Rais Jakaya Kikwete ameagiza Wakuu wa Mikoa na Wilaya, kusimamia ujenzi wa hosteli nyingi katika shule za sekondari za Kata, vinginevyo watoto wa vijijini hawatasoma.
Alisema kufikia mwakani (2007/2008), taifa litahitaji hosteli nyingi katika sekondari za Kata kutokana na idadi ya wanafunzi katika shule za sekondari nchini, kuongezeka maradufu.
Wataongezeka kutokana na mafanikio ya Mpango wa Kuboresha Elimu ya Msingi (MMEM), ambapo mwakani wale walioanza darasa la kwanza chini ya mpango huo, watamaliza.
Alisema hayo wakati akifunga Semina Elekezi kwa Wakuu wa Wilaya na Mikoa.
Alisema hosteli zitafanya watoto wa mbali kusoma kwa urahisi.
Alisema pia kuwa uzoefu umeonyesha kuwa vijiji vipo mbali hata katika Kata moja, hivyo dawa pekee ni kujenga hosteli.
Pia alisema hosteli zinapunguza tatizo la wanafunzi wa kike, kupata mimba ovyo.
Alisema hivi sasa wasichana katika sekondari za Kata, wanaishi kwa kupanga kwa watu, ambako wanakutana na vishawishi vingi na hatimaye kupata mimba, hivyo kuacha shule.
Akifafanua kuhusu wimbi hilo kubwa la ongezeko la wanafunzi sekondari, alisema ifikapo 2007/2008 vijana wapya watakaohitaji madarasa watakuwa 285,199, wakati nafasi zilizopo sasa zinatosha wanafunzi 230,963.
Kwa hiyo, watoto wanaotakiwa kutafutiwa madarasa hadi sasa ni 54,236.
”Maandalizi ya ujenzi wa shule zaidi za sekondari na hosteli yaanze sasa ili kukabiliana na wimbi kubwa la vijana watakaoingia kidato cha kwanza mwaka 2008,” alisema.
Alisema kazi mojawapo ya Wakuu wa Wilaya ni kusimamia masuala ya elimu, ikiwemo ujenzi wa madarasa na hosteli.
Pia, alisema kazi nyingine ni lazima iwe ni kuimarisha kilimo na alitaka wasimamie vizuri Programu ya Kuendeleza Kilimo (ASPD).