KAYA 179 katika kata nne za Halmashauri ya Wilaya ya Songea Vijijini, Ruvuma hazina vyoo, hali ambayo inahatarisha afya za wananchi hao kupata magonjwa ya mlipuko.
Mratibu wa Huduma ya Afya ya Msingi (HAM) katika Tarafa ya Ruvuma, Abel Mapunda, aliiambia Tanzania Daima juzi kuwa waligundua tatizo hilo katika utafiti walioufanya katika kata hizo kupitia kampeni ya ‘piga kambi’ yenye lengo la kuhamasisha jamii kujenga vyoo na kuvitumia.
Alizitaja kaya ambazo hazina vyoo kuwa ni katika Kata ya Litisha ambako kaya 37 hazina vyoo, sawa na asilimia 13.6, Kata ya Kilaghano kaya 41 hazina vyoo, sawa na asilimia 10.4, Kata ya Maposeni kaya 66 hazina vyoo, sawa na asilimia 13.6 na Kata ya Lilambo kaya 35 hazina vyoo, sawa na asilimia 5.
Mratibu huyo alibainisha kuwa kutokana na hali hiyo, kampeni ya piga kambi katika kata hizo itaendelea, ili kuhamasisha wananchi kujenga vyoo na kuvitumia, ili kupunguza tatizo la magonjwa ya kuhara, ukiwamo wa kipindupindu katika tarafa hiyo.
Alisisitiza kuwa Tarafa ya Ruvuma kupitia mpango wa kuboresha afya ya msingi umejiwekea malengo ya kupunguza au kumaliza kabisa tatizo la ugonjwa wa kuhara ifikapo Desemba mwaka huu kupitia kampeni ya piga kambi.
Naye Katibu Tarafa ya Ruvuma, Abdula Mbawala, ameagiza kaya zote katika tarafa hiyo kujenga vyoo na kuvitumia na kwamba kaya yoyote ambayo haitakuwa na choo hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yake.