritanzania.com/blogs/41/Longido-wataka-mkataba-uchimbaji-madini-utenguliwe</link>
					  <description>na Ramadhani Siwayombe, Longido WANANCHI wa Wilaya ya Longido, mkoani Arusha, wameiomba serikali kutengua kibali cha uchimbaji wa madini cha Kampuni ya Mundarara Ruby Mining, kwa kuwa kampuni hiyo imeshindwa kuchangia maendeleo katika maeneo yanayozunguka mgodi huo.  Akizungumza kwa niaba ya wananchi wa Kata ya Mundarara, Diwani wa kata hiyo, Peter Sengui, wakati wa kikao maalumu na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Utawala Bora), Hawa Ghasia, alimwomba waziri huyo kufikisha kilio chao kwa Rais Jakaya Kikwete, ili afute mkataba huo.  Sengiu alimwambia Waziri Ghasia kuwa mkataba huo utaiwezesha kampuni hiyo kuchimba madini ya rubi yaliyopo katika kata hiyo kwa muda mrefu, huku wananchi wa wilaya hiyo wakiwa hawanufaiki na chochote kutoka katika mgodi huo.  Alisema hivi sasa madini ya rubi yana thamani kubwa nje kuliko hata dhahabu na yanapatikana kwa wingi katika mgodi huo, lakini kampuni hiyo haichangii kiasi chochote katika wilaya hiyo.  Aidha, Diwani wa Kata ya Kitumbeine, Joseph ole Saadira, alimwomba Waziri Ghasia kuangalia uwezekano wa kupeleka watumishi wa afya haraka katika wilaya hiyo, kwani licha ya kuhamasisha wananchi katika ujenzi wa zahanati lakini kumekuwa na ukosefu wa wahudumu.  Alitoa mfano wa kata yake ambayo ina vijiji vinne wamejitahidi kujenga zahanati katika kila kijiji, lakini ni zahanati moja tu ndiyo inafanya kazi na nyingine tatu zimefungwa kutokana na ukosefu wa wahudumu.  Alitaja vijiji vilivyoathirika na tatizo hilo ni Kijiji cha Noondoto, Elang'atadabashi, na Kitumbeine, huku Kijiji cha Kiseriani pekee ndicho kilicho na zahanati, hivyo kulazimu wananchi kutembea zaidi ya kilometa 40 kuifuata zahanati hiyo kupata huduma.  Waziri Ghasia, yupo katika ziara maalumu ya kutembelea wilaya zote za Mkoa wa Arusha kuzungumza na watendaji wa serikali na wa chama, kutoa ufafanuzi na kutoa maelekezo juu ya matumizi ya bajeti ya serikali ya mwaka huu.</description>
					  <author>Marshy Abdu</author>
					  <pubDate>Wed, 03 Oct 2007 00:00:00 EAT</pubDate>
					  <subject />
					</item>

				

					<item>
					  <title>Kwa nini tunawapinga?</title>
					  <link>http://www.habaritanzania.com/blogs/40/Kwa-nini-tunawapinga%3F</link>
					  <description>   M. M. Mwanakijiji     TAIFA letu liko katika kipindi cha mpito. Kipindi cha kutoka mawazo ya chama kimoja kuelekea mawazo ya vyama vingi, na kutoka ukiritimba wa hoja za chama kimoja kwenda kwenye wingi wa hoja za vyama na vyanzo vingi.  Kiini cha kipindi hiki cha mpito ni mabadiliko makubwa ya kiteknolojia hususan kuenea na kusambaa kwa mtandao wa kiintaneti na upatikanaji wa simu za mkononi. Mabadiliko haya yamechangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya kisiasa ambayo hivi karibuni yamekuwa yakiwasha moto wa kizalendo ndani ya mioyo ya Watanzania.  Katika hili CCM wamechelewa na wako nyuma. Tatizo lao kubwa lililowafikisha walipo sasa ni kujiamini kuwa &#34;ushindi wao wa kishindo&#34; wa 2005 umewapa leseni ya kusema na kufanya lolote kwani wao ndiyo &#34;chama kinachopendwa&#34; ni &#34;safi&#34;, na &#34;wana ridhaa ya wananchi&#34;.  Walipomfungia Zitto kushiriki vikao vya bunge kwa kosa la &#34;kusema uongo&#34;, walijihukumu wenyewe na sasa wanalipa gharama ya hukumu hiyo. Kwa miongo minne na miaka sita sasa, CCM na viongozi wake hawajawahi kupata changamoto kama wanayoipata sasa, na bila ya shaka &#34;wakulu&#34; wa chama hicho wanajiuliza &#34;tumekosea wapi?&#34; na bila ya shaka wanajiuliza &#34;kwanini tunapingwa namna hii? Hatua ya kwanza kutatua matatizo yoyote yale ni kukubali kwanza kuwa kuna tatizo. CCM hadi hivi sasa hawajakubali kuwa wanakabiliwa na tatizo au matatizo licha ya ushahidi wote uliopo.  Matukio ya rushwa, kashfa za mikataba, ukiritimba wa chama n.k. ni miongoni tu mwa matatizo tunayoweza kuyataja hadharani na kwa haraka. Kwanini wananchi wanawapinga? Kwanini watu hawaogopi tena na wanaanza kuwahoji? Kwanini hadi vijijini wanakijiji wenzangu wameanza kuuliza &#34;maswali ya ziada&#34; ambayo huko nyuma majibu yake yalikuwa &#34;yanafikirika?&#34;.  Tunawapinga kwa sababu moja kubwa - tunatofautiana nao. Msingi wa kulumbana na serikali na kufunua na kuchambua matendo yao ni tofauti iliyopo kati yetu na wao. Tofauti hiyo ni tofauti ya msingi (fundamental difference). Ni tofauti inayolingana na tofauti ya rangi nyeusi na nyeupe, usiku na mchana, mvua na jua, na Mashariki na Magharibi. Tofauti hiyo kubwa inatokana na tofauti katika mambo yafuatayo:  Tofauti ya kimtazamoWakati CCM bado wanaiangalia Tanzania kwa mtazamo wa &#34;wao ni watawala wasiopingika&#34; na sisi wengine tumeanza kuiangalia Tanzania kwa mtazamo wa &#34;CCM ni watawala wanaopingika&#34;. Katika hili wao wanapozungumza au wanapotenda sisi tunaangalia na kupima wanachozungumza na wanachotenda. Wanapotoa maelezo ya &#34;kihuni&#34; sisi tunawaambia kama maelezo yao ni &#34;ya kihuni&#34; hilo linawashtua!   Tofauti ya maoni   Wakati wao huko nyuma walijiambia kuwa maoni yao ndiyo maoni pekee ya kusikilizwa Tanzania, siku hizi wanashtuka kuwa maoni yao yana thamani kiduchu na yanachambuliwa kama maoni mengine yoyote yale. Huko nyuma walipoitisha waandishi wa habari au kutoa &#34;taarifa kwa waandishi wa habari&#34; basi mjadadala uliisha. Sasa hivi, mjadala hauishi kwa vile &#34;Rais kasema&#34; au &#34;Waziri Mkuu kasema&#34;. Wasipotoa majibu ya kueleweka au majibu yenye utata, watarajie kuwa watu watauliza maswali ya ziada. Ule ukiritimba wa mawazo ambao CCM ilikuwa nayo kwa muda mrefu kiasi cha kuamini kuwa wao pekee ndiyo wenye mawazo bora katika kuongoza taifa letu leo, unathibitishwa kuwa haukuwa na msingi wowote ule. Kashfa zinazowaandamana viongozi wake na watendaji wake ni ushahidi wazi kuwa kipindi cha utawala wa mawazo ya CCM kimekwisha na kipindi kipya cha mwamko wa kimawazo kimefika.   