MKE wa Rais, Salma Kikwete, amejiingiza kwenye mgogoro na wanaharakati wa masuala ya jinsia na harakati za wanawake barani Afrika.
Mtandao wa mashirika yasiyo ya kiserikali yanayoshughulikia masuala ya haki za binadamu na maendeleo (FEMACT), jana ulitoa tamko kuelezea kusikitishwa na kitendo cha Salma Kikwete kushiriki sherehe zinazodaiwa kuwadhalilisha wanawake nchini Swaziland, hivi karibuni.
Katika sherehe hizo, Mfalme Mswati anapata fursa ya kuoa mke miongoni mwa wasichana wadogo kila mwaka.
Taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA), Ananilea Nkya, inaeleza kuwa FEMACT inaungana na wanaharakati wote wa masuala ya jinsia na maendeleo ya wanawake barani Afrika katika kupiga vita mila hiyo ya Swaziland, kwa sababu inaendeleza mfumo kandamizi dhidi ya wanawake na wanaume masikini.
“Mila hiyo ya kuwapanga wasichana wadogo hadharani wakiwa nusu uchi ili Mfalme aweze kuchagua msichana kuongeza idadi ya wake zake, ni mila mbaya ya kumdhalilisha mwanamke na utu wa binadamu katika zama hizi.
“FEMACT tunaamini kwamba utamaduni huo unaomwezesha rais kuongeza mke kila mwaka unapaswa kupigwa vita na wanaume na wanawake wote barani Afrika kwa sababu unawapa fursa wanaume wenye madaraka kuwatumia wanawake kama chombo cha kujistarehesha na hivyo kuathiri maendeleo ya wanawake katika namna mbalimbali.
“Kadhalika, FEMACT tunatambua kuwa Tanzania imesaini Azimio la Jumuiya ya Uchumi ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) kuhusu jinsia na maendeleo ambalo linazitaka nchi wanachama kutokomeza vitendo vya kikatili na vinavyodhalilisha wanawake.
“FEMACT, inaamini kuwa viongozi wa SADC wanapaswa kukataa kuhudhuria sherehe hiyo ya kimila na kuwa mstari wa mbele kuishawishi Swaziland kuachana na mila hiyo.
“Hivyo tunashangaa ilikuwaje mke wa rais wetu, Mama Salma Kikwete kushiriki sherehe hiyo, jambo ambalo linatafsiriwa kama kuihalalisha mila hiyo.
“Tunaona pengine mke wa rais alishauriwa vibaya au hakupewa taarifa kuwa wanawake na wanaharakati wa maendeleo nchini Swaziland wamekuwa katika harakati za kuitokomeza mila hiyo kwa miaka kadhaa sasa,” ilieleza sehemu ya taarifa hiyo.
Taarifa hiyo inahoji kushiriki kuwa, kwa Mama Kikwete katika sherehe hiyo hakutampa athari mbaya kama kiongozi mwanamke wa kupigwa mfano katika kutetea haki za wanawake Tanzania, Afrika na dunia?
Taarifa inaeleza kuwa, FEMACT iko mstari wa mbele kumpatia mke wa rais maoni yao ya masuala ya jinsia na maendeleo, hususan yanayohusu mila na haki za wanawake.