ASKOFU wa Jimbo Katoliki la Musoma, Mhashamu Justine Samba, amefariki dunia jana jijini Dar es Salaam, baada ya kuugua.
Katibu Mtendaji wa Idara ya Mawasiliano ya Baraza la Maaskofu Tanzania (TEC), Padri Revocatus Makonge, akizungumza kwa njia ya simu jana alisema, Askofu Samba alikuwa akisumbuliwa na ugonjwa wa moyo na figo.
Alisema, askofu huyo ambaye ni wa pili mzalendo wa jimbo hilo baada ya Askofu Mkuu Anthony Mayala aliyehamishiwa Jimbo Kuu la Mwanza, amekuwa askofu tangu mwaka 1989.
“Askofu alikuwa akipata matibabu kwenye hospitali za Aghakan na Regent, matibabu hayo yalikuwa ni maandalizi ya kumpeleka nchini India kwa matibabu zaidi ya moyo,” alisema Padri Makonge.
Askofu Samba alizaliwa wilayani Rombo Mkoa wa Kilimanjaro Desemba 12, 1950. Baada ya kuhitimu elimu ya msingi alijiunga na masomo ya sekondari katika Seminari ya Mtakatifu James, Kilema, Moshi mwaka 1965 hadi 1968.
Alijiunga na Seminari Kuu ya Kibosho kwa masomo ya falsafa na kisha nchini Kenya akisoma Tauhidi kwenye Seminari Kuu ya Mt. Thomas Aquinas. Alipewa daraja la upadri Januari 21,1974 katika Jimbo la Musoma.
Baada ya kufanya kazi za kitume miaka miwili, alijiunga na Chuo cha Ualimu Chang’ombe, Dar es Salaam, na kuhitimu Diploma ya Ualimu. Akiwa jimboni Musoma, alifundisha katika Seminari ndogo ya Mtakatifu Pius X Makoko tangu mwaka 1977 hadi 1986.
Mwaka 1986 alipelekwa Roma, Italia kwa masomo ya juu ya sheria za kanisa. Aliteuliwa kuwa Askofu wa Jimbo la Musoma Oktoba 25,1988 na kusimikwa Askofu wa Jimbo la Musoma Januari 6, 1989.
Enzi za uhai wake ameshika nyadhifa mbalimbali TEC; 1994-2000 amekuwa Mwenyekiti wa TEC, Mwenyekiti wa Tume ya Sheria za Kanisa tangu mwaka 2000-2005 na Mjumbe wa Bodi ya Hospitali ya Bugando tangu mwaka 1991 hadi 2006.
Mipango ya kusafirisha mwili wa marehemu kwenda Musoma kwa mazishi inafanywa na taarifa za mazishi yake zitatolewa baadaye