SHIRIKA la Nyumba la Taifa (NHC), linazidai wizara mbalimbali sh milioni 600 kwa ajili ya upangishaji katika nyumba zake.
Mkurugenzi Mtendaji wa NHC, Martin Madekwe, alibainisha hayo jana wakati wa uzinduzi wa Bodi Mpya ya Wakurugenzi ya Shirika hilo uliofanyika katika Makao Makuu ya NHC, Barabara ya Mandela, Dar es Salaam.
Hata hivyo, Madekwe hakuwa na kumbukumbu ya idadi kamili ya wizara zinazodaiwa na kiasi cha fedha kwa kila wizara.
Akizungumza wakati akizindua bodi hiyo, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, John Magufuli, aliitaka bodi hiyo kufuatilia madeni hayo ili fedha zitakazopatikana zitumike katika shughuli mbalimbali, ukiwamo ujenzi wa nyumba nyingine za NHC.
“Ni jukumu lenu kufuatilia madeni katika wizara yanayodaiwa ili makusanyo yatumike kwa shughuli mbalimbali za kuinufaisha nchi,” alisema Magufuli.
Sambamba na hilo, Magufuli aliwataka watendaji wa NHC kuendeleza ubia kwa kuyaendeleza majengo ili kuiwezesha miji kukua na kubadilika.
Magufuli aliitaka NHC kutoishia kujenga majengo ya ghorofa moja au tatu, bali ipige hatua kwa kujenga majengo yenye ghorofa nyingi.
“Jengeni ghorofa saba hadi mia moja, tutumie wataalamu wetu tulionao kubadilisha miji yetu,” alisema.
Aliwataka pia kutojenga mijini tu, bali wafike hadi wilayani na mikoa mbalimbali kwa lengo la kuwa na nyumba bora na za kisasa hivyo kuifufua NHC.
Alisema soko la nyumba lipo, linazidi kukua, na kwamba kinachotakiwa ni kujenga nyumba nyingi na za kisasa.
Pamoja na mambo mengine, Waziri Magufuli aliwataadharisha wananchi wanaotumia udanganyifu kwa kupanga nyumba za NHC wakati hawaishi katika nyumba hizo.
Katika uteuzi huo, Balozi Sulemani Hemed, ameteuliwa kwa mara nyingine kuwa Mwenyekiti wa Bodi hiyo mpya. Wajumbe ni Dk. Tumsifu Nkya, Elius Mwakalinga, Andrew Masawe, Mhandisi Consolata Ngimbwa, Blandina Nyoni, Blasi Seleki na William Ngeleja.