MTANDAO wa Jinsia Tanzania (TGNP), Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA) na mashirika mengine ya kijinsia wanapenda kutoa mchango wao kwenye gumzo lililozuka kuhusu mazingira ya kimaudhui yaliyoitawala filamu ya Darwin’s Nightmare inayozungumzia biashara ya samaki na habari ya umaskini wa wakazi wa Mkoa wa Mwanza.
Mjadala mkubwa umezuka kuhusu maudhui ya filamu hiyo, ingawa wananchi wengi bado hawajaiona. Tunataka kujiuliza kuna nini kimejificha katika maudhui yake na kwa nini imekuwa na malumbano?
Je, ni kwa manufaa ya nani filamu hiyo imetengenezwa? Imeambatana na inatufundisha siasa za mabara za kibeberu na mfumo dume? Haya ndiyo aina ya maswali tunayouliza na tunatumaini taarifa hii itawahamasisha na kutia watu moyo kufuatilia suala hili.
Filamu hii inazungumzia nini? Filamu hii ya Darwin’s Nightmare inaelezea biashara ya samaki inayoendeshwa na kampuni zinazomiliki viwanda vikubwa vilivyopo kandokando ya Ziwa Victoria, wakishirikiana na kampuni za biashara za samaki zilizopo Ulaya.
Filamu hiyo inaonyesha namna ambavyo kampuni hizo zilivyojinufaisha na biashara hiyo kwa kusafirisha samaki hao nje ya nchi, wakati wananchi wa Mwanza na nchi za jirani wakiendelea kuwa maskini.
Inaeleza pia kuwa, wakulima wamekuwa wakilazimishwa kuhama kwenye mashamba yao, ikiwa ni matokeo ya utandawazi, wakiacha wenye viwanda na wachimba migodi kuendelea kutumia maeneo yao, wakati wao wakienda mijini kufanya biashara za kimachinga na ukahaba, na watoto wao wakiishia kuwa watoto wa mitaani.
Jamii ya wavuvi inanyimwa haki yao ya kufanya uvuvi wao wa asili, hasa kwenye maeneo waliyozoea kwa kigezo kuwa wanaharibu mazingira. Matokeo yake watoto wao wanakimbilia mjini na kufanya biashara za ukahaba.
Filamu hiyo inaelezea kutokuwapo usawa huo kwa kufananisha namna ambavyo minofu minono ya samaki aina ya sangara inavyosafirishwa kwenda ng’ambo, huku wananchi wa Mwanza wakiachiwa vichwa vya samaki na mifupa, maarufu kama mapanki.
Filamu hii inaelezea kuwa biashara ya samaki imo kwenye ukanda wa biashara wa pembe tatu kati ya Ulaya, nchi za Kongo, Angola na Mwanza. Pembe tatu ambapo bunduki na risazi zinapakiwa kutoka Ulaya na kupelekwa nchi zilizo vitani, ambazo ni Kongo, Angola na nchi nyingine kwenye ndege zilizochakaa za Ulaya Mashariki, ambapo tena ndege hizi hubeba samaki kutoka Mwanza kurudisha Ulaya.
Mfumo huu wa biashara unafanana na mfumo wa biashara ya utumwa ya zamani, ambapo meli kutoka Mashariki ya Mbali zilileta nguo, silaha, shanga na vitabu vitakatifu Afrika na kuchukua pembe za ndovu, karafuu na watumwa kwenda Ulaya na bara Arabia.
Mfumo na usanii wa hali ya juu uliotumika kuitengeneza filamu hii unaifanya kuwa na hisia kali na mhemko mkubwa, hivyo kuchangia kutoa hisia nyingi tofauti za kutatanisha.
Ni sauti za kina nani zinasikika katika filamu hii? Filamu imejikita kwenye picha na mahojiano na kundi la wasichana wanaofanya biashara ya ukahaba, watoto wa mitaani na rubani wa moja ya ndege zinazosafirisha minofu hiyo ya samaki.
Filamu hiyo pia imefanya mahojiano na watu binafsi, wakiwamo mmiliki wa kiwanda cha kutengenezea samaki na mwandishi wa habari.
Kwa mtazamo wa haraka wa macho, ni nini cha kitofauti mno kuhusu habari hii? Ripoti za serikali kama ile ya Umasikini na Maendeleo ya Jamii ya mwaka 2003 na 2005 zimethibitisha kuwa idadi kubwa ya Watanzania hawajanufaika na ukuaji wa uchumi na kuwa kuna tofauti kubwa kati ya matajiri na masikini kutokana na sera za uchumi huria na ubinafsishaji.
Habari hizi zinabeba taarifa sawa kila siku; wakulima wanalazimishwa kuuza maharage bora zaidi Malawi na Zambia na kuacha maharage na mawe yasiyo na ubora ‘mapanki’ kwenye soko la ndani ya nchi sawasawa na kahawa na chai. Wananchi wengi hasa waishio vijijini wameshindwa kumudu maisha yao kutokana na athari za utandawazi.
Wananchi wengi wamepoteza ardhi zao kwa kampuni za utalii na migodi. Walionyanyasika na kuathirika zaidi ni wasichana na wanawake, wengi wao wamelazimika kuingia katika biashara ya ukahaba kwa kukosa shughuli mbadala ya kufanya, kama ambavyo vijana wadogo na wanaume wamefurika njiani kama wamachinga na wafanyabiashara wadogo wadogo na wafanyabiashara ya mapenzi pia.
