WAZIRI wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Joseph Mungai, amesema hajawahi kuandika wala kusaini mkataba wowote unaohusu ubinafsishaji wa mashamba ya Mbarali na Kapunga.
Alisema Tume ya Rais ya Kurekebisha Mashirika ya Umma (PSRC) ndiyo yenye jukumu hilo kwa niaba ya serikali. “PSRC ndio wanaotangaza zabuni (tender) na kuteua wawekezaji kwa niaba ya serikali.
“Nakanusha tuhuma zilizotolewa dhidi yangu binafsi katika mojawapo ya magazeti ya kila siku katika toleo la tarehe 20 Agosti 2006 kama ifuatavyo: Sijawahi kuishinikiza Tume ya Rais ya Kurekebisha Mashirika ya Umma (PSRC) katika kutekeleza wajibu wake.
“Aidha, inafaa ieleweke kuwa tume hiyo haiko chini ya Wizara yangu ya Kilimo Chakula na Ushirika bali iko chini ya Wizara ya Mipango Uchumi na Uwezeshaji ambayo ndiyo yenye dhamana ya ubinafsishaji.
“Sijawahi kuomba wala kupokea rushwa ya aina yoyote kutoka kwa mtu yeyote, kama mwandishi wa habari hiyo anao ushahidi wowote autoe badala ya kunituhumu tu.
“Kuandika tuhuma nzito kama hizo bila kutoa ushahidi na bila hata kujaribu kupata maelezo ya yule anayetuhumiwa ni uandishi wa habari wenye mapungufu makubwa unaokiuka maadili ya fani hiyo.
“Uandishi unaofanywa bila kufuata maadili ya fani yenyewe ni hatari kwa jamii yetu inayotukuza ukweli, uwazi, heshima, utulivu na amani. Wajibu wa vyombo vya habari ni kutangaza na kutaarifu umma kuhusu mambo yaliyo sahihi na siyo kutumiwa kuchafua majina ya viongozi wa serikali,” alisema Mungai katika taarifa aliyoisaini.
Wizara ya Mipango Uchumi na Uwezeshaji inaongozwa na Dk. Juma Ngasongwa.
Waziri Mungai alisema anategemea PSRC watatoa maelezo kuhusu mchakato wa ubinafsishaji wa mashamba hayo kuanzia mwanzo hadi hivi karibuni yalipouzwa kwa wawekezaji.
Kwa mujibu wa waziri huyo, kwa sasa uuzaji wa mashamba umekwisha na inatarajiwa mashamba hayo yataanza uzalishaji msimu unaokuja chini ya wawekezaji walionunua na kuwa wizara yake inashirikiana na PSRC kuhakikisha kuwa walioyanunua mashamba ya Mbarali na Kapunga wanatekeleza makubaliano ya uwekezaji kwa mujibu wa programu zilizopo katika mikataba husika.