CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kimetangaza utaratibu wa kuteua wanachama wanaotaka kugombea ubunge wa Afrika Mashariki, na sifa za waombaji.
Taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa jana na Katibu Mkuu wa chama hicho, Dk. Willibroad Slaa, sifa ya kwanza ya mwombaji lazima awe raia wa Tanzania.
Sifa nyingine ni kuwa mbunge wa Bunge la Tanzania na awe na nia thabiti ya kupenda kuendeleza malengo na madhumuni ya Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Taarifa hiyo inaeleza kuwa fomu za kuomba kuteuliwa zinapatikana katika ofisi za mkoa na ofisi ya Katibu Mkuu. Inawataka waombaji kuwasilisha maombi yao katika ofisi ya Katibu Mkuu Septemba 30.
Anaelekeza Katibu Mkuu huyo kwenye taarifa yake hiyo kuwa waombaji wanatakiwa kufika kwenye ofisi ya Katibu Mkuu Dar es Salaam kwa ajili ya mahojiano Oktoba 15.
Baada ya kukamilika kwa taratibu hizo, Kamati Kuu itakutana kuchagua jina moja la mwanachama atakayegombea nafasi ya ubunge wa Afrika Mashariki kupitia CHADEMA.