RAIS Jakaya Kikwete anatarajiwa kuondoka nchini leo kuelekea Angola kwa ziara ya siku mbili.
Taarifa iliyotolewa na Ikulu mwishoni mwa wiki ilisema kuwa ziara hiyo ni mwendelezo wa ziara zake katika nchi jirani na zilizo katika Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC) alizokuwa ameanza kuzifanya mapema mwaka huu.
Nchi ambazo Rais hakupata fursa ya kuzitembelea ni Angola, Zambia, Malawi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).
Hakwenda Malawi na DRC kwa vile kulikuwa na harakati za kisiasa, ikiwa ni pamoja na matayarisho ya uchaguzi mkuu DRC. Nchi nyingine, marais hawakuwapo kutokana na majukumu mbalimbali
Katika ziara hizo, Rais Kikwete huchukua fursa ya kujitambulisha kisiasa na pia kuelezea nia ya Tanzania kukuza na kufanya biashara kati yake na nchi hizo.
Rais Kikwete amefanya ziara za namna hiyo katika nchi za Botswana, Lesotho, Msumbiji, Namibia, Swaziland na Afrika Kusini.
Pia ameshazuru Kenya, Uganda, Rwanda na Burundi.
Katika ziara ya Angola, Rais ataongozana na mkewe, Mama Salma; Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Dk. Asha - Rose Migiro; na Waziri wa Utalii, Biashara na uwekezaji wa Zanzibar, Samia Suluhu Hassan.
Wengine ni Mbunge wa Ngara, Feethan Banyikwa (CCM); na Mbunge wa Manyoni Magharibi, John Lwaji (CCM).