WIZARA ya Nishati na Madini Kanda ya Kaskazini, imekana kutoa kibali kwa waandaaji wa filamu ya ‘Watumwa wa Vito’ ambayo inawahusisha watoto wadogo katika uchimbaji wa madini ya tanzanite.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jana, Ofisa Mfawidhi wa Madini Kanda ya Kaskazini, John Nayopa, alisema waandaaji wa filamu hiyo walifika ofisini kwake, lakini aliwanyima kibali.
Hata hivyo, watengenezaji wa filamu hiyo walipata kibali cha serikali kutoka Idara ya Habari (MAELEZO), Ofisi ya Waziri Mkuu wakati huo.
“Mimi niliwakataza kwenda Mererani. Leo nashangaa kuona picha hizi… huu ni uhuni, na una athari kubwa," alisema Nayopa.
Alisema watu hao walikuwa wanataka kwenda kwenye machimbo ya tanzanite Mererani, lakini baada ya kuzuiwa kupiga picha ndipo walirejea ofisini mwake.
“Sisi tumejiwekea utaratibu, huwezi kwenda tu kupiga picha kwenye migodi bila idhini yetu," alisema Nayopa.
Filamu hiyo ambayo ilitarajiwa kuzinduliwa jana Jijini New York, Marekani, imeandaliwa na Shirika la Habari la Kimataifa la IRIN kwa msaada wa mashirika mengine ya UNICEF na ILO.
Filamu hiyo inaonyesha jinsi haki za watoto zinavyokiukwa sambamba na jinsi wanavyotumikishwa vibaya.
Waliofika nchini kuandaa filamu hiyo ni William Rondolph aliyekuwa na pasi ya kusafiria namba 205538707 na Jandries Groenendik aliyekuwa na pasi namba NF 6412034.
Imebainika kuwa aliyewapa kibali ni Ofisa Habari Mkoa wa Arusha, Richard Mwangulube, kwa maelekezo ya mkuu wake, John Hokororo aliyekuwa makao makuu.
Akizungumzia filamu hiyo, Mratibu wa Shirika la Good Hope, Harry Mushi, alisema: "Mimi nilikuwa Mererani nikapigiwa simu na ILO na ofisa habari kuwa niwasaidie hawa na nilifanya kazi hiyo, lakini nashangaa walichokionesha ni mapungufu pekee."