Tofauti ya mwelekeo   CCM inataka kuongoza kama ilivyoongoza huko nyuma na kwenda ilikotaka kwenda miaka 20 iliyopita. Inasikitisha kuwa kwa chama kilichowahi kuwa cha &#34;mapinduzi&#34; leo hii kinashindwa kubadilika kwa haraka na kwenda na wakati mpya wa machipuko mapya ya kisiasa yanayoendelea Tanzania. Kiini cha machipuko hayo ni mchango mkubwa wa waandishi na wajenga hoja mbalimbali ambao siku za hivi karibuni wamefungua kwa namna ya pekee mawazo ya Watanzania kuangalia ni wapi tunataka kwenda na ni wapi tunapaswa kwenda. Uzembe, kulindana, kufichana na kubebana kulikokuwa kunafanywa na CCM kwa muda mrefu sasa kumeanza kuwatokea puani. Leo hii walipodhania kuwa &#34;orodha ya ufisadi&#34; ya muungano wa upinzani ilikuwa ni propaganda za kuchafuliana majina, na ambayo inapaswa &#34;kupuuzwa&#34;, sasa wanajuta kwanini hawakuitilia maanani, na waliotajwa mmoja mmoja wanaanza kujaribu kujitetea na kati yao wengine hawajui kama ni waadilifu wamebakia kuwa na &#34;imani&#34; kuwa wao ni waadilifu. Kuchanganyikiwa huku ni jambo jipya, na ni mwanga katika chumba chenye giza! CCM wamechanganyikiwa. Hata hivyo, huu ni mwisho wa CCM na anayedhania kuwa CCM imefika mwisho ni bora aamke. CCM bado ina uwezo na nia ya kufanya mapambano haya ya kifikra na kisiasa. Hata hivyo gharama kubwa itabidi wailipe kuweza kurudisha imani kwa wananchi. Sehemu kubwa ya gharama hiyo inahusu uwazi, ukweli, na kujisafisha. Haitoshi kukanusha tuhuma au kuzipuuzia. CCM ijiangalie tangu ndani na kuona ni wapi kuna udhaifu na ni wapi kunakovuja kiasi cha kuhitaji kutengenezwa mara moja. Kwa kadiri ambavyo viongozi wa CCM bado wako kwenye hatua ya kukana ndivyo hivyo fikra za mabadiliko zinavyozidi kukita katika mioyo ya watu. Kwenye hili CCM wameshindwa kuongoza na sasa wanajikuta wanafuata. Ni kiburi chao na ubabe wao ndio unaowaumbua sasa, na ni shimo hili ambalo wao wenyewe wamelichimba wakitumaini wapinzani watatumbukia. Bahati mbaya ni wao walioanza kutumbukia na walipotarajia kuwa wapinzani wataanza kuwafukia, wanajikuta ni wao wenyewe ndio wanaoanza kufukiana huku wapinzani wakikaa pembeni wakicheka kuwa &#34;CCM wamelikoroga wenyewe na sasa wanalinywa&#34;. Kwa kadiri siku zinavyoendelea ndivyo hivyo vuguvugu la mabadiliko ya kisiasa linavyozidi kupamba moto. CCM wako kwenye kona ya ulingo wa kisiasa huku wapinzani wakiendelea kurusha makombora ya ngumi. Kama wapinzani wanadhania kuwa CCM imeanguka chini na iko tayari kwa 'knockout'.. wasijidanganye. CCM itajikusanya na kujiandaa kujibu mapambano kwa nguvu na kwa haraka. Wakosoaji tujiandae for the 'final showdown! I'm ready... are you?' </description>
					  <author>Marshy Abdu</author>
					  <pubDate>Wed, 03 Oct 2007 00:00:00 EAT</pubDate>
					  <subject />
					</item>

				

					<item>
					  <title>Wapinzani ndio wenye uchungu na taifa hili?</title>
					  <link>http://www.habaritanzania.com/blogs/39/Wapinzani-ndio-wenye-uchungu-na-taifa-hili%3F</link>
					  <description>   Gervas Zombe     MCHAKATO wa kuboresha maisha kwa Watanzania unaoendelea miaka hadi miaka, ni kama hadithi inayofurahisha, kuhuzunisha na kufikirisha pia.  Wanaofuatilia ahadi za viongozi, hotuba za viongozi, wanasiasa na hata wabunge wakiwa bungeni watakubaliana nami.  Wingi wa kauli na ahadi za viongozi tayari ni maendeleo tosha kabla hata ya kufanya lolote.  Tumesikia kutoka kwa viongozi na wanasiasa nahau za kila namna, methali, vitendawili, hadithi, kejeli na hata ngojera, lakini bado dhiki za Watanzania wengi ziko palepale.  Wanasiasa na viongozi wa vyama na serikali kauli na matamshi yao, yanaonekana yanashabihiana kuwa na lengo moja la kuboresha maisha kwa Watanzania. Lakini utekelezaji wake kwa vitendo, hapo ndipo kila mmoja anatafuta njia yake.  Na kutokana na njia hizi kuwa nyingi, zinazaa mijadala isiyo kwisha. Huku wananchi wengi wakiogelea kwenye dimbwi la umaskini. Na inaonekana walio nje ya mfumo wa uongozi wanauona udhaifu wa walio ndani kwa jicho pevu. Je, jicho hilo pevu linawasaidia wao au wananchi?  Haya yote yanafanyika huku wananchi walio wengi maskini wanaendelea kutaabika. Wakipakwa mafuta kwa mgongo wa chupa kupitia vyombo vya habari.  Mwananchi mwenye njaa, anachohitaji ni chakula tu na si wingi wa maneno, nyaraka wala hotuba. Mgonjwa hospitalini anachohitaji ni huduma ili apone na si maneno wala pole za huzuni. Maana maneno hayatendi!  Inawezekana kumsaidia mgonjwa bila kuongea maneno mengi. Mtu mwenye njaa ukimpa chakula bila kusema neno hatashiba? Na kwa utamaduni wetu Waafrika, anayepatiwa huduma ndiye anastahili kutoa shukrani.  Lakini kwa sasa jamii, wakiwemo baadhi ya viongozi hawawezi kutoa huduma bila kuwepo vyombo vya habari au bila kuonekana kwamba wametoa huduma.  Wanachofanya hapa ni kwa manufaa ya nani? Vivyo hivyo, wakifanya ovyo, vyombo hivyo hivyo vya habari vinaonyesha udhaifu huo. Kama tunavyoendelea kuona.  Imenishangaza pia, siku za hivi karibuni. Masuala nyeti yanayogusa masilahi ya nchi mara nyingi yanachimbuliwa na wabunge wa upinzani.  Mfano mzuri ni hili sakata la ufisadi na hoja ya Buzwagi lilikoanzia na linaloendelea. Wanaopiga kelele ni wabunge wa upinzani na viongozi wao. Kwanini?  Hili linaleta maswali mengi yasiyo na majibu. Je, inawezekana wabunge wa upinzani wana uchungu na nchi hii kuliko wale wa chama tawala? Au wana agenda ya siri tusiyoijua?  Au kwa sababu wako nje ya uwanja hivyo wanauona vizuri mpira kuliko wachezaji waliomo ndani?  Lakini historia na uzoefu unaonyesha, kuna wabunge wa sifa hizi waliokuwa machachari pindi wako upinzani lakini baada ya kurudi chama tawala sasa hawasikiki. Je, kuna nini kilicho nyuma ya ukimya wao?  Nilivunjwa moyo na majibu dhaifu ya maswali nyeti ya wabunge kwa Waziri wa Miundombinu. Sijui kama ni mimi tu lakini pia wabunge wengi walivunjwa moyo, ndiyo maana wengine wakapendekeza muda uongezwe ili wapatiwe majibu mazuri.  Wengine walifikia hata kutishia kufanya kampeni hasi dhidi ya kiongozi huyo. Je, kama wabunge hawakuridhishwa inakuwaje wananchi wenyewe wanaozionja shida hizo warithike? Siamini kama wangekuwa wanajua wangerithika na majibu hayo.  Inawezekana wingi wa maneno bila vitendo ni miongoni mwa virusi vinavyo itafuna nchi hii. Na machungu ya dhiki na shida za wanyonge walio wengi haziwahusu viongozi hao wanaopigia siasa hata masuala ya muhimu.  Kama unakula na kushiba, unalala pazuri, unatembelea gari la kifahari, tena unapata mafuta bure, utaguswa kweli na shida za wananchi walio vijijini au maporini huko? Inawezekana aliyeshiba kumjua mwenye njaa? Ni wachache na wateule.  Lakini utekelezaji wa miradi yote ya maendeleo unategemea fedha ambazo wananchi hao hao ndio waliolipa kodi.  Pamoja na kuwa wanalipa kodi na wao kuwa ndio tabaka la wazalishaji, bado dhiki na shida zinawaandama kweli kweli.  Tabaka dogo lisilozalisha ndilo linalofaidika na mapato yanayozalishwa na wanyonge pamoja na rasilimali za wanyonge hawa wengi.  Jaribu kufikiri. Nani ana kazi kubwa kati ya mkuu wa wilaya na daktari wa wilaya mwenye dhamana ya kuokoa maisha ya watu kwa kufanya upasuaji bila kuchoka hadi usiku wa manane?  Lakini uliza mshahara wa daktari, huzuni tupu! Tutayaota maendeleo hadi lini pamoja na wingi wa rasilimali zetu?  0773 - 960606. </description>
