RASHID Othman sasa ndiye Mkurugenzi Mkuu wa Usalama wa Taifa.
Anachukua nafasi ya Cornel Apson, ambaye anastaafu rasmi leo kwa mujibu wa sheria.
Uteuzi wa Othman umefanywa na Rais Jakaya Kikwete. Kabla ya kushika wadhifa huo mkubwa, Othman alikuwa Mkurugenzi wa Utawala na Utumishi katika Idara hiyo ya Usalama wa Taifa.
Taarifa ya uteuzi huo ilitolewa jana na Mkurugenzi wa Idara ya Habari (MAELEZO), Kassim Mpenda.
Hakuna maelezo yoyote ya wasifu wa Othman yaliyoweza kutolewa na serikali.
Apson amestaafu baada ya kushika wadhifa huo kwa mwongo mmoja. Mtangulizi wake ni Amran Kombe, ambaye aliuawa mwaka 1996 na polisi kwa madai kwamba walidhani ni mwizi wa magari aliyekuwa akitafutwa.
Apson alikuwa Mkuu wa Usalama wa Ndani kuanzia mwaka 983 hadi 1996.
Katika uteuzi mwingine, Rais Kikwete, amemteua Ludovick Utouh kuwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali. Uteuzi huo ulianza Agosti 19, 2006.
Anaziba nafasi iliyoachwa na Thomas Kiama, ambaye amestaafu kwa mujibu wa sheria. Uteuzi wake unaanza mara moja. Alitarajiwa kuapishwa leo saa 3 asubuhi.
Kabla ya uteuzi huo, Utoah alikuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Uhasibu na Ukaguzi wa Hesabu (NBAA), wadhifa ambao amekuwa nao tangu mwaka 1987.
Kabla ya wadfhifa huo, Utouh alikuwa Msajili wa Bodi ya NBAA.
Ameshakuwa Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo cha Maendeleo Mzumbe ambacho sasa ni Chuo Kikuu Mzumbe.
Katika uteuzi mwingine, Rais Kikwete, amemteua Anthony Itatiro kuwa Mnikulu. Uteuzi huo ulianza rasmi Agosti 19, 2006.
Aliyekuwa akishikilia wadhifa huo, Balozi Fanuel Kuzilwa, amestaafu kazi kwa mujibu wa sheria.
Kabla ya uteuzi huo, Itatiro alikuwa Naibu Mnikulu. Uteuzi huo nao unaanza mara moja.