Watalii sita kutoka Marekani na Australia waliopo nchini, wamenusurika kufa baada ya ndege waliyokuwa wakisafiria kuzima injini ikiwa angani.
Tukio hilo lilitokea jana mkoani hapa, lilimfanya rubani wake, Bw. Steven Jolly (32) ambaye ni raia wa Afrika Kusini, kutua kwa dharura katika kijiji cha Lengungu wilayani Monduli mkoani hapa.
Watalii hao walikuwa wakisafiri kwa kutumia ndege hiyo aina ya Cessna yenye namba 5HUNT, mali ya kampuni ya Airwaves Ltd ya jijini Dar es Salaam wakutokea Kleins Camp, kwenye mbuga ya Serengeti.
Hata hivyo, watalii hao hawakupata majeraha makubwa na hakuna mtu yeyote aliyepoteza maisha kutokana na tukio hilo.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Bw.Basilio Matei aliwaambia waandishi wa habari jana kuwa, ajali hiyo ilitokea jana mchana, wakati ndege hiyo ikiwa inakaribia maeneo ya kutua kwenye uwanja mdogo wa ndege wa mjini hapa.
Aliwataja walionusurika katika ajali hiyo Bw. Leflie Weiss, Bw. Lee Shlanger, Bi. Betri Shlanger na Sydney Cowrad, wote raia wa Marekani kutoka jimbo la Texas.
Wengine ni Bw. Johns Adam na Bi. Anne Adam kutoka nchini Australia.
’’Hawakupata majeraha makubwa isipokuwa mshtuko kutokana na ajali hiyo na tayari wameshachukuliwa na kampuni ya Safari Express ambayo ndiyo wakala wa utalii iliyowapeleka Serengeti,’’ alisema