Chama cha Wananchi-CUF kimepania kuiga mbinu za ushindi zinazotumiwa na CCM ambapo sasa wameamua kuanzisha jumuiya za chama, badala ya mtindo wao wa kuwa na mabaraza.
Hatua hiyo imetangazwa na Profesa Ibrahim Lipumba jana wakati akifungua kikao cha siku mbili cha Baraza Kuu la Uongozi la Wanawake Taifa la CUF.
Kikao hicho kinaendelea makao makuu ya chama hicho Buguruni Jijini Dar es Salaam.
Profesa Lipumba alisema kuwepo kwa jumuiya kumeisaidia sana CCM kushinda katika uchaguzi mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani mwaka jana.
Alisema kwa upande wa Tanzania Bara, bado hakuna msisimko wa kutosha kisiasa kwa upande wa chama chake cha CUF. Alisema kwamba CCM inategemea kura nyingi toka kwa akina mama.
Hata hivyo alisema ingawa CCM inategemea kura nyingi za akina mama, wanawake hao ndio waathirika wakubwa kwa matatizo mbalimbali kama vile uzazi, afya, elimu na matatizo ya kupata huduma zingine za kijamii.
’Sasa tunahitaji kuwa na jumuiya zitakazojiendesha zenyewe, badala ya kuwa na mabaraza, hizi zitasaidia sana katika uhamasishaji wa kinamama,’ alisema.
Alitaja jumuiya tatu ambazo chama cha CUF kinatarajia kuwa nazo kuwa ni Wanawake, Vijana na Wazee.
Aliwaeleza wajumbe wa Baraza hilo kuwa ni lazima wawe na taasisi ya akina mama inayojiendesha yenyewe, ili wawahamasishe wanawake wenzao kushiriki kwa wingi katika siasa.
’Tumefanya maamuzi haya mapema ili kukipa nguvu chama hasa upande wa Bara,’ alisema na kuongeza Jumuiya itawaelimisha akina mama kuhusu matatizo yaliyopo pamoja na kujenga hoja kwa akina mama.
SOURCE: Nipashe