					  <author>Marshy Abdu</author>
					  <pubDate>Wed, 03 Oct 2007 00:00:00 EAT</pubDate>
					  <subject />
					</item>

				

					<item>
					  <title>Serikali yamjibu Slaa</title>
					  <link>http://www.habaritanzania.com/blogs/38/Serikali-yamjibu-Slaa</link>
					  <description>na Mwandishi Wetu  WIKI mbili tangu wapinzani watoe tuhuma nzito za rushwa dhidi ya viongozi waandamizi serikalini na wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), serikali imetoa tamko ikitoa majibu yake.  Serikali katika tamko lake hilo lililotolewa kwa upendeleo maalumu kwa vyombo kadhaa vya habari leo hii, inakanusha tuhuma takriban zote zilizotolewa na wapinzani, wakiongozwa na Katibu Mkuu wa Chadema, Dk. Willibrod Slaa.  Katika tamko lake hilo, serikali, inaziita tuhuma zote za Slaa, kuhusu Benki Kuu (BoT), Kampuni ya Tangold na nyinginezo kuwa ni za kizushi na ambazo zimetolewa pasipo kufanyika kwa utafiti wa kutosha.  Kuhusu Benki Kuu, serikali katika taarifa yake hiyo inasema; "Baada ya kufuatilia kwa kina kuhusu tuhuma hizi, serikali inatoa tamko kuwa ni za uzushi na upotoshaji wa makusudi wa ukweli. Aidha, tuhuma kuhusu majina ya wanaodaiwa kuingiza fedha za kigeni nchini na baadaye kulipwa na Benki Kuu, ni vyema ieleweke kuwa wadai wanaozungumziwa hawakuingiza fedha za kigeni nchini, bali walilipa fedha za Kitanzania kwa iliyokuwa Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) kama malipo ya kuagiza bidhaa kutoka nje katika miaka ya 80."Aidha, katika hilo serikali inasema BoT ilishindwa kufanya malipo hayo wakati huo, baada ya kupokea fedha kutoka NBC kutokana na kutokuwa na fedha za kigeni enzi hizo.  Bila ya kutaja wakati, serikali inaeleza katika taarifa yake hiyo kuwa, baada ya tuhuma za uwezekano wa kuwepo kwa malipo yasiyo sahihi kupitia akaunti hii kujitokeza, ilimuagiza Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, kuteua mkaguzi wa kimataifa (International Auditing Firm) kwa utaratibu wa wazi wa zabuni ili kufanya uchunguzi maalumu na kuwasilisha taarifa yake serikalini.  "Uchunguzi huo unaendelea na serikali inasubiri ukamilike ili kuamua hatua muafaka. Mhe. Dk. Slaa na wenzake wanafahamu vizuri hatua zilizochukuliwa na serikali katika suala hili, kwani serikali ilitoa taarifa kwenye vyombo vya habari na imetoa maelezo ya hatua za utekelezaji wake bungeni mara kadhaa," inasomeka sehemu ya taarifa hiyo.  Kuhusu madai mengine ya wapinzani kwamba, ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali (CAG) kuhusu hesabu za Benki Kuu kwa mwaka 2005/06 kuonyesha mapungufu makubwa, serikali katika tamko lake inasema imepitia taarifa ya ukaguzi wa hesabu hizo, lakini haikuona hoja za ukaguzi zinazodaiwa kutolewa na CAG.  Mbali ya hilo, serikali inasema, taarifa ya hesabu za Benki Kuu kwa mwaka 2005/2006, ziliwasilishwa katika Kamati ya Fedha na Uchumi ya Bunge mapema mwaka huu na kukubaliwa na kamati hiyo na kwamba (kamati hiyo) iliwasilisha taarifa yake bungeni na Bunge likairidhia.  Serikali inaeleza katika tamko lake hilo kwamba, kwa nyakati tofauti, Kamati ya Fedha ya Uchumi ya Bunge pamoja na Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) zimepata nafasi ya kutembelea miradi ya ujenzi wa majengo ya Benki Kuu ya Dar es Salaam na Zanzibar ili kupatiwa maelezo ya kutosheleza, kuhusu utekelezaji na gharama za miradi hiyo, hali ambayo inaifanya hoja ya Slaa kuonekana kuwa ni ya kubuni na yenye nia mbaya.  "Nia mbaya ya Mheshimiwa Dk. Slaa na wenzake katika kutoa tuhuma hizi, inadhihirishwa na upotoshaji wa makusudi wa takwimu zilizo katika hesabu hizi, ili kupindisha ukweli. Kwa mfano, anaituhumu Benki Kuu kutumia shilingi 522,459,255,000 (Bilioni 522.5) kwa ujenzi wa "Twin Towers" mjini Dar es Salaam. Ukweli ni kwamba kiasi hicho ni thamani ya mali zote za kudumu za Benki Kuu hadi tarehe 30 Juni, 2006. Taarifa hizi ziko wazi katika nyaraka zilizowasilishwa bungeni na zinaweza kuthibitishwa na mtu yeyote kutokana na Taarifa ya Benki Kuu ya Mwaka 2005/06 iliyosambazwa kwa umma," inasema taarifa hiyo ya serikali.  Aidha, serikali katika tamko lake hilo, imewatetea watumishi wake wanaotajwa kuwa miongoni mwa mafisadi katika orodha ya Dk. Slaa, ikisema kuwa kwao wakurugenzi katika Kampuni ya Tangold Limited, kunatokana na uamuzi wa serikali na kuwa kampuni hiyo inamilikiwa kwa asilimia 100 na serikali.  "Wakurugenzi wa Tangold wameteuliwa na Serikali ya Tanzania, wote ni watumishi wa umma ambao ni pamoja na wale ambao Mheshimiwa Slaa anawatuhumu katika tamko lake.  "Watumishi hao wameteuliwa kuwa wakurugenzi wa Tangold kutokana na nafasi zao katika utumishi wa umma. Kuwa mkurugenzi katika chombo cha umma hakusababishi mgongano wa kimaslahi, kwani ni sehemu ya utumishi wa umma," inasomeka sehemu moja ya tamko hilo la serikali.  Mbali ya hilo, tamko hilo la serikali linasema wakurugenzi hao wa Tangold hawana hisa katika kampuni hiyo, kwa sababu hisa zake zote zinamilikiwa na Mfuko wa Udhamini wa Maendeleo (Tanzania Development Trust) kwa niaba ya Watanzania wote.  "Kwa maana hiyo, wakurugenzi wa Bodi ya Kampuni ya Tangold hawana maslahi yoyote binafsi zaidi ya kusimamia maslahi ya Watanzania," inasema taarifa hiyo.  Serikali katika tamko lake hilo, imekanusha madai mengine ya wapinzani, kwamba kulikuwepo na shinikizo kwa Kampuni ya Alex Stewart (Assayers) Government Business Corporation ya Washington, Marekani, kupewa kazi ya kukagua hesabu za kampuni za uchimbaji dhahabu.  Serikali katika tamko lake inasema, kampuni hiyo ilipatikana kwa kuzingatia sheria na kanuni za ununuzi wa umma na hakukuwa na shinikizo lolote.  Hata hivyo, kuhusu tuhuma zilizoelekezwa katika sekta ya madini, serikali katika tamko lake hilo imesema kutokana na unyeti wa suala lenyewe, inakusudia kulitoa tamko rasmi kuhusu jambo hilo katika taarifa nyingine maalumu kwa lengo la kuwaeleza wananchi ukweli kuhusu sekta hii.  "Sekta ya madini ni muhimu sana kwa uchumi wa nchi yetu. Kutokana na unyeti wa sekta hii na tuhuma nzito zilizotolewa dhidi ya serikali juu ya sekta hii, serikali inaona ni vyema kutoa maelezo ya ufafanuzi zaidi. Hivyo, serikali itatoa taarifa maalumu na ya kina kuelezea wananchi juu ya sekta hili," linasema tamko hilo.  Akizungumzia hoja za serikali katika tamko lake hilo, Dk. Slaa aliyejibu kwa maandishi kipengele kwa kipengele, anasema majibu takriban yote ya serikali yana mapungufu makubwa na akasema bado alikuwa akisubiri hatua za kisheria ili akatoe ushahidi alionao kuhusu madai yake mahakamani.  