VIONGOZI wa ngazi ya juu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano na ya Mapinduzi Zanzibar, kuanzia kesho watakuwapo Ngurdoto, kilometa 25 nje ya Jiji la Arusha kwa mkutano wa siku tano wa wakuu wa mikoa, makatibu tawala wa mikoa na wakuu wa wilaya.
Rais Jakaya Kikwete atafungua na kuwa mwenyekiti wa semina elekezi hiyo itakaojadili utekelezaji wa kazi za serikali ya awamu ya nne. Itamalizika Agosti 26.
Viongozi wengine watakaokuwapo ni Makamu wa Rais, Dk. Ali Mohammed Shein; Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Amani Abeid Karume; Waziri Mkuu, Edward Lowassa; na Waziri Kiongozi wa Zanzibar, Shamsi Vuai Nahodha.
Wakuu wa mikoa watakaoshiriki ni pamoja na wa mikoa mitano ya Tanzania Visiwani na wakuu wa wilaya za mikoa hiyo. Tanzania ina mikoa 26.
Baadhi ya mawaziri na makatibu wakuu ambao wizara zao zitatoa mada, pia watashiriki.
Jaji Mkuu, Barnabas Samata; Spika wa Bunge, Samuel Sitta; Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi, Jenerali George Waitara; na Mkuu wa Jeshi la Polisi, Inspekta Jenerali Saidi Mwema, ni miongoni mwa watakaotoa mada.
Madhumuni ya semina hiyo ni kuwapa nafasi wakuu wa mikoa, makatibu tawala wa mikoa na wakuu wa wilaya ya kupata malekezo kuhusu vipaumbele vya awamu ya nne, baada ya rais kukamilisha kupanga safu ya viongozi hao.
Kwa vile shughuli za maendeleo zimepelekwa kwenye halmashauri zilizo chini ya Serikali za Mitaa, viongozi hao wa mikoa ndiyo wasimamizi wa Serikali za Mitaa.
Karibu maandalizi yote yamekwishakamilika kwa ajili ya semina hiyo.
Semina ya aina hiyo imeshafanywa kwa mawaziri, naibu mawaziri na makatibu wakuu. Ilifanyika hotelini hapo Machi, mwaka huu.
Rais Kikwete tayari amekwishazitembelea karibu wizara zote na kutoa maelekezo ya utendaji kazi.
Waziri Mkuu, Edward Lowassa naye amekuwa akifanya ziara huku na kule kuhimiza utekelezaji.