WATU wawili wamekamatwa visiwani hapa, wakifanya utapeli na kujipatia sh milioni 2.5, wakati walipojifanya maofisa usalama wa taifa, waliopewa kazi maalumu na Rais Jakaya Kikwete.
Watu hao; Khatim Mohammed Khatib (30) mkazi wa Magomeni mjini Unguja na Mohammed Mutalia (46) wa Fuoni, Wilaya ya Magharibi Zanzibar, walikamatwa baada ya kumtapeli Ali Hassan Rajab, wakimweleza ni wajumbe wa Tume Maalumu ya Usalama wa Taifa iliyoundwa na Rais Kikwete.
Baada ya polisi kuwakamata, walifikishwa Mahakama ya Mwanakwerekwe, mbele ya Hakimu Janet Sekihola, na kusomewa mashitaka ya kujipatia kima hicho cha fedha kwa njia ya udanganyifu.
Mwendesha Mashitaka wa Polisi, Haji Abdallah, alidai mahakamani hapo kuwa, washitakiwa walitenda kosa hilo eneo la Kibandamaiti Julai 31, majira ya saa 3:30 asubuhi.
Alidai kwamba watuhumiwa walifanikiwa kuchukua fedha, baada ya kujitambulisha kuwa ni maofisa wa tume hiyo maalumu, na wanahitaji kiasi hicho cha fedha.
Washitakiwa hao walikana mashitaka na Hakimu Sekihola aliwataka waandikishe dhamana ya maandishi ya sh milioni moja na mdhamini mmoja mwenye kitambulisho. Kesi hiyo itatajwa tena mahakamani hapo Agosti 21, mwaka huu na watuhumiwa wako nje.
Wakati huo huo, askari wa Jeshi la Kujenga Uchumi Zanzibar (JKU), Ali Shaha Ali (29), amefikishwa mahakamani, akituhumiwa kujihusisha na vitendo vya ujambazi. Askari huyo anatoka Makao Makuu ya JKU, Saateni mjini Unguja.
Ilidaiwa mahakamani na mwendesha mashitaka, Fatma Abdallah Hassan kuwa, askari huyo na wenzake walifanya shambulio la kumvamia mfanyabiashara Mohammed Nassor Suleiman Msumar na kuiba mali inayokisiwa kufikia sh milioni 20.5 mnamo Julai 4, mwaka huu, katika mtaa wa kibiashara wa Darajani