SHIRIKA la Umeme Tanzania (TANESCO) limesema kuwa hakutakuwa na umeme nyakati za mchana kwa wiki nzima.
Kutokana na mabadiliko hayo, Ijumaa na Jumapili ambazo zilikuwa na umeme siku nzima, sasa hazitakuwa na umeme.
Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Adriaan van der Merwe katika taarifa yake kwa vyombo vya habari jana alisema kuwa, hatua hiyo inatokana na idhini ya serikali ya kufanya mabadiliko ya mgawo wa umeme kwa nchi nzima.
Alisema kutokana na mabadiliko hayo, umeme utazimwa kuanzia saa 1.00 asubuhi na kurejeshwa saa 1.00 usiku kila siku.
Tangu TANESCO ilipotangaza kuwapo kwa mgawo wa umeme nchi nzima, kumekuwa na malalamiko kutoka kwa wateja wakidai kuwa wamekuwa wakipoteza muda wa kuzalisha tofauti na ilivyokuwa awali.
Mgawo huu ulianza baada ya kuharibika kwa mtambo wa Kampuni ya Songas inayozalisha umeme kwa kutumia gesi asilia.
Mtambo huo ulioharibika Agosti 23, mwaka huu tayari umepelekwa nchini Uholanzi kwa matengenezo yatakayochukua wiki nane ambapo gharama ya matengenezo hayo inayolipwa na Songas ilitarajiwa kufikia dola bilioni moja.