SERIKALI ya Thailand imesema kuna haja ya kukuza ushirikiano na Serikali ya Tanzania katika nyanja za utalii na biashara, kwani hapajawahi kuwa na mkakati mahsusi baina ya nchi hizi mbili.
Taarifa ya Ofisi ya Waziri Mkuu iliyopatikana jana jijini Dar es Salaam, imesema kuwa, Waziri Mkuu wa Thailand, Dk. Thaksin Shinawatra akizungumza juzi usiku katika hafla aliyomwandalia mgeni wake, Waziri Mkuu Edward Lowassa na mkewe, Regina Lowassa, nchini humo, alisema sasa umefika wakati wa kuzichukulia sekta hizo kwa makini zaidi.
“Tanzania na Thailand hazijawahi kuwa na uhusiano mkubwa wa kibiashara wala utalii, tuangalie namna ya kuziimarisha na tuende pia katika kilimo na afya na hasa UKIMWI,” alisema.
Pia alimwalika Rais Jakaya Kikwete kutembelea nchi hiyo wakati wowote, ili kuona namna ambavyo nchi hizi mbili zinaweza kushirikiana kuinua hali ya uchumi na maisha ya watu wake.
Akizungumza katika hafla hiyo, Waziri Lowassa alisema Tanzania itaendeleza ushirikiano huu wa sasa na akaahidi kufuatilia mazungumzo yaliyofanyika hivi karibuni jijini Dar es Salaam baina ya Naibu Waziri Mkuu wa Thailand, Surakiart Sathirathan na Rais Kikwete na baadhi ya mawaziri wa serikali ya awamu ya nne.
Pia alishukuru kwa mapokezi mazuri na heshima aliyopewa yeye na viongozi wengine wa serikali ambao wako nchini humo na kuahidi kujifunza mengi katika ziara hiyo, hasa katika kilimo.
“Serikali ya Thailand ni maarufu duniani kwa kilimo cha hali ya juu na hasa uzalishaji wa mchele, tunaamini tuna mengi ya kujifunza katika ziara hii ambayo yataisaidia Tanzania,” alisema.