MAMIA ya wakazi wa mji wa Vwawa wilayani hapa, juzi walijitokeza kumzika Lucas Msuya, aliyefia mikononi mwa polisi wa Zambia wiki iliyopita.
Akiwasilisha salamu za serikali, Mkuu wa Wilaya ya Mbozi, Halima Kihemba, amesema msiba huo si wa familia ya Msuya pekee, bali ni wa Watanzania wote kutokana na mazingira ya kifo chake.
Msuya aliuawa na polisi wa Zambia akiwa kwenye mahabusu ya Kituo cha Polisi Nakonde, nchini Zambia.
Mkuu huyo wa wilaya aliwataka wananchi wawe watulivu wakati polisi wakiendelea na uchunguzi wa kifo hicho.
Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini (IGP), Said Mwema, ametuma salamu za rambirambi na sh 100,000 kwa familia ya marehemu ambazo ziliwasilishwa na Mkuu wa Upelelezi wa Wilaya ya Mbozi, Steven Mtengeti.
Kwenye salamu hizo, Mwema aliwataka kutulia na kuahidi kuwa serikali itahakikisha haki inatendeka.
Mwili huo umechukuliwa kutoka Zambia baada ya wataalamu wa upasuaji kutoka Tanzania kwa kushirikiana na wataalamu wa Zambia kumaliza kuufanyia uchunguzi.
Kifo cha Lukas Msuya, kimekuwa ukombozi kwa watuhumiwa wengine kwani baada ya kufikia muafaka wa pande mbili hizi, mahabusu Watanzania waliokuwa katika kituo cha Nakonde wameachiwa huru.