Waziri Mkuu Bw. Edward Lowassa amesema serikali ya awamu ya nne inafanya jitihada za makusudi kuhakikisha mpango wa ugawaji chakula mashuleni unatekelezwa nchi nzima.
Bw. Lowassa aliyasema hayo jana kwenye kilele cha matembezi ya dunia ya mwaka 2006 yenye lengo la kuunga mkono ukomeshaji wa njaa na kukuza elimu, yaliyofanyika kitaifa huko Marangu mkoani Kilimanjaro.
Alisema kupitia mpango huo, serikali inakusudia kutoa walau mlo mmoja kwa kila mwanafunzi kwa siku, hali ambayo pamoja na mambo mengine itawawezesha kufuatilia vema masomo yao.
’’Tumejizatiti kulifanyia kazi suala hilo, lakini inahitajika subira kwa sababu sisi kama serikali ndiyo tunaanza kazi, tunahitaji muda zaidi lakini tunawahakikishia kuwa mpango huo utatekelezwa kwa ari mpya, nguvu mpya na kasi mpya,’’ alisema.
Pia alisema, mpango wa lishe utatekelezwa pia kwa watu wanaoishi na virusi vya Ukimwi.
Kwenye ujumbe wake katika matembezi hayo, Balozi wa Kupambana na Njaa wa Mpango wa Chakula wa Umoja wa Mataifa (WFP), Bw. Reginald Mengi alisema kuwekeza katika elimu na lishe ni mambo ya muhimu kwa maslahi ya kizazi kinachokuja.
Naye Mashaka Mgeta anaripoti kuwa HALMASHAURI za wilaya, manispaa na jiji nchini, zimetakiwa kushirikiana na kamati za shule kufanikisha mpango wa kuwapa wanafunzi chakula wanapokuwa shuleni, ili kuweka mazingira mazuri ya ushiriki wao wakati wa vipindi vya masomo madarasani.
Agizo hilo lilitolewa jana na Waziri wa Elimu na Ufundi, Bi. Margaret Sitta alipokuwa anahutubia kwenye kilele cha matembezi ya dunia ya mwaka 2006 kwa ajili ya kuchangia chakula kwa wanafunzi mashuleni na watoto wengine wanaoishi katika mazingira magumu.
Bi. Sitta alisema suala la uhakika wa chakula kuwafikia wanafunzi kwa muda wote, litafanikiwa ikiwa uongozi wa halmashauri hizo utashirikiana na kamati za shule kupanga mikakati inayotekelezeka badala ya kuzifanya shule husika kutegemea msaada kutoka serikalini pekee.
Naye Mratibu wa Mpango wa WFP, Bw. Philippe-Serge Degernier alisema njaa imekuwa ni miongoni mwa matatizo makubwa yanayowaathiri na kusababisha vifo vingi kuliko Ukimwi.
’’Mwaka jana watu wengi walikufa kutokana na njaa na utapiamlo kuliko waliokufa kutokana na virusi vya Ukimwi, malaria na kifua kikuu wakiunganishwa pamoja,’’ alisema.
Matembezi hayo yaliyoanzia kwenye ofisi za WFP na kuishia uwanja wa Patel, yaliwashirikisha watu wa kada mbalimbali wakiwemo wanafunzi ambapo mtoto mdogo kuliko walioshiriki alikuwa Dia Patel (mwaka mmoja na nusu) na mtu mwenye umri mkubwa zaidi alikuwa Bi. Anna Zulu (68).