Katika sehemu moja ya majibu yake, Dk. Slaa anaeleza kusikitishwa na tamko la serikali linalozungumzia uchaguzi wa mwaka 2005 na kushindwa kwa upinzani, kuwa ndiyo sababu kuu ya wapinzani kujaribu kuwahadaa wananchi ili wawachague wao siku zijazo.  "Hoja hii ni ya watu walioshiwa, na wamebaki na fikra mgando. Nani kati yetu kipindi chote hiki amezungumzia masuala ya uchaguzi? Ni kazi yetu ya kikatiba kuelezea Watanzania pale ambapo serikali imefanya makosa. Si kazi ya upinzani kuipigia makofi serikali. Kazi ya kambi ya upinzani duniani kote inajulikana. Na ndiyo maana tuko kikatiba," anasema Slaa katika majibu yake.  Aidha, Dk. Slaa anaitaka serikali kujieleza kwa wananchi ili ieleweke, badala ya kutafuta mchawi, na akasisitiza kuwa leo hii wananchi wanalalamika kila kona ya nchi maisha bora hayajaonekana, na kwamba vyama vya upinzani vina wajibu wa kuhoji kwa niaba ya wananchi kutaka kujua kuhusu rasilimali za taifa.</description>
					  <author>Marshy Abdu</author>
					  <pubDate>Mon, 01 Oct 2007 00:00:00 EAT</pubDate>
					  <subject />
					</item>

				

					<item>
					  <title>Menejimenti na na uongozi katika vijiji, mitaa</title>
					  <link>http://www.habaritanzania.com/blogs/37/Menejimenti-na-na-uongozi-katika-vijiji%2C-mitaa</link>
					  <description>WATANZANIA sote tunaishi kwenye vijiji na kwenye mitaa. Hivyo uongozi wa vijiji na mitaa ni muhimu kwa kila Mtanzania. Kama tujuavyo maofisa watendaji wa vijiji na mitaa ndiyo wasimamizi na waendeshaji wakuu wa shughuli za serikali za mitaa katika ngazi ya kijiji na mtaa, hivyo ni vema kwao kuelewa dhana ya misingi ya menejimenti ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi.  Lakini pia kwa vile Watanzania wote wanaishi vijijini na kwenye mitaa ni bora dhana hii ya menejimenti na uongozi ikaeleweka kwa wote.  Katika makala hii nitajadili mbinu za menejimenti na uongozi katika ngazi ya vijiji na mitaa. Zimetolewa tafsiri mbali mbali za maana ya menejimenti. Mfano, E.F.L Breach, katika kitabu cha 'Misingi ya Menejimenti' (Principles of Management) anaeleza kwamba menejimenti ni uwajibikaji katika usimamizi katika ofisi au kiwanda ili kufikia malengo fulani.  Naye Dynier katika kitabu chake kinachohusu 'Utawala wa Ofisi' (Office Administration) anaelezea kwamba menejimenti ni utaratibu wa utendaji kazi katika ofisi au kiwanda ili kufikia malengo fulani.  Tukizingatia tafsiri zote mbili zina uwiano kwa kiasi kikubwa, hivyo menejimenti ni utaratibu wa upangaji wa matumizi ya rasilimali zilizopo (watu, fedha, mitambo, majengo, ardhi, muda na kadhalika) utendaji kazi, usimamizi na uratibu wake ikiwa ni pamoja na uwajibikaji katika sehemu za kazi katika kufikia malengo au matarajio yaliyowekwa.  Utaratibu huu hujibu maswali kama:- Nini kitafanyika, lini na ni matokeo gani yanatarajiwa? Nani watafanya, watafanyia wapi na watafanya namna gani? Watatumia zana, vifaa, malighafi au fedha kiasi gani na zitatoka wapi? Usimamizi utafanyikaje na uwajibikaji na uratibu wa shughuli utakuwajie? Kila shughuli muhimu itachukua muda gani, na je, shughuli nzima itachukua muda gani kukamilika? Hivyo misingi ya menejimenti imegawanywa katika maeneo ya kupanga, kuratibu watumishi, kuongoza na kudhibiti.  Upangaji wa shughuli zitakazofanyika ni muhimu ili kufikia malengo kikamilifu. Hivyo ofisa mtendaji wa kijiji au mtaa lazima aweke mpango mzuri wa kutenda shughuli zake ili malengo yafikiwe. Na ni muhimu kuwa na watumishi wenye ujuzi ili kazi zifanywe ka ufanisi. Ofisa mtendaji wa kijiji au mtaa si mwajiri, ni msimamizi tu wa utendaji wa watumishi katika eneo lake ili wote wafanye kazi kama timu moja.  Vivyo hivyo, watendaji hawa inabidi waratibu utendaji kazi wa wananchi ili wafanye kazi za kujenga taifa kwa ukamilifu. Ofisa mtendaji wa kijiji/mtaa, kama kiungo cha idara zote za halmashauri, anatakiwa kuzielewa barabara sifa za kiongozi bora na kuzihusisha na shughuli zake za kila siku ipasavyo. Uongozi ni mahusiano kati ya viongozi wa ngazi ya juu na wale wanaoongozwa. Wenye kuongozwa ni vema wapate kiongozi mzuri mwenye uwezo atakayehakikisha malengo ya ofisi/kiwanda yanafikiwa. Kwa hiyo, ofisa mtendaji wa kijiji/mtaa ni lazima awe ni mtu mwenye uwezo wa kuongoza ili malengo ya halmashauri, kata, kijiji na mtaa yafikiwe.  Pia ikumbukwe kwamba udhibiti ni muhimu katika utendaji kazi kwani unasaidia kuona kama kila mtumishi/mfanyakazi ametekeleza majukumu yake ipasavyo. Udhibiti unasaidia kufikia malengo yaliyowekwa. Mtendaji wa kijiji/mtaa anatakiwa adhibiti watumishi walio katika eneo lake ili kuona kama kila mmoja anatekeleza wajibu wake ipasavyo.  Mtendaji wa kijiji/mtaa, anayeifahamu kazi yake vizuri ni lazima awe na tabia ya kujiwekea utaratibu wa kutenda mambo, na baadaye kwa matumizi bora ya rasilimali zilizopo na kwa njia hii anaweza kupata ufanisi mkubwa zaidi.  Pia mtendaji bora wa kijiji/mtaa ni lazima awe na upeo wa kuunda vikundi na kuvikabidhi wajibu na majukumu ya kutekeleza malengo fulani. Faida ya mbinu hii ni kwamba mtendaji si lazima afanye kila kitu mwenyewe, bali anaweza kuwatumia watu alio nao. Baada ya kuunda vikundi vya kazi lazima kuweka uongozi wenye uwezo na wajibu wa shughulli hizo ili watoe usimamizi wa karibu. Vile vile, shughuli za usimamizi zinaweza kufanywa kwa kutumia uandishi wa taarifa za utekelezaji kwa vipindi maalum. Taratibu za usimamizi zinawajibisha watekelezaji.  Mipango, ratiba, makisio na taarifa mbalimbali ni mbinu za menejimenti katika kudhibiti shughuli za kiongozi. Njia hizi za udhibiti zinawezesha kupima utekelezaji na kulinganisha na malengo yaliyokusudiwa na kusaidia kueleza sababu za kushindwa kufikia malengo.  Mtendaji bora wa kijiji/mtaa ni lazima awasiliane na anaowaongoza kuhusu mambo yaliyokusudiwa kufanyika na pia lazima apate taarifa za utekelezaji. Mbinu ya mawasiliano inaweza kutumika kuwahamasisha wanaoongozwa kwa kutumia maelekezo ya mdomo au maandishi. Mtendaji anapaswa kuelewa kinachotendeka wakati wote na kuwafanya anaowaongoza waelewe kwamba anaelewa wanachofanya. Mawasiliano ni kigezo cha msingi katika kufanikisha malengo yote ya serikali.  Mtendaji bora wa kijiji/mtaa ni yule anayezingatia ushirikishwaji. Hii ni zana na mbinu ya msingi sana katika kufanikisha majukumu ya umma. Ushirikishwaji zaidi ya kutegemea kanuni na sheria rasmi hutegemea pia mwenendo wa kiongozi anayehusika. Ni muhimu pia wanawake washirikishwe kikamilifu katika uongozi - hii ni kwa sababu idadi yao ni kubwa na ndiyo wazalishaji wakubwa. Mbinu za kuwashirikisha ni pamoja na kuwahamasisha wajitokeze kugombea nafasi mbalimbali za uongozi na kuwapa majukumu, changamoto na misaada.  