Je, filamu hii ina matatizo gani? Tunaamini suala kubwa ni upungufu wake kutoshirikisha na kunakili ongezeko la harakati za jamii ya Kitanzania na makundi ya wanaharakati yanayotoa changamoto kwenye masuala mazima ya utandawazi na mfumo dume katika ngazi zote.
Zipo wapi sauti za wanaharakati wa nchini wa mazingira na haki za binadamu ambao wanapiga vita biashara ya kampuni kubwa za samaki, kutokana na kuharibu mazingira ya Ziwa Victoria na kuwatelekeza wavuvi wadogo wadogo kupata rasilimali zao za ziwa?
Zipo wapi sauti za vyama vinavyotetea haki za watoto wa mitaani bila kuchoka na vyama vya wanajinsia wanaotetea haki za wanawake Mwanza na kwingine, pamoja na haki za wafanyabiashara ya mapenzi?
Kwa nini basi filamu hii imeangalia tu upande mmoja wa jamii na kukandamiza jamii ya Kitanzania bila kuonyesha namna ambavyo wanawake, wanaume na watoto wa Kitanzania wanavyokazana kupinga hujuma zinazotokana na harakati za utandawazi, kukosekana usawa katika matabaka ya watu na mfumo dume?
Kama madhumuni ya mtayarishaji wa filamu ilikuwa ni kuangalia ubaya wa utandawazi kwa kuangalia habari ya biashara ya samaki wa Ziwa Victoria, kwa nini alishindwa kuwahusisha viongozi wa taasisi za kijamii, wanaharakati walio kinyume na utandawazi na watengenezaji wa filamu wa Kitanzania ili kupata picha halisi ya harakati dhidi ya utandawazi unaofanywa na Watanzania ili ionyeshe picha halisi ya harakati hizo?
Tunajiuliza pia, kwa nini mtayarishaji huyo hakuhakikisha kuwa filamu hiyo inaonyeshwa kwa Watanzania, hasa kwa kuwapa kipaumbele wao kwanza kwa sababu ni walengwa, hasa Watanzania wa Mwanza?
Majibu kwa maswali haya yanasaidia kuonyesha namna ambavyo filamu hii ilitayarishwa na kusambazwa katika mazingira ya mfumo wa ukoloni mamboleo. Hii inatuelekeza kwenye suala muhimu; je, filamu hiyo ina athari gani kitaifa na kimataifa? Katika ngazi ya kitaifa, filamu hii imewezesha kuweka wazi biashara ya samaki, hasa kwa wananchi ambao walikuwa hawajui habari ya biashara ya viwanda vya samaki wa Ziwa Victoria.
Katika mtafaruku ambao umegubika filamu hii, wauzaji samaki wakubwa wamefanikiwa kupata kuungwa mkono na jamii, kama tulivyoona kwenye maandamano ya halaiki kupinga. Imeonekana kwamba wamiliki, matajiri wa viwanda vya samaki wameonekana kuwa ndio walioonewa (victims) na si wanawake, wanaume na watoto maskini na waliowekwa pembezoni na kupoteza utu wao kutokana na umaskini uliokithiri.
Kutokana na siasa za mabara ya kibeberu, tunapaswa vile vile kujiuliza; ni nini matokeo ya mtazamo wa filamu hii kwa watazamaji wa Ulaya? Ni kweli kwamba watu wengi wenye nia njema – wanawake na wanaume wameacha kula sangara kutokana na ujumbe wa filamu hii?
Na kama ni hivyo, je, hii si kwa sababu za kibiashara za ushindani wa biashara Ulaya na kwinginepo ambako pia walifaidika awali na kufungiwa kwa uuzaji wa minofu ya samaki wa Ziwa Victoria na Umoja wa Ulaya?
Tunatambua utata ulipo kwenye kutengeneza na usambazaji wa filamu hii, tunatarajia utata uliojitokeza hautuondoi kwenye mtazamo wetu kwenye masuala makubwa ya msingi yaliyojitokeza kwenye filamu hii.
Kwa mfano, kati ya viongozi wa jamii ya wavuvi, kuna mvutano mkali katika eneo la ziwa juu ya nani amiliki samaki wanaopungua kila siku – wavuvi wadogo wa asili au kampuni kubwa za uvuvi wa samaki?
Nini kinahitajika kumaliza tofauti zinazoongezeka kati ya Watanzania wachache matajiri na wageni ambao wanaweza kuishi katika majumba makubwa ya kifahari na kula minofu ya samaki katika hoteli kubwa za kifahari za kitalii na maskini walio wengi?
Maskini na walio pembezoni wanaweza wakaongeza sauti na nguvu zao kumiliki rasilimali hizi na kuwa na maisha yenye heshima na utu, bila kulazimishwa kwenye biashara ya mapenzi au kuishi maisha ya kutegemea mitaani.
Sisi wote tunataka kuwe na mjadala wa sera ya ‘neo-liberal’, soko huria na ukuaji wa nguvu za ‘corporate-led’ utandawazi katika nchi yetu. Kama sehemu ya mjadala, Watanzania wote wanahitaji kujionea filamu hii ya Darwin’s Nightmare na kujadili maudhui yake.
Changamoto kubwa itakuwa kuitafsiri filamu hii kwenye Kiswahili na kusambazwa zaidi kwenye vituo vya televisheni na mahali pa video kuhakikisha kila Mtanzania anajumuishwa katika mjadala.
tamwa@raha.com