JENERALI Liu Dongdong wa Jeshi la Ukombozi la Watu wa China (PLA), akiongozana na wajumbe tisa, anatarajia kuwasili kesho kwa ziara ya siku nne.
Jenerali huyo na wenzake, ni wageni wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ).
Taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari jana ilisema kuwa ziara hiyo ya kirafiki ina lengo la kukuza, na kudumisha uhusiano na ushirikiano uliopo kati ya Tanzania na China; na kati ya majeshi ya nchi hizo mbili.
Ugeni huo ukiwa nchini, utazuru mikoa ya Arusha na Dar es Salaam, na kuwa na mazungumzo na viongozi mbalimbali. Pia utatembelea vivutio vya utalii.
Ziara hiyo itaanzia Arusha ambako watatembelea maeneo ya utalii ili kujionea utajiri mkubwa wa wanyama.
Baadaye ujumbe huo utakwenda Dar es Salaam ambako kwa nyakati tofauti utakutana na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), Profesa Juma Kapuya, na Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi, Jenerali George Waitara.
Utakamilisha ziara yake kwa kutembelea Makao Makuu ya Kamandi ya Navy, Kigamboni ambako utaonana na Mkuu wa Kamandi hiyo. Pia utazuru Makao Makuu ya Mamlaka ya Reli ya Tanzania na Zambia (TAZARA).
Hii ni mara ya nne kwa Tanzania kupokea ujumbe kutoka Jamhuri ya Watu wa China kwa mwaka huu. Ujumbe wa kwanza uliwasili nchini Machi, ukiongozwa na Mkuu wa Mambo ya Nje, Jenerali Zhang Bhandong.
Uhusiano kati ya Tanzania na China ulianza tangu enzi za Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere; na Mao Tse Tung.