KINYANG’ANYIRO cha kutafuta ubunge wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) kimeanza, ambapo wenye nia ya kugombea tayari wanajipitisha kwa njia mbalimbali, wakijinadi, bila kueleza nia yao.
Wapo wanaoshiriki kupita kiasi katika hafla, wanaotoa misaada maeneo tofauti, na wengine wanaosema sana katika vyombo vya habari, bila kusahau wanaofanya ziara nyingi, kujiweka karibu na jamii.
Lakini ukweli ni kwamba, kipindi kingine kigumu kwa wanaowania uwakilishi kimewadia, kwani wakati ukomo wa Bunge la EAC unakaribia, taratibu za kupata uwakilishi ndani ya vyama tayari zimeanikwa.
Chama Cha Mapinduzi (CCM), kama ilivyotarajiwa, wameanza mapema, ambapo katika kikao chake cha Kamati Kuu (CC) kilichomalizika mwishoni mwa wiki iliyopita mkoani hapa, wameamua fomu zianze kutolewa wiki ijayo, Septemba 30 na ziwe zimerejeshwa hadi ifikapo saa 10, Septemba 30, wakitoa wiki mbili hivi kwa wahusika.
Katibu Mkuu wa CCM, Yusuf Makamba, aliwaambia waandishi wa habari jana mjini Dodoma kwamba, gharama ya kuchukua fomu ni sh 100,000 na kwamba Kamati Maalumu ya Halmashauri Kuu ya Taifa itajadili majina hayo Oktoba 10.
Makamba alisema kwamba Oktoba 12, CC itakaa kuteua wagombea, Oktoba 28 kamati ya wabunge wote wa CCM itakaa kufanya uteuzi wa mwisho na Oktoba 30 majina yatapelekwa kwa Katibu wa Bunge.
Muda wa wabunge wa Bunge la Jumuiya ya Afrika Mashariki unamalizika mwishoni mwa Novemba mwaka huu. Mchakato wa kuwapata wabunge hao ni kupitia vyama vya siasa vyenye wabunge ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.