Ikumbukwe kwamba kuongoza ni kuonyesha njia, kutanguliza na kuelekeza katika utekelezaji wa majukumu ya umma. Kuongoza ni kujenga moyo wa pamoja miongoni mwa wanaoongozwa na kuwahamasisha ili watekeleze yale yaliyokusudiwa. Ili kiongozi aongoze, lazima apate wafuasi ambao wanamkubali na kumfuata. Hivyo, ni jukumu la kiongozi kujenga mazingira mazuri mahali pake ili kuhakikisha kuwa anakubalika.  Kuna aina mbali mbali za uongozi: Kuna uongozi wa kiimla, hii ni aina ya uongozi ambao mkubwa hutoa amri na kutekelezwa na anaowaoongoza bila ya wao kutoka kauli yeyote. Aina nyingine ya uongozi ni uongozi huria, aina hii hutoa madaraka makubwa kwa wanaoongozwa kufanya kila watakacho bila ya maelekezo yoyote kutoka kwa viongozi. Lakini sisi hapa uongozi tunaofuata ambao maofisa watendaji wa vijiji na mitaa wanalazimika kufuata ni uongozi wa kidemokrasia.  Uongozi huu umezingatia kwamba wanaoongozwa wanao uwezo wa kujiamulia mambo yanayowahusu. Kwa hiyo, kiongozi huwashirikisha na kuwashawishi wanaoongozwa wachangie kwa mawazo na vitendo mambo ya kufanya. Pale ambapo hawajaelewa, kiongozi huwaelimisha na kuwashauri mpaka watakapokubali.  Uongozi wa kidemokrasi tofauti na ule wa kiimla, unalaumiwa kwa kufanya mambo polepole na unachelewesha maamuzi. Uongozi huu una faida kwamba watu wakishakubaliana na jambo linalohusika wanalitekeleza hata wakati msimamizi hayupo maana tabia ya kulitekeleza imekuwa ndani ya mioyo yao.  Hivyo ili kupata ufanisi wa hali ya juu katika mfumo wa serikali za mitaa ni muhimu maofisa watendaji wa vijiji na mitaa kuzingatia na kufuata mbinu za menejimenti na uongozi, kwani wao ndiyo wasimamizi na watekelezaji wakuu wa shughuli za serikali za mitaa katika ngazi ya kijiji na mtaa.</description>
					  <author>Marshy Abdu</author>
					  <pubDate>Mon, 01 Oct 2007 00:00:00 EAT</pubDate>
					  <subject />
					</item>

				

					<item>
					  <title>Tanzania bila Kikwete, Warioba inawezekana</title>
					  <link>http://www.habaritanzania.com/blogs/36/Tanzania-bila-Kikwete%2C-Warioba-inawezekana</link>
					  <description>"TUNAWANYONGA vibaka na kuwachagua wezi wakubwa kuwa viongozi wa umma." Kauli hii ilitolewa na mtumwa wa Kigiriki, Aesop, aliyeishi kati ya miaka 620 na 560 Kabla ya Kristo.  Aesop alifariki dunia miaka ipatayo 2,500 kabla ya Jaji Joseph Sinde Warioba, aliyewahi kuwa Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Tanzania.  Mtumwa huyu wa Kigiriki ana ujumbe mzito kwa Watanzania wa leo. Kwangu mimi, ujumbe huu ni mzito kuliko kauli ya Jaji Warioba wiki hii katika mkutano wake na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam.  Labda inaonekana ajabu kumlinganisha mtumwa na waziri mkuu mstaafu! Lakini hekima haina cheo. Mang'amuzi ya maisha yametudhihirishia kwamba wakati mwingine watu wasio na madaraka wana hekima kuliko hao wanaotawala.  Kosa tunalofanya, mara nyingi, ni kudhani kwamba mtu akipewa uongozi anapewa na hekima.  Hekima kuendana na uongozi imetokea mara chache maishani; na baadhi ya viongozi waliokuwa na hekima hawakuipatia madarakani. Walikuwa nayo awali, na mahali pengine, ndiyo iliyowashawishi watu kuwapa nafasi hizo za uongozi.  Tanzania imeshasahau enzi hizi, si katika uongozi wenye hekima tu bali pia uongozi unaozingatia uadilifu. Waadilifu tuliokuwa nao wamekufa, wengine wanaendelea kufa; hata waliobaki, tuliokuwa tunawategemea, wameanza kutukatisha tamaa.  Kwa nini nimemkumbuka Aesop? Nimesoma alichosema Jaji Warioba akiwalaumu wananchi wanaotoa shutuma na tuhuma kwa viongozi, wasaidizi wao na wastaafu. Vyombo vya habari vimemnukuu Warioba akisema:  "Unapomtaja rais kama fisadi unakuwa na unataka kufanya wananchi wakose imani na serikali yao, suala ambalo ni hatari, wananchi watakimbilia wapi kama wanayetaka kumkimbilia naye anachafuliwa?... Mengine yanashitusha. Umoja wa nchi hii unaweza kufika mahali pabaya. Yaani rais anaitwa fisadi kwa sababu hizi na zile tu.  Huyu ni mwanadamu kama wengine, lakini ndiyo symbol (alama) ya taifa, ukishamwita fisadi, na unakwenda unazungumza hivyo, hakuna uongozi wa taifa.  Hata Mkapa aliyemtangulia anaitwa fisadi, hivi hivi tu, habari hizi zinaleta picha gani? Kwamba alijitajirisha yeye na ndugu zake katika miaka yake 10. Mkapa kama binadamu alikuwa na weakness zake, lakini kwa nchi hii huwezi kufuta historia yake.  Watu wameacha kushughulikia matatizo ya wananchi, mambo ya msingi ya wananchi. Kwa mfano, mwaka jana, tumepata tatizo la chakula na umeme, lakini badala ya kuzungumzia jinsi ya kulikabili mwaka huu, watu wako busy kuzungumzia mambo ya uongozi. Wanazungumzia nani fisadi, kutueleza mambo yao ya uongozi. Vipaumbele vyetu vinaanza kupotoshwa. Maendeleo hayawezi kuletwa na viongozi na serikali.  Yataletwa na wananchi, serikali inatunga sera tu na kuzisimamia."Hii ni hekima mpya ya mzee Warioba. Ni wosia anaowapa Watanzania. Nimemsoma Warioba nikamkumbuka mlezi wake kisiasa, Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere.  Nikaona jinsi baadhi ya wanafunzi wake wanavyosahau mafundisho yake kwa kasi kubwa, na wanavyobadilika badilika kila kukicha na kupuuza misingi aliyowaachia. Walisema wangemuenzi. Nasi tunashuhudia jinsi wanavyomuenzi kwa kejeli.  Huyu si Warioba tunayemjua. Warioba ni mtu ambaye alistahili kupelekewa rufaa zote za rushwa nchini. Si mtu wa kusimuliwa jinsi rushwa inavyotafuna nchi yetu. Si mtu wa kuelezwa kuwa wala rushwa wakubwa ni wale wenye nafasi kubwa katika uongozi wa jamii.  Si mtu asiyefahamu jinsi vita ya rushwa imetushinda kwa sababu serikali inashughulika na rushwa ndogo na kuziacha kubwa kubwa zikitamalaki. Warioba si mtu wa kusema vita dhidi ya rushwa si kipaumbele cha kitaifa. Huyu huyu ndiye amekuwa analalamika mara kwa mara kuhusu kukithiri kwa rushwa nchini. Lipi limemsibu?  Au anataka kutueleza kwamba amezeeka kiasi hicho? Ameanza kupoteza kumbukumbu? Au anaanza kupakaribia pale ambapo Mwalimu Nyerere alipakataa aliposema anang'atuka akiwa bado na 'akili nzuri?'Sioni mantiki katika kauli ya kiongozi mstaafu, mwanasheria aliyebobea, mtu anayeheshimika kimataifa kudai kwamba mjadala juu ya ufisadi na uongozi si kipaumbele cha taifa! Hizo huduma anazojadili, matatizo ya umeme anayozungumzia na mengine, yamegubikwa na rushwa ya wakubwa. Anatuambia tunyamazie hili, tuzungumzie utabiri wa hali ya hewa! Warioba amepata ufunuo mpya. Sasa anadhani kwamba viongozi hawawezi kuwa mafisadi. Anataka kutuambia kwamba hata tunapopata shaka juu ya uadilifu wa kiongozi, tunyamaze ili wananchi wasikose imani na kiongozi huyo.  