Na Mary Ngoboko, Mwanza
WATU watatu wamekufa katika matukio tofauti mkoani hapa, likiwamo la mwanaume kujinyonga baada ya kumkatakata mkewe kwa mapanga.
Tukio la kwanza lilitokea juzi katika kijiji cha Mtakuja wilayani Geita mkoani hapa, ambapo mtu alikutwa amejinyonga.
Akizungumzia tukio hilo jana, Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mwanza, Bw. Zelothe Stephen, alimtaja aliyejinyonga kuwa ni Dominick Jackson (36) na kwamba alijinyonga nje ya nyumba yake.
Kamanda Zelothe alisema marehemu alikutwa amejinyonga kwa kamba ya manila juu ya mti.
Alisema chanzo cha kujinyonga kwa mwanaume huyo ni kumtuhumu mkewe Bibi Theresia Ernest (31) kwamba alikuwa akifanya vitendo vya kiasherati.
Pia Kamanda alisema inadaiwa mkewe huyo alikuwa amefungua mashitaka mahakamani ya kudai talaka.
Kamanda Zelothe alisema siku moja kabla ya tukio saa mbili usiku Dominick alimpiga mkewe na kumkatakata kwa mapanga huku amembeba mtoto Sada Dominick (1) ambao walijeruhiwa na kupelekwa katika hospitali ya wilaya ya Sengerema kwa matibabu.
Alisema mwanamke huyo alilazwa katika hospitali hiyo na baadaye alifariki dunia.
Katika tukio lingine lililotokea juzi, mkazi wa Igombe, Ilemela jijini hapa, Bw. Jadiuo Obeid (21), anahofiwa kufa maji baada ya mtumbwi aliokuwa akiutumia kuvua samaki kupigwa na dhoruba na kuzama.
Kamanda Zelothe alisema inadaiwa kuwa siku hiyo, marehemu na wenzake ambao hawajafahamika, walikwenda kuvua samaki na kuzama.
Kamanda alisema wavuvi wengine ambao alikuwa nao walijiokoa kwa kuogelea huku yeye akishindwa kufanya hivyo na kwamba mpaka sasa hajapatikana.
Aidha Kamanda Zelothe alisema Jeshi la Polisi kwa ushirikiano wa wananchi na vikundi mbalimbali wanaendelea na kumtafuta mvuvi huyo