Rais Jakaya Kikwete amewashauri wafanyabiashara Wamarekani, kuja kuwekeza na kufanya biashara nchini Tanzania.
Alitoa ombi hilo kwenye hafla ya chakula maalum kilichoandaliwa kwa heshima yake na wafanyabiashara maarufu nchini Marekani na kufanyika katika?Makao makuu ya chama cha wafanyabiashara wa masoko ya hisa kwa njia ya elektroniki (NASDAQ) chenye kampuni 3,200 zinazofanya biashara mbalimbali.
?Rais Kikwete alisema, wafanyabiashara hao wanaochangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya uchumi wa Marekani, hawana sababu ya kuogopa wala kusita kuja kuwekezeka na kufanya biashara nchini.
Alibainisha kuwa gazeti la Financial Times la Uingereza katika moja ya matoleo yake ya mwaka 2005/2006, liliitaja Tanzania kama nchi ya pili baada ya? Afrika ya Kusini yenye mazingira mazuri ya kuvutia uwekezaji na biashara.
’’Kutokana na taarifa hiyo na nyinginezo, itatupa moyo sana ikiwa miongoni mwenu mtakuja Tanzania na kutafuta maeneo ya uwekezaji,’’ alisema.
?Rais Kikwete aliyataja maeneo kadhaa yanayowafaa wafanyabishara hao kuwekeza kuwa ni sekta za madini, utalii, ujenzi wa miundombinu, uzalishaji hasa wa mazao ya kilimo, fedha na teknolojia ya mawasiliano (IT).
Aidha,? Rais Kikwete alisema alisema pia eneo jingine linalovutia uwekezaji ni mafuta ambayo utafiti unaonyesha dalili kama vile kuwepo kwa gesi asilia katika maeneo kadhaa ya Tanzania ni kiashiria kizuri kuwa huenda (mafuta)? yanapatikana katika ardhi ya Tanzania.
Alisema, zaidi ya kampuni 20? ikiwamo ya Shell zinaendesha shughuli za utafiti wa mafuta katika maeneo mbalimbali nchini.
Akimtambulisha Rais kwa wafanyabiashara hao kutoka makampuni makubwa mengi ya hayo yakijishugulisha na bishara ya soko la hisa, Bw. Stan Bergam aliisifia Tanzania kwa maelezo kuwa ’’imejipanga’’ vema katika kuleta mabadiliko na mageuzi ya uchumi.
?Alisema, Tanzania ni nchi inayozingatia misingi ya utawala wa kidemokrasia, yenye amani isiyoteteleka na vivutio vikubwa vya uwekezaji.
Bw. Begram ambaye familia yake pia inaendesha miraji ya vituo vya kisasa vya kijamii maalumu kwa ajili ya vijana kwenye mikoa ya Arusha na Ruvuma, iliwahi kutoa msaada wa vitabu? 25,000 katika maktaba ya Chuo Kikuu cha Ruaha mkoani Iringa.
Wakati huo huo Rais Kikwete amesema ukosefu wa rasilimali ni miongoni mwa sababu zinazokwamisha jitihada za nchi maskini sana duniani kukabiliana na changamoto za utawala bora.
Alisema kutokana na hali hiyo, kuna haja ya kuimarisha ushirikiano kati ya nchi maskini na zilizoendelea ili kuweka mazingira yatakayochochea uwezekano kwa nchi maskini kuzingatia na kusimamia misingi ya utawala bora.
Rais Kikwete aliyasema hayo alipokuwa akizundua ripoti ya Umoja wa Mataifa ambayo maudhui yake ni ’’Governance for the future; Democracy and development in the least developed countries ’’ kwenye hafla iliyofanyika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa hapa New York.
Alisema, utawala bora ni moja ya misingi muhimu katika uwajibikaji wa serikali na kwa maendeleo ya nchi na watu wake.
’’Kwa mtizamo wangu serikali inayosikiliza, iliyo na uwazi na inayowajibika kwa watu ni muhimu sana kwa maendeleo ya uchumi na kijamii, na kwa hakika utawala bora ni nguvu muhimu ya maendeleo,’’ alisema.
Rais Kikwete ambaye alizindua ripoti hiyo mbele ya wawakilishi kutoka nchi mbalimbali maskini sana duniani alisema, utawala bora unajenga mazingira yanayotoa fursa kwa asasi binafsi na vyama vya kisiasa na kijamii kuheshimiwa na kuendelezwa.
SOURCE: Nipashe