WAZIRI wa Miundombinu, Basil Mramba, ameibuka na kuwashambulia wabunge walioichachafya hotuba yake ya bajeti katika Mkutano wa Nne wa Bunge uliomalizika mjini Dodoma mwezi uliopita.
Mramba ambaye ni Mbunge wa Rombo, amesema kwamba kilichoibuliwa bungeni juu ya ujenzi wa barabara ya Marangu -Tarakea hadi Kamwanga, ilikuwa fitina ya wabaya wake.
Akiwahutubia wananchi wa Tarafa ya Mengwe katika ziara yake ya wiki moja jimboni mwake, alisema kuwa ujenzi wa barabara hiyo yenye urefu wa kilometa 90 (si tisa kama ilivyokuwa ikiripotiwa awali), umo kwenye Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2005.
Ingawa hakuwataja wabunge ambao ni wabaya wake, bila shaka alimlenga Mbunge wa Nzega, Lucas Selelii (CCM), ambaye ndiye alikuwa wa kwanza kuibua sakata la Mramba kutenga kiasi cha sh bilioni 17 kwa ajili ya ujenzi wa barabara hiyo.
Baadhi ya walioichachafya wizara ya Mramba ni Mbunge wa Bariadi Magharibi, John Cheyo (UDP) na Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe (CHADEMA).
Katika mkutano huo, Mramba alisema kuwa, hata Rais Jakaya Kikwete katika ziara yake mkoani Kilimanjaro wakati wa kampeni mwaka jana, aliahidi kujengwa kwa barabara hiyo katika kiwango cha lami.
Kama kawaida yake, Mramba aliipamba hotuba yake kwa vionjo ambavyo ni adimu kuvipata kwa wanasiasa wengi.
Alitamba kwa kusema kwamba baada ya wabunge kupewa ‘somo’, waliipitisha
bajeti ya wizara yake kwa kishindo, na sasa barabara hiyo haina pingamizi katika ujenzi wake.
Katika hatua nyingine, Mramba alisema, awamu ya pili ya ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami kutoka Tarakea hadi Makao Makuu ya Wilaya ya Rombo, Mkuu; itaanza mwaka huu wa fedha baada ya mkandarasi kupatikana.
Alimtaja mkandarasi huyo kuwa ni Kampuni ya Great Nile ya Misri yenye ofisi zake nchini Uganda.
Kampuni hiyo itajenga barabara hiyo yenye urefu wa kilometa 43 kwa miezi 30