HAIKUTARAJIWA, lakini ilitokea. Ujirani na uhusiano mwema kati ya Rais Jakaya Kikwete na waandishi wa habari jana uliingia dosari baada ya waandishi kufukuzwa katika ziara yake.
Waandishi hao wa vyombo mbalimbali vya habari nchini, walikuwa katika siku ya mwisho ya ziara yake ya kutembelea Wizara ya Usalama wa Raia kwenye Ukumbi wa Diamond Jubilee, Dar es Salaam.
Ilikuwa baada ya Rais Kikwete kutembelea maeneo mbalimbali ya wizara hiyo na kuzindua mfuko wa akiba na mikopo (SACCOS) wa wafanyakazi wa wizara hiyo.
Msemaji wa Jeshi la Polisi, Essaka Mugasa, ndiye aliyewagombanisha waandishi na Rais Kikwete, baada ya kutangaza kwa vipaza sauti na kusema: “Waandishi wa habari na wageni toka benki ya CRDB tunaomba muondoke.”
Baada ya kauli hiyo, waandishi walipigwa butwaa na kutoka nje ya ukumbi huku wakiulizana maswali, kuna siri gani katika kikao cha rais na askari, huku wakizungumza kupitia vipaza sauti.
Waandishi wengi walinung’unika na kulalamika, kwamba hawakutendewa haki, lakini hakuna aliyewasikiliza.
“Tunakubali kuondolewa kwenye mkutano huu, lakini hawajatutendea haki kabisa, tumeshirikiana nao tangu asubuhi kwa kutembelea maeneo mbalimbali…, inasikitisha na inakatisha tamaa,” alisema mwandishi mmoja ambaye pia ni mpiga picha.
Rais Kikwete alikuwa anakutana na maofisa wa ngazi za juu, wakuu wa vitengo, na askari wa ngazi za chini ikiwa ni moja ya utaratibu wake aliojiwekea kwa kutembelea wizara mbalimbali.
Hii ni mara ya kwanza kwa waandishi kufukuzwa katika tukio linalomhusu Rais Kikwete, ambaye amekuwa akidaiwa kuwa karibu na waandishi. Kwa sababu hiyo, waandishi wengi walilalamika kwamba ndiye aliyewafukuza, na kwamba kama angetaka angewazuia maofisa wake kutenga waandishi.
Hata hivyo, Chama Cha Mapinduzi (CCM) tayari kimeingizwa katika ubaguzi wa waandishi wa habari. Wiki chache zilizopita, Katibu Mkuu wa CCM, Yusuf Makamba aliwafukuza waandishi katika mkutano mmoja wa ndani aliokuwa anauhutubia mkoani Singida. Baada ya kuwafukuza ukumbini kwa kauli kali, kwa kisingizio kuwa wanapotosha anayosema, aliwaita tena waandishi wa Radio Tanzania na magazeti ya Daily News, Uhuru na Mzalendo.