Nani amemwambia kwamba ufisadi wa viongozi ni nyenzo ya kudumisha imani na amani ya wananchi? Mbona anajua mifano ya viongozi wengi, ndani na nje ya Afrika waliojitumbukiza katika ufisadi kwa kutumia nyadhifa zao? Kwa nini anadhani kwamba hilo haliwezekani Tanzania?  Warioba anakumbuka hotuba ya Mwalimu Nyerere katika mkutano wake na waandishi wa habari Hoteli ya Kilimanjaro mwaka 1995 kuhusu sifa za rais anayefaa?  Hivi Mwalimu alitoa wapi wasiwasi wake hadi akaanza kuzungumzia 'utakatifu wa Ikulu?' Mbona Warioba hakuamsha kidole kumpinga Mwalimu Nyerere aliposema 'kanchi kananuka rushwa?' Alidhani ni rushwa ya makarani wa mahakama?  Hivi Warioba na Kingunge Ngombale-Mwiru wanaanza kuwa na uwezo sawa wa kufikiri na kujadili masuala ya kitaifa - kwa kuchezea akili za Watanzania? Mwalimu Nyerere ameshafariki, lakini tunu zimebaki. Hivi hata baada ya kusoma kitabu cha Mwalimu Nyerere: 'Uongozi wetu na hatima ya Tanzania,' bado anataka tuamini kwamba uongozi wa nchi si kipaumbele chetu?  Nyerere huyo huyo ndiye alisema ili tuendelee tunahitaji mambo manne. Ardhi, watu, siasa safi na uongozi bora. Kinachojadiliwa hapa ni suala la uongozi bora. Warioba anasema si jambo la msingi kujadili uongozi unaohusishwa na ufisadi?  Anataka kutuaminisha kwamba umaskini wa Watanzania hauchangiwi kwa kiasi kikubwa na uongozi mbovu unaokumbatia ufisadi? Na hao wanaharakati wenye maisha bora anaowazungumzia, wanaishi maisha bora kuliko yake yeye? Tumwamini yeye tuwapuuze wao?  Watanzania wangetarajia Warioba awashauri watuhumiwa wajisafishe na wajiuzulu ili haki itendeke. Huu ndio uadilifu tunaoutarajia. Yeye na wenzake hao, walipaswa kujifunza katika tukio jingine la wiki hii lililotokea mkoani Kilimanjaro.  Mwinjilisti wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Kaskazini alituhumiwa kumbaka mwanafunzi wa kidato cha tatu na kumsababishia ujauzito. Hata kabla hajafikishwa mahakamani, uongozi wa kanisa lake umetoa tamko kwamba mwinjilisti huyo amesimamishwa kazi hadi hapo tuhuma dhidi yake zitakapofikia tamati.  Huyu ametuhumiwa tu. Hajahukumiwa. Watumishi wetu (viongozi) wanaotuhumiwa kwa ufisadi wanasema eti hawawezi kujiuzulu kwa sababu ya kutuhumiwa tu! Wanataka wakae ofisini mwetu wabadili mafaili na kuharibu kumbukumbu huku wanatafuta namna ya kutumia mamlaka yao kuathiri mwenendo wa upatikanaji wa haki! Hata bosi wao, hajawachukulia hatua. Wanakwenda mahakamani kupataje haki wakiwa madarakani?  Kama hawako pale kwa masilahi binafsi, kipi kinawazuia kujisafisha kwa kuachia ngazi? Kama Mwalimu Nyerere alivyowahi kuhoji na kutoa mfano wa mke wa mfalme, hata kama si kweli, 'kwa nini mke wa mfalme atuhumiwe?' Kwanini watuhumiwe wao si wengine? Wataturidhishaje kwamba ni waadilifu kama hawataki kukaa pembeni? Au wanadhani wakiondoka ofisini nchi inabomoka?  Warioba anasema: "Sikutumwa na mtu, simo katika siasa wala serikali, mimi ni mtu huru, hakuna mtu aliyenituma, nasema ninachokiamini."Napenda kuamini kwamba hakutumwa na mtu. Laiti angesema kuwa ametumwa. Tungemsamehe kwani tunajua kwamba mjumbe hauawi. Lakini kama hayo ndiyo mawazo yake, basi amejiingiza kwenye kundi jipya.  Na nikiyaunganisha na yale ya Kingunge Ngombale-Mwiru, sasa naanza kuelewa kwanini Nyerere alisema anang'atuka akiwa 'bado na akili nzuri.'Hayo mambo ya msingi kwa taifa ni yapi? Tutayafanikishaje? Huko tulikotoka tumekwama wapi?  Hivi bado Warioba anaamini kwamba 'rushwa ni adui wa haki,' halafu akiwa mwanasheria na kiongozi mstaafu, haoni uhusiano kati ya vurugu hizi anazoziogopa na haki isiyotendeka katika jamii yetu? Anaamini kwamba amani inawezekana bila haki? Na kama amani itatoweka, ni kwa sababu ya wanaosema 'tumeibiwa' au kwa sababu ya wale walioiba?  Warioba anaogopa kuona mtu muhimu kama rais akiguswa na tuhuma. Kwani Rais Jakaya Kikwete ni wa kwanza kuguswa?  Tena afadhali yeye kaguswa na tuhuma za zamani alipokuwa waziri. Mbona Warioba hakung'aka wakati mzee Ali Hassan Mwinyi aliporushiwa makombora?  Tena mengine yalirushwa na Mwalimu Nyerere akiwa amesimama mita 200 tu kutoka mlango wa ofisi ya rais! Mbona Warioba alikaa kimya?  Hivi Warioba anadhani kwamba Watanzania wa leo ndio wale aliokuwa anawatawala akiwa Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais? Anadhani wananchi wa leo wanapima ukweli kwa kutazama cheo cha aliyeutoa? Au anadhani hawana mamlaka ya kutoa 'hukumu' kwa uongozi ulioshindwa?  Bado anadhani wananchi wa sasa wanaweza kufugwa na kuchezewa akili, kwa kisingizio cha 'amani na utulivu?' Anadhani hawajui umuhimu wa nafasi ya rais kama nembo ya taifa na alama ya umoja wa kitaifa?  Na anadhani hawajui kwamba rais ni mtumishi wao na hapaswi kujizungushia watu wenye uadilifu wa mashaka au yeye mwenyewe kujihusisha katika mambo yatakayomletea kashfa kama hizi?  Watanzania wanajua. Lakini hawalazimiki kuumia kwa sababu ya kujua kwao. Wananchi wanataka viongozi wawe sehemu ya ufumbuzi wa matatizo ya taifa. Viongozi wakishiriki kusababisha matatizo yetu tutasema.  Wananchi wanajua pia kwamba wao na viongozi wao ni watu wa kupita, lakini taifa litadumu. Wanataka uongozi unaotazama mbele na kuweka misingi ya kudumisha taifa.  Wanajua kwamba viongozi wakijiingiza katika 'kutafuna nchi' nao watatatafunwa! Tusiwatishe wananchi kwa kusingizia amani na umoja. Tusiwalazimishe kuwa na imani na viongozi wasiojiaminisha.  Wananchi wanajua umuhimu wa rais, lakini wanajua kuwa maisha yao ni muhimu kuliko maisha ya mtu mmoja anayetukuzwa hata katika makosa. Wanajua kuwa yeye ni binadamu, atapita na taifa litabaki. Wanajua kuwa akishindwa yeye, wapo wengine wataweza.  Warioba asitudanganye wala kututisha kwamba bila rais fulani nchi hii haiendi. Nyerere alipotaka kung'atuka, watu wenye mawazo kama ya Warioba walimwendea kumshawishi aendelee, kwa kisingizio kwamba asingepatikana mwingine wa kuongoza Tanzania. Sasa yuko wapi?  Kwa hiyo, ni vema Warioba ajue kuwa tunatambua uwezo, udhaifu na mipaka ya viongozi wetu.  Ajue kwamba wananchi wanajua kuwa nguvu za rais leo ni sawa na mavazi ya mganga wa jadi. Ukimvua yale manyoya anayovaa kutisha na kutiisha wateja wake unagundua kuwa naye ni mtu wa kawaida kama sisi! Tena wakati mwingine viongozi wetu ni dhaifu kuliko sisi.  