KAMPUNI ya simu za mkononi ya Vodacom, imejitwisha jukumu kusomesha wanafunzi watano katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM).
Walionufaika na mpango huo maalumu chini ya Vodacom, ni wanafunzi wa mwaka wa tatu na nne katika fani ya uhandisi.
Hao ni Razier Given, Bomassy Anis Kuan na Placid Joseph ambao wote wanasomea ufundi wa kompyuta.
Wengine walionufaika na ofa hiyo ya Vodacom ni Felician Mwesigwa anayesomea mawasiliano na Kisamo Arthur George anayesomea umeme.
Hii ni programu maalumu iliyobuniwa na Vodacom mwaka 2004, ikiwa ni mchango wake katika kuinua kiwango cha taaluma kwa maslahi ya wanafunzi wenye uwezo na taifa.
Chini ya programu hiyo, wanafunzi hao watalipiwa gharama zote za ada ya shule, masomo ya ziada, posho ya kujikimu wakati wa likizo, mafunzo na muda wa gharama za mawasiliano.
Hafla ya kuwatangaza na kuwapongeza wanafunzi hao, ilifanyika mwishoni mwa wiki katika Hoteli ya Oysterbay, jijini Dar es Salaam na kuhudhuriwa na Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Mathew Luhanga.
Mbali na kusomeshwa, pia wanafuzni hao watano, wamepewa ajira katika kampuni hiyo pamoja na wengine wawili walio mwaka wa mwisho.
Profesa Luhanga aliipongeza Vodacom kwa kuwa mdau muhimu katika suala la taaluma, kwa maslahi ya vijana na taifa, na kushauri programu hiyo iguse na taaluma nyingine.
“Nawapongeza Vodacom kwa juhudi hizi ambazo zinapaswa kuigwa na sekta na kampuni nyingine, kwani hii ni kuwajengea uwezo vijana katika kukidhi ushindani soko la ndani na nje kitaaluma,” alisema.
Vodacom imekuwa ikichangia kwa kiasi kikubwa suala la ajira kwa vijana, kwani hadi sasa, asilimia 97 ya waajiriwa 472 ni Watanzania.
Wakizungumzia umuhimu wa programu hiyo iliyoasisiwa na Vodacom, wanafunzi hao waliishukuru kampuni hiyo na kutaka kampuni nyingine ziige mfano huo.