WAZIRI wa Viwanda, Biashara na Masoko, Nazir Karamagi, amegoma kutaja wamiliki wa kampuni ya kusafisha madini ya Mwananchi Gold Company Limited.
Badala yake, aliwataka wabunge na mwananchi yeyote anayetaka kujua wamiliki wa kampuni hiyo na hisa zao, waende Ofisi ya Msajili wa Kampuni (BRELLA) kujua wamiliki wa kampuni hiyo.
Waziri Karamagi alitoa jibu hilo juzi wakati akijibu hoja mbalimbali za wabunge waliochangia hotuba ya makadirio ya mapato na matumizi ya bajeti ya wizara yake kwa mwaka wa fedha 2006/2007.
Huku wabunge wakionyesha kutoridhishwa na majibu hayo, Waziri Karamagi alisema suala la kutaka kujua wamiliki wa kampuni hiyo na hisa zao, halina sababu ya kuletwa bungeni na kusisitiza kuwa, anayetaka kujua undani wa kampuni hiyo, ofisi ya BRELLA iko wazi kwa ajili hiyo.
Hoja ya kutaka kujua wamiliki wa kampuni hiyo, ambayo kwa siku za hivi karibuni imekuwa gumzo juu ya wamiliki wake, ilichangiwa na Mbunge wa Moshi Mjini, Philemon Ndesamburo (CHADEMA).
Ndesamburo wakati akichangia hotuba ya bajeti ya wizara hiyo, alisema kuna maneno mengi na baadhi ya vyombo vya habari vimeripoti kuwa kampuni hiyo inamilikiwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM), huku wengine wakidai kwamba inamilikiwa na baadhi ya vigogo wa serikali na CCM.
Alisema uanzishwaji wa kampuni hiyo umetokana na mkopo kutoka Benki Kuu ya Tanzania (BoT), hivyo Watanzania wana haki ya kujua nani wamiliki wa kampuni hiyo na hisa zao.
Ingawa Ndesamburo hakutaja hata jina moja la mmiliki wa kampuni hiyo, lakini mmoja wa wamiliki wa kampuni hiyo, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi, ni Waziri Mkuu wa zamani, Jaji Joseph Warioba.
Kampuni hiyo ilianzishwa mwaka jana na ilizinduliwa na Rais mstaafu wa awamu ya tatu, Benjamin Mkapa. Ipo eneo la Vingunguti na kazi yake kubwa ni kusafisha madini ya dhahabu na kuyaongeza thamani kabla ya kuuzwa nje ya nchi.
Kuanzishwa kwa kampuni hiyo ambayo wamiliki wake hawajawekwa wazi, kumetokana na mkopo wa mabilioni ya fedha kutoka BoT. Hoja kubwa ni jinsi mkopo huo ulivyotolewa wakati kampuni hiyo haina dhamana hata ya kiwanja kwani majengo wanayotumia pia ni ya kukodi.
Katika hatua nyingine, Waziri Karamagi alisema kati ya viwanda 108 vilivyobinafsishwa, vilivyonunuliwa na wazawa ndio vyenye matatizo makubwa nchini