Warioba atambue kuwa kama wananchi wana haki ya kutokuwa na imani na Bunge, wana haki pia ya kutokuwa na imani na kiongozi mmoja mmoja - hata rais. Na katiba inawalinda.  Ajue pia hata viongozi wetu wanajua hilo, na ni waoga. Ndiyo maana wanatunga sheria za kuwalinda wakiwa madarakani na wakishastaafu. Hawatungi sheria hizi kulinda usafi wao, bali uchafu wanaoufanya wakiwa madarakani. Wananchi wa Tanzania hawawezi kukubali kufikishwa mahali pa kupiga makofi kushangilia uchafu wa viongozi wao kama Warioba anavyotaka kutulazimisha. Makosa yaliyofanyika katika nchi nyingine yamekuwa somo kwetu.  Warioba ajue kuwa kila mtu huandika historia yake mwenyewe. Wala hakuna anayeweza kuifuta. Hivyo, historia ya Rais mstaafu Benjamin Mkapa, kwa mfano, imeshaandikwa na inaendelea kuandikwa. Imejaa mengi; mazuri na mabaya. Wanaotaka kuzungumzia mazuri yake waseme. Lakini tusiwazuie wanaotaka kuzungumzia mabaya yake, ambayo tunapaswa kuyatumia kama somo, ili wengine wasianguke katika mtego ule ule.  Hata historia ya Warioba imeshaandikwa na inaandikwa. Na sasa ameongeza ukurasa mpya katika historia yake, kwa tamko hili la wiki hii.  Viongozi wetu ni binadamu. Wana makosa. Mengine ni ya makusudi, mengine ni ya bahati mbaya. Mengine wamesababishiwa, na mengine wameyatafuta wenyewe, tena kwa ushawishi wa hoja na kwa nguvu ya madaraka yao - na kwa tamaa zao. Mengine wanayafanya kwa dharau na jeuri, wakizitegemea sheria zinazolenga kutubana tusiwahoji.  Tukubaliane kwamba udhaifu wao si utetezi wa makosa yao. Hatuwezi kuyaacha makosa yao yaende tu na yawe mfano wa kuigwa.  Tutawakosoa, tutawakemea na kuwatuhumu. Kwa kufanya hivyo, hatuwachafui bali tunasema kwamba wamechafuka; wajisafishe.  Warioba anamwonea Dk. Willibrod Slaa aliyetangaza orodha ya watuhumiwa. Anasema Dk. Slaa anawachafua aliowatuhumu. Hivi Dk. Slaa ndiye alisuka mipango yao ya ulaji ambao anawatuhumu kufanya?  Warioba anathibitishaje kwamba walikuwa safi kabla ya Dk. Slaa kuwataja? Mbona sasa Warioba mwenyewe anadai tuhuma hizi si mpya? Kumbe alikuwa anawajua? Mbona hakuwakemea? Mbona hakuwashauri? Au mbona hakuwasafisha? Kutokuwa jipya kunaondoa makosa yaliyofanyika huko nyuma? Alitarajia ziletwe mpya wakati hizo za zamani hazijashughulikiwa?  Mzee Warioba alipewa jukumu la kuongoza tume ya rushwa miaka 10 iliyopita.  Alitoa mapendekezo kwa serikali, na amekuwa akilalamika kwamba hayatekelezwi. Alipoombwa majina ya waliotuhumiwa kwenye tume yake, akaruka hatua 100.  Woga! Sasa si awaache walio na ujasiri watamke majina waliyo nayo? Si aache mahakama ishughulikie madai yao?  Hata kama yeye ni jaji, kesi hii haijapalekwa kwake. Haruhusiwi kutoa hukumu. Na hata kama anatoa hukumu si ofisini mwake katika mkutano na wanahabari. Kile anachowalaumu kina Dk. Slaa kufanya kwa kuwatuhumu viongozi wenzake hadharani, ndicho anachofanya yeye kuwahukumu kina Dk. Slaa hadharani.  Zaidi ya hayo, Warioba anakwenda mbali. Anakejeli ushahidi wa wanaotoa tuhuma hata kabla haujatolewa. Je, anajuaje kiwango cha ushahidi kilicho mikononi mwa Dk. Willibrod Slaa na wenzake hata kabla hajaenda mahakamani?  Nadhani Warioba anaanza kupitwa na wakati. Wananchi hawawezi kulazimishwa kuwa na 'imani.' Imani inapaswa kujengwa na watawala mioyoni mwa wananchi. Rais Kikwete alianza vizuri na alianza pazuri. Mtangulizi wake alimjengea mazingira mazuri ya kuongoza nchi. Yanayompata sasa hivi hayatoki nje ya serikali yake. Hayaletwi na wananchi wake. Yawezekana ni sehemu ya matokeo ya majivuno waliyoingia nayo madarakani.  Wananchi wamempenda kweli; lakini yeye ameanza kuwakataa taratibu. Wamekuwa na matumaini makubwa naye, sasa wanaishia kuonyesha moyo wa kukata tamaa.  Rais wetu hataki kupendeka. Wananchi wameamini kauli zake, hawajaona matendo yake. Wameamini nafsi yake, hawajawaamini wasaidizi na maswahiba wake. Kama watu leo wanamgeuka, basi ni kwa sababu ameshindwa kushikamana nao.  Warioba anawaeleza nini wananchi waliofurahia kauli ya rais kwamba serikali ingepitia mikataba ya madini ili iwe na manufaa, na sasa wanasoma habari za mkataba mpya wa Buzwagi kwamba nao ni yale yale!  Lakini sababu ya pili ya matatizo ya serikali ya Kikwete inatokana na hoja ya pili inayotolewa na Jaji Warioba. Anasema: "Mwaka 2005 niliyasema haya ya kupakana matope, ukianza dhambi hii huwa haiishi, wakati huo wapo waliokuwa wakisema oh huyu Mwarabu! Dhambi hii ndiyo inaendelea sasa."  Hapa nakubaliana na Warioba. Harakati na kampeni za Kikwete kuingia madarakani zilifanywa kwa kuwaandama na 'kuwachafua' vigogo kadhaa ndani ya CCM na serikali. Nilishaandika huko nyuma kwamba miongoni mwao walikuwamo kina Frederick Sumaye, Profesa Mark Mwandosya, John Malecela, Iddi Simba na wengine waliodhaniwa wangeutaka urais.  Baada ya kuwaondoa hao katika mioyo ya wananchi, harakati hizi zilimalizikia kwa akina Benjamin Mkapa na Dk. Salim Ahmed Salim. Mkapa aliguswa ili alegeze kamba, amtupe 'mtu wake' akumbatie mtu wao. Walifanikiwa.  Wengi tunajua kuwa Mzee Warioba alikuwa mmoja wa waathirika wa kampeni hizi kwa sababu mtu wake hakupita. Nilimtazama Warioba kwenye luninga siku Kikwete aliposhinda na kutangazwa mgombea wa CCM, Dodoma. Warioba alishindwa kuficha hisia zake. Alinuna na kuchukia waziwazi kwa sababu alijua sababu za mtu wake kushindwa.  Najua itamchukua muda kusahau hili. Ndiyo maana amelizungumzia hata wiki hii. Lakini hilo limepita. Yeye, kama wengine, amekuwa majeruhi wa siasa za kurushiana mabomu. Anajua walioyarusha. Sasa imekuwa zamu yao kurushiwa kutoka upande mwingine.  Kinachowaumiza ni kwamba kwa kuwa wameanza kurushiwa mapema mno. Wanajua pia athari ya mabomu waliyowarushia wenzao kwa miaka kadhaa.  Wanaona mazingira magumu yanayowakabili sasa na huko waendako. Tofauti na zama zao, mabomu ya sasa yanarushwa kutoka nje ya CCM, lakini yana vyanzo ndani ya serikali yao.  Tena mingine yana mizizi mirefu. Wanaogopa kwamba mizizi hii ikiendelea kuchimbwa, mwishowe ukweli waliouficha kwa muda mrefu utagundulika. Kwa hiyo, kinacholindwa na kauli za kina Warioba si uhai wa Watanzania; si amani ya taifa, bali ya viongozi wa sasa na waliostaafu.  Kama Warioba angekuwa na busara ya uzeeni, asingewashutumu wanaorusha mabomu haya, kwa sababu tayari ameshakiri kwamba wanaorushiwa mabomu walitengeneza njia hiyo wao wenyewe.  Angepaswa kuyatarajia hayo. La msingi, awashauri hao anaowatetea wajisafishe. Na kuna tofauti kati ya kujitetea na kujisafisha. Kujisafisha ni kuishi na kutenda kwa uadilifu na uangalifu katika nafasi walizo nazo. Wakati mwingine, ni vema kukubali ukweli, kuomba radhi, kurekebisha mambo na kusonga mbele.  Lakini kama hawezi kuwashauri wanaotuhumiwa, akae kimya ashuhudie mabadiliko ya kifikra.  Ajue kuwa mbinu za kisiasa zimebadilika. Atambue kuwa umma umeamka. Ajue kuwa sasa harakati na ulinzi wa rasilimali zimepamba moto. Na Watanzania wa leo wanajua fika kwamba Tanzania yenye neema inawezekana bila Mkapa, Warioba wala Kikwete. ansbertn@yahoo.com +447828696142 www.ngurumo.blogspot.com</description>
