MUSA Jumanne (29), mkazi wa Kitongoji cha Kati, kijijini Majengo, katika Wilaya ya Arumeru, anatafutwa na Jeshi la Polisi, baada ya kumkatakata mwanawe wa kuzaa na kitu chenye ncha kali hadi kumuua.
Akielezea tukio hilo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Basilio Matei, alisema kwamba, Jumanne alitenda kosa hilo juzi asubuhi akiwa nyumbani kwake Arumeru. Alikuwa na mwanawe tu nyumbani.
Kamanda Matei alisema kwamba, mtuhumiwa huyo alitenda kosa hilo baada ya kumfukuza mkewe Mwajuma Daudi (24) Septemba mosi mwaka huu, kutokana na ugomvi wao binafsi na alibaki akiishi na mwanawe huyo aitwaye Jumanne Musa (4).
Kamanda Matei alisema cha kushangaza, juzi majira ya asubuhi alimchukua mtoto wake huyo na kuanza kumkatakata na kitu chenye ncha kali hadi alipokata roho na kumtelekeza kwenye nyumba yao bila majirani kujua kilichokuwa kinaendelea.
Alisema kwamba, baada ya Jumanne kufanya unyama huo, alikwenda nyumbani kwa mkewe aliyemfukuza na kumweleza aende nyumbani, kwani mtoto wake ni mgonjwa na yeye alikuwa na safari.
Mwajuma alikwenda nyumbani kwa mumewe ili ampeleke mwanawe hospitali, lakini alipofika nyumbani kwa mumewe, alikuta mlango ukiwa wazi na alipoingia ndani alishitushwa baada ya kukuta mwanawe amelala chini, akiwa ameshakata roho, huku akiwa ametapakaa damu mwili mzima.
Kamanda Matei alisema mama huyo alianza kupiga kelele, ndipo majirani na viongozi wa kitongoji wakafika kushuhudia unyama huo, wakatoa taarifa polisi, ndipo askari walipofika katika eneo hilo la tukio na kuchukua maiti ya mtoto huyo.
Kamanda Matei alisema polisi imepata taarifa kuwa Jumanne alionekana katika Mererani, wilayani Simanjiro mkoani Manyara, ambako alikuwa akiuza baiskeli yake ili aweze kutokomea pasipojulikana. Mwili wa mtoto huyo umehifadhiwa katika Hospitali ya Mkoa ya Mount Meru.