NAIBU Waziri wa Mipango, Uchumi na Uwezeshaji, Salome Joseph Mbatia, amesema serikali imedhamiria kuona watoto wa kike wanapata elimu kama ilivyo kwa watoto wa kiume.
Amesema idadi ya wanawake wasiojua kusoma na kuandika, ni kubwa kuliko wanaume, hali inayotoa changamoto kwa serikali na jamii kuhakikisha watoto wa kike wanapata elimu.
Naibu Waziri Salome alisema hayo mwishoni mwa wiki wilayani Siha wakati wa mahafali ya nne ya wahitimu wa kidato cha nne wa Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Visitation Bethel.
Akinukuu ripoti ya Umaskini na Maendeleo ya Binadamu ya mwaka 2005, alisema idadi ya Watanzania wenye umri zaidi ya miaka 15 wanaojua kusoma na kuandika ni aslimia 69.
Kati ya hao, wanaume ni asilimia 78 na wanawake ni asilimia 62 tu.
Alisema serikali imeshaona sababu mbalimbali zinazowakwamisha watoto wa kike kutopata nafasi ya kusoma kama ilivyo kwa watoto wa kiume.
Alisema juhudi za kumwendeleza mwanamke, zinalenga kuleta uwiano sawa.
Alisema serikali ya awamu ya nne imedhamiria kuboresha mfumo mzima wa elimu kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa ndani na nje ya nchi.
Katika mahafali hayo, Naibu Waziri Salome aliongoza harambee iliyowezesha kupatikana kwa sh milioni 17. Kati ya kiasi hicho, fedha taslimu zilikuwa sh milioni saba.
Naibu Waziri huyo alichangia sh 700,000; huku akiwa amehamasisha wadau wengine wengi kuchangia maendeleo hayo ya kitaaluma. Fedha hizo zote zitatumika katika ujenzi wa mabweni ya wasichana shuleni hapo.
Katika hatua nyingine, Naibu Waziri Salome aliiasa jamii kuishi kwa maadili, hasa ya dini zao ili iweze kujikinga na maambukizi ya UKIMWI.
Alisema matumizi ya kondomu si kinga ya UKIMWI, hivyo watu wasijidanganye kwa kuamini zana hizo.
Alisema kuwa dawa ya kuutokomeza UKIMWI ni kuishi katika ndoa na kwa uaminifu.
Alitumia fursa hiyo kuwaasa wanafunzi hao kuacha kujihusisha na vitendo vya ngono, kwani kwa kuendekeza vitendo hivyo, wataharibu maisha yao na ya taifa kwa jumla.
Alitoa wito kwa jamii kuwajali na kuwasaidia watu wenye maradhi ya UKIMWI, na kuacha kabisa unyanyapaa.
Salome alisema takwimu zinaonyesha kuwa kiwango cha mambukizi ya virusi vya UKIMWI ni wastani wa asilimia saba; huku kiwango hicho kwa wanawake kikifikia asilimia 7.7 na wanaume asilimia 6.3.