SIKU ya maombolezo imetangazwa nchini Ukraine, huku uchunguzi wa chanzo cha ajali ya ndege ya Russia iliyoua watu 170 mashariki mwa Ukraine ukianza.
Ndege hiyo ya abiria iliyokuwa na watoto zaidi ya 40 ilianguka karibu na mpaka wa Ukraine na Russia juzi na kuua abiria wote, Wizara ya Tahadhari ya Russia ilisema.
Ndege hiyo aina ya Tupolev Tu-154, inayomilikiwa na Shirika la Ndege la Pulkovo, ilianguka muda mfupi baada ya rubani kuripoti kuwapo kwa moto na moshi mkubwa ndani ya ndege.
Ilikuwa ikisafirisha abiria kwenda mji wa St. Petersburg kutoka mji maarufu wa pwani ya Bahari Nyeusi wa Anapa.
Wafanyakazi wa uokoaji walikimbilia eneo la ajali mara moja na walifanya kazi hadi usiku kujaribu kuwanusuru abiria pamoja na kukitafuta kiboksi cheusi.
Miili karibu 30 ilinasuliwa kutoka mabaki ya ndege hiyo, karibu kilometa 40 kaskazini magharibi mwa Jiji la Donetsk, wizara ilisema.
Walioshuhudia waliripoti kwamba hakukuwa na mlipuko kabla ya ndege hiyo kuanguka.
Gia ya kutua iligoma kufanya kazi wakati rubani alipojaribu kutua kwa dharura karibu dakika 20 kabla ya ajali.
Wizara imesema kuwa inachunguza iwapo ndege hiyo ilipigwa na radi. Watabiri wa hali ya hewa waliripoti kuwapo kwa ngurumo na radi eneo hilo la ajali.
Rais wa Russia, Vladimir Putin amemuagiza Waziri Mkuu, Mikhail Fradkov kuanzisha tume ya uchunguzi na alisema kwamba leo itakuwa siku ya maombolezo kwa nchi yake.
Ndege hiyo yenye injini tatu aina ya Tu-154 ndiyo tegemeo la biashara ya usafirisaji nchini hapa na inachukua karibu nusu ya idadi ya ndege zote za abiria za Russia.
Ilitengenezwa nyakati za utawala wa Kisovieti kushirikina na Boeing 727 na Trident, lakini ikiwa imeboreshwa uwezo wa kufanya kazi katika mazingira magumu yakiwamo shoti, njia mbovu za kurukia.
Pamoja na umaarufu wa ndege hiyo, imekuwa ikikumbwa na ajali mbaya ambapo tangu ianze kutoa huduma mwaka 1968 imekumbana na ajali mbaya zipatazo 30.
CNN