Na. Prosper Kwigize
Kibondo
Afisa mtendaji wa kijiji cha nyaruyoba katika kata ya Busagara Zacharia Filbert amekataliwa na wajumbe wa serikali ya kijiji kwa kile kinachodawa kushindwa kufanya kazi.
Kwa mujibu wa muhitasari wa kikao cha serikali ya kijiji kilichokaa tarehe 21 mwezi huu afisa huyo amedaiwa kutoshirikiana na viongozi pamoja na wananchi katika kuleta maendeleo..
Kikao hicho ambacho nakala ya mhitasari wake umepatikana katika mtandao wa www.habaritanzania.com, kimebainisha kuwa kiongozi huyo haendi kabisa sambamba na kauli mbiu ya serikali ya awamu ya nne ya ari, nguvu na kasi mpya na amekuwa kikwazo kwa maendeleo ya kijiji cha Nyaruyoba.
Aidha Bw, Zacharia anatuhumiwa kwa makosa makuu matatu ambayo ni kutotekeleza maagizo mbalimbali ya vikao vya kijiji, kutotoa taarifa ya mapato na matumizi, na kulewa pombe saa za kazi.
Afisa mtendaji huyo anatuhumiwa pia kukusanya ushuru na faini mbalimbali bila kutoa stakabadhi na kwamba pesa zinazotozwa kutokana na faini ya mifugo wanaozagaa huzitumia kwa maslahi binafsi bila taarifa.wala idhini ya serikali ya kijiji.
Bw. Zacharia pia anadaiwa kupokea Rushwa ya pombe kutoka kwa wananchi wenye shida na mwananchi asiyetoa hapewi huduma harali za kijiji na wakati mwingine afisa huyo hushiriki kucheza kamali.jambo ambalo ni kinyume na taratibu za nchi
Kikao cha wajumbe wa serikali ya kijiji hicho wamemtaka mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya Bw Paul Nkulila kumhamisha kituo cha kazi mtendaji huyo na wamependekeza achukuliwe hatua za kinidhamu.
Hii ni imekuwa ni desturi kwa wananchi pamoja na wajumbe wa serikali za vijiji wilayani Kibondo kuwakataa watendaji wa vijiji kwa tuhuma za uzembe na uzorotaji wa maendeleo katika vijiji vyao ambapo mwezi uliopita afisa mtendaji wa kijiji cha Kigendeka naye alikataliwa na wananchi na kushushiwa kipigo toka kwa wananchi wenye hasira.kwa madai ya kushindwa kutekeleza wajibu wake.
Jinamizi hili pia limewahi kuwakumba watendaji wa vijiji vya Kigogo na Mukabuye ambao walikataliwa na wananchi mara tu baada ya kuhamishiwa katika vituo vyao na kupelekea kuwepo kwa maandamano makubwa ya wananchi kupinga uhamisho wao kwa kile kinachodaiwa kuwa halmashauri imekuwa na desturi ya kuwahamishia watendaji wabovu katika vituo vingine vya kazi