WATU wenye silaha walilipua gari nje ya Ubalozi wa Marekani kabla ya kukabiliana na walinzi wa Syria jana katika shambulio lililoshindwa kwenye eneo lenye balozi za nje.
Makachero wa Syria walifanikiwa kuua watu watatu, serikali ilisema.
Wizara ya Mambo ya Ndani, inayohusika na polisi ilisema kwamba mtu wa nne alijeruhiwa katika kile ilichokiita shambulio la kigaidi.
Ripoti zilizotokea kwenye televisheni inayoendeshwa na serikali zilisema kwamba uchunguzi uko njiani.
Mjini Washington, Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani alithibitisha kutokea kwa shambulio hilo lililofanywa na watu wasiojulikana, na alisema kwamba hali imerudi kuwa ya kawaida.
“Mamlaka husika zimefanikiwa kuzima jaribio hilo na ziko eneo la tukio,” msemaji huyo Kurtis Cooper alisema na kuongeza kwamba hana habari zaidi kwa sasa.
Wasyria wanaofanya kazi katika ubalozi huo walisema kwamba hakuna raia wa Marekani aliyejeruhiwa.
Makachero wa usalama walilizingira eneo la Rawda ambalo ni eneo lenye majengo mengine ya balozi, na makazi ya maofisa waandamizi.
Vyanzo vya Kiusalama vililiambia Shirika la Habari la Uingereza (BBC) kwamba inaaminika makachero wa Syria waliuvunja mpango wa kuushambulia ubalozi huo.
Magari ya wagonjwa na zima moto yalionekana yakipishana nyakati za asubuhi kuelekea na kutoka eneo hilo.
Mashambulizi hayo yamekuja wakati kuna mvutano kati ya Washington na Damascus, huku Syria ikikasirishwa na Marekani kuunga mkono mashambulizi ya Israel nchini Lebanon.
Marekani inaituhumu Syria kusaidia wanamgambo nchini Iraq na kutofanya lolote kuzuia uvushaji wa silaha kwenda kwa wapiganaji wa Hezbollah nchini Lebanon.
BBC/AP