					  <author>Marshy Abdu</author>
					  <pubDate>Mon, 01 Oct 2007 00:00:00 EAT</pubDate>
					  <subject />
					</item>

				

					<item>
					  <title>Zitto azua kizaazaa Chuo Kikuu</title>
					  <link>http://www.habaritanzania.com/blogs/35/Zitto-azua-kizaazaa-Chuo-Kikuu</link>
					  <description>na Charles Mullinda na Dauson Harlod  JUMUIYA ya wanafunzi wa vyuo vikuu mbalimbali hapa nchini wameonya kwamba iwapo serikali haitakuwa tayari kufanya majadiliano ya wazi kuhusu tuhuma zinazowaandama baadhi ya watendaji wake, hawatasita kuwaunga mkono wanaharakati na wanasiasa wa vyama vya upinzani katika madai yao.  Walitoa tamko hilo jana, baada ya kufunga lango kuu la kuingia Chuo Kikuu cha Ardhi (zamani Chuo Kikuu Kishiriki cha Ardhi), Dar es Salaam wakishinikiza kuruhusiwa kwa Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Kabwe Zitto, kuruhusiwa kuingia chuoni hapo kushiriki mdahalo wa nafasi ya mwanafunzi wa elimu ya juu katika jamii.  Walisema wamefuatilia kwa kina tuhuma za ufisadi zinazotolewa sasa na baadhi ya viongozi wa vyama vya siasa na wanaharakati dhidi ya viongozi kadhaa wa serikali na kwamba wameona kuna haja ya kutoa mchango wao kama wasomi wanaotegemewa na jamii ya Watanzania katika maendeleo ya taifa.  "Taifa sasa liko katika malumbano makali na mabaya yanayowahusisha viongozi wetu ambao wamepewa dhamana ya uongozi, lakini wanadaiwa kujinufaisha wao na familia zao kwa nyadhifa hizo tulizowapa.  "Madai yanayotolewa ni makubwa na kwa msomi yeyote, lazima ukisikia tuhuma hizi utazifuatilia tu, kwa sababu zinahusu uhai wa taifa letu, sasa tumeamua kuanza kukutana na hawa viongozi wetu, wanaotuhumu na wanaotuhumiwa, tuzungumze nao katika midahalo, wametuambie kuhusu mambo haya na sisi tuwahoji, wanao wajibu wa kutujibu, kwa sababu mchango wetu ni muhimu kwa maendeleo ya taifa hili," alisema Makune Cosmas, mwanafunzi wa mwaka wa tatu katika Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE).  Hata hivyo mjadala uliokuwa umeandaliwa na Mtandao wa Wanafunzi Tanzania (TSNP) kwa kushirikiana na Umoja wa Wanafunzi Wanaosoma Sayansi ya Siasa na Utawala (DUPSA) jana, ulishindwa kufanyika baada ya uongozi wa chuo hicho kumpiga marufuku kuingia chuoni hapo, mtoa mada katika mdahalo huo, Kabwe Zitto.  Tangazo la kupigwa marufuku Zitto lilitolewa na Mratibu wa Mahusiano wa (TSNP), Dady Igogo, akieleza kuwa Zitto amezuiliwa kuingia katika eneo la Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, kwa sababu uongozi huo ulikuwa unahisi kuwa anaweza kuwashawishi wasomi hao kuiasi serikali.  Igogo alisema kabla ya kumwalika Zitto kuhudhuria mdahalo huo, taratibu zote kwa ajili ya kufanya mjadala huo zilifuatwa, ikiwa ni kuandika barua kwa uongozi wa chuo, kuhusu kufanyika kwa mdahalo na kupewa ruhusa ya kufanya mkutano katika Ukumbi maarufu wa Nkrumah, uliopo katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, sehemu ya Mlimani.  Alisema walipewa kibali cha kutumia ukumbi huo Septemba 25, jioni na walianza kubandika matangazo ya kuwepo kwa mdahalo katika eneo la UDSM.  Alisema Sept 26, waliarifiwa kubadili ukumbi wa kufanyia mdahalo huo na wakitakiwa kujiandaa kwa ajili ya kukutana katika Ukumbi wa Theatre One.  Kwa mujibu wa Igogo, Septemba 28 uongozi wa wanafunzi uliitwa tena na uongozi wa chuo na kuelezwa kuwa kama Zitto atafika katika mjadala huo hatatakiwi kuzungumzia mambo ya siasa, na juzi asubuhi, ilitolewa amri nyingine kuwa wanafunzi hawaruhusu kutumia ukumbi huo, kwa sababu ukumbi wa jirani unatumiwa na mabalozi, na kwamba walitakiwa kuacha kufanya mjadala huo.  Mratibu wa haki za wanafunzi (TSNP), Fute Imani, alisema kufutwa kwa mdahalo huo katika hatua za mwisho, ni usumbufu kwa washiriki ambao walialikwa kutoka vyuo vikuu mbalimbali hapa nchini.  Taarifa ya DUPSA imeeleza kwamba, nia ya wanafunzi, wanajamii ya vyuo vikuu si kuvunja sheria na taratibu za chuo, lakini uongozi wa chuo umekuwa ukiwalazimisha kufanya hivyo.  Baada ya Zitto kuzuiliwa kuingia chuoni hapo, wanafunzi waliokuwa wamefurika katika Ukumbi wa Theatre One waliandamana hadi lango kuu la kuingia chuoni karibu na Chuo Kikuu cha Ardhi, ambako alikuwa amezuiliwa, na kukuta tayari amekwisha arifiwa kuondoka.  Wanafunzi hao waliwatimua walinzi wa geti hilo na kushika doria wao wenyewe, huku wakizuia magari na pikipiki kupita katika eneo hilo, isipokuwa watembea kwa miguu na waendesha baiskeli.  Mmoja wa wanafunzi waliokuwa wakilinda doria getini hapo, Gastor Florence, wa mwaka wa tatu, UDSM, alilieleza gazeti hili kuwa walikuwa wamejiandaa kumhoji Zitto dhidi ya tuhuma zinazotolewa na viongozi wa kambi ya upinzani ili wazipime na kujadiliana naye mambo mbalimbali yanayohusu ustawi wa taifa.  Alisema baada ya Zitto, walipanga kuendelea kukutana na viongozi wengine wanaohusishwa katika kashfa ya ufisadi ili kuwahoji na kujadiliana nao kama Zitto, lengo likiwa kupata ukweli kuhusu tuhuma hizo.  Florence alisema jumuiya ya wanafunzi imeshangazwa na hatua ya chuo kuonyesha udhaifu mkubwa kwa kumuogopa Zitto kuwa anaweza kuamsha ari ya kimapinduzi kwa wanafunzi iwapo angekutana nao na kujadiliana nao.  Waliapa kuendelea kulifunga geti hilo hadi hapo Zitto atakaporuhusiwa kuingia chuoni hapo na kujadiliana nao.  Hata hivyo walitawanyika baada ya askakri polisi wenye silaha kuwasili katika eneo hilo na kuanza kufanya doria huku wakiruhusu msururu wa magari uliokuwa umezuiliwa kupita katika geti hilo.  Ofisa Uhusiano wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Julius Saule, alisema kuwa uongozi wa chuo uliamua kuzuia mdahalo huo baada ya kubaini kuwa Zitto atahudhuria.  Alisema wakati kibali kinatolewa, barua ya kuomba kufanyika kwa mdahalo haikuonyesha ni nani atakayezungumza katika mdahalo huo. Alisema sababu nyingine ya kuzuiwa kwa mdahalo huo ni kujaa kwa kumbi zote, na wanafunzi walitaarifiwa kuwa wanapaswa kuahirisha mdahalo wao au kuusogeza mbele.</description>
					  <author>Marshy Abdu</author>
					  <pubDate>Mon, 01 Oct 2007 00:00:00 EAT</pubDate>
					  <subject />
					</item>

				
				  </channel>
				</rss>
			