Na Seleman Bitala, Mwanza
WIZARA ya Mji nchini imetoa ushauri kwa TAMISEMI kuajiri wahandisi wenye utaalamu wa shughuli za maji.
Naibu Waziri wa Maji Shamsa Mwangunga aliyasema hayo katika majumuisho ya ziara katika Wilaya za Geita, Misungwi na Nyamagana ambayo ililenga kuangalia huduma za maji zilivyo katika wilaya hizo na mradi wa kupeleka maji katika miji ya Shinyanga na Kahama.
Hata hivyo, pamoja na jitihada zinazofanywa na Serikali kutoa maji kwa wananchi, Shamsa alisema bado Watanzania waishio vijijini wanashida ya kupata maji safi na salama yatokanayo na mabomba na wanakuwa na unafuu tu pale mvua zinaponyesha.
Akizungumzia tatizo la huduma hafifu za maji katika wilaya nyingi nchini, Shamsa alisema inatokana na kutokuwepo kwa wahandisi wa kutosha hali inayosababisha nafasi nyingi za uhandisi wilayani kukaimiwa na mafundi bomba.
Kuhusu utekelezaji wa sera ya kuwafikishia wananchi waishio vijijini huduma ya maji kwa asilimia 65 ifikapo mwaka 2020 alisema Serikali Kuu imeafikiana na serikali za mitaa kuendelea kutatua masuala ya maji kwa kutumia fedha zake na wafadhili.
Aliwakumbusha kwamba pamoja na Serikali kujitahidi kutekeleza ahadi za Chama tawala lakini maji ni gharama hivyo wananchi washirikishwe na kuchangia kidogo gharama, licha ya kwamba hivi sasa Serikali inasaidiana na nchi wafadhili kama Uingereza, Ufaransa, Japan na Benki ya Maendeleo ya Afrika (ADB) na Benki ya Dunia.