Rais Jakaya Kikwete kesho anaanza ziara ya kikazi ya siku sita Mkoani Mara.
Akiwa Mkoani humo, Rais atazindua miradi mbalimbali ya maendeleo, kuhimiza shughuli za maendeleo pamoja na kuzungumza na wananchi katika mikutano ya hadhara.
Miradi ambayo Rais ataifungua ni wadi ya watoto na wazazi katika Hospitali ya Mkoa, kutembelea na kukagua shule ya Sekondari Bulhmba na kukagua shughuli za ukulima wa kisasa.
Aidha Rais akiwa mkoani humo, pia atakwenda wilaya ya Bunda ambako ataweka jiwe la msingi la Hospitali ya Wilaya na kufanya mkutano wa hadhara.
Baada ya kutembelea wilaya ya Bunda, Rais atakwenda wilaya ya Tarime ambako atakagua miradi ya ufugaji, kilimo na zahanati, kufungua shule ya Sekondari ya Bukama, na kuzindua jengo la Halmashauri na kuhutubia mkutano wa hadhara.
Rais pia atatembelea wilaya ya Serengeti ambako atafungua bweni la wasichana katika shule ya Sekondari ya Natta na kuhutubia mkutano wa hadhara.
Rais atarejea jijini Dar es Salaam Agosti 14.