POLISI wa Zambia, wanatuhumiwa kumuua mfanyabiashara Mtanzania, Lucas Msuya (34), akiwa katika mahabusu ya Polisi Kituo cha Nakonde nchini humo.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Suleimani Kova, alisema jana kwamba Mtanzania huyo alifia mikononi mwa polisi wa Nakonde, Zambia.
Alisema Msuya ambaye alikuwa mkazi wa Tunduma, alikuwa akituhumiwa kwa ujambazi wa kutumia silaha.
Kamanda Kova alisema polisi mkoani Mbeya wanafanya uchunguzi wa kina kuhakikisha wanafahamu chanzo cha kifo cha mfanyabiashara huyo ambaye ni maarufu kwa jina la “Mangi”.
Aliwaomba wakazi wa Tunduma kuwa watulivu, wasilipize kisasi kwa madai kuwa polisi itafanya kila jitihada kujua chanzo cha kifo hicho.
Polisi wa Kituo cha Nakonde walidai kwamba Msuya na mwenzake, Alex Nzowa, walivamia nyumba ya askari polisi aishie uraiani mjini Nakonde, wakavunja na kuiba mali.
Walikaririwa wakidai kwamba Msuya hakukamatwa katika tukio hilo, bali alitajwa na Nzowa; ndipo Agosti 17 polisi walipomtia mbaroni.
Akizungumza na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Mbozi iliyotembelea mahabusu ya Nakonde ikiongozwa na Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Mbozi, Leonard Magacha, Nzowa alikiri kwenda kuiba akiwa na baadhi ya wakazi wa Nakonde ambao ni raia wa Zambia.
Alisema alikamatwa yeye pekee kabla ya kufanya wizi waliokusudia kuufanya.
Aliithibitishia kamati hiyo kwamba Msuya hakuwapo katika tukio hilo na kwamba polisi wa Nakonde walimlazimisha na kumfundisha jinsi ya kuzungumza ili kumtia mbaroni Msuya.
Akizungumza kwa hofu, Nzowa alisema kuwa mara baada ya kufikishwa kituoni, polisi walimpiga mno Msuya, hadi kumsababishia kifo.
Nzowa alisema Msuya alipata majeraha kichwani, mgongoni na miguuni; hali iliyosababisha hofu kwa mahabusu wengine.
Alisema Msuya alikata roho saa 11 alfajiri ya Agosti 28, na kusababisha simanzi kwa mahabusu walioshuhudia unyama huo.
Akizungumza na ndugu wa marehemu baada ya kamati kuangalia mwili wa marehemu katika chumba alichohifadhiwa hospitalini Nakonde, Magacha alisema watahakikisha vitendo vya kinyama vinakomeshwa, kwa kuwa sasa imekuwa kawaida kuwafanyia unyama Watanzania.
Alisema kuwa mwili wa marehemu haukuchukuliwa kwa kuwa maofisa, akiwamo Mkuu wa Polisi Wilaya ya Nakonde, walikuwa wameitwa mkoani kwao kuzungumzia kifo hicho.
Magacha alisema kuwa mwili wa marehemu utachukuliwa leo na kufanyiwa uchunguzi.
Ndugu wa marehemu Msuya, aliyejitambulisha kwa jina la Saimon Kessy, alisema kuwa tangu ndugu yao alipokamatwa, walizuiwa kumwona, na kwamba waliporuhusiwa, walimkuta akiwa na vidonda vinavyotoa usaha.
Alisema alipoomba kumpeleka hospitali au kumnunulia dawa, polisi wa Nakonde waligoma, na siku iliyofuata, alifika polisi asubuhi na kuelezwa kwamba ndugu yake alikuwa amekata roho.
Hii ni mara ya pili kwa miezi miwili kwa Watanzania kufanyiwa unyama.
Juni, David Mwamakomba, alipigwa risasi akiwa amelazwa chali na askari wa Nakonde. Kuna habari kwamba amehamishiwa wilayani Isoka.