WAFANYAKAZI 16, wa kampuni binafsi ya ulinzi ya Yono Security ya jijini Dar es Salaam, wanamshitaki mwajiri wao, wakidai wamefukuzwa kazi kinyume cha sheria.
Kampuni hiyo ni miongoni mwa kampuni nyingi zinazomilikiwa na Mbunge wa Njombe Magharibi, Stanley Kevela (CCM).
Wafanyakazi hao wamefungua madai yao kwa Ofisa Kazi Mkoa wa Dar es Salaam, wakidai walifukuzwa kazi Agosti 5, mwaka huu bila kupewa stahili zao.
Kampuni hiyo ilimtuma mhasibu wake aliyejulikana kwa jina moja la Gunda, kwenda kwa Ofisa Kazi kujibu tuhuma hizo.
Mhasibu huyo, kwa niaba ya mkurugenzi wake, alisema kila mfanyakazi atalipwa sh 109,000 kama mafao yao kwa kipindi chote cha miaka mitatu walichofanya kazi. Mshahara wa kila mfanyakazi ni sh 48,000 kwa mwezi.
Wafanyakazi wanalalamika kuwa kiasi cha mafao walichopangiwa kulipwa ni kidogo.
Ofisa Kazi Mkoa ametaka wafanyakazi hao walipwe mishahara yao kuanzia siku walipoachishwa kazi, mapunjo ya mishahara yao, malipo ya muda wa ziada kazini, na malipo ya likizo.
Mkurugenzi huyo ametakiwa afike ofisini kwa Ofisa Kazi Agosti 24, mwaka huu.