Wakulima wadai kudharauliwa na halmashauri ya wilaya
Waeleza kuwa ingekuwa sikukuu ya wafanyakazi isingebezwa kisi hicho
Watishia kuandamana kudai haki yao ya kusherehekea
Wakati taifa la Tanzania likiazimisha sikukuu ya wakulima nane nane wilayani Kibondo hakuna kilichofanyika kuadhimisha siku hiyo.
Utafiti uliofanywa na vyombo vya HabariTanzania.com umebaini kuwa halmashauri ya wilaya haikufanya maandalizi yoyote kuhusiana na siku ya wakulima kitendo kilichosababisha usumbufu mkubwa kwa wakulima.
Jumla ya vikundi kadhaa vya ngoma na michezo mbalimbali ambavyo vilivyoalikwa kushiriki maazimisho hayo vimejitokeza na kujikuta havimpati kiongozi yeyote katika ngazi ya kata wala wilaya.
Wakiongea kwa jaziba na masikitiko wakulima hao waliofika makao makuu ya wilaya kwa ajili ya kuifurahia sikukuu yao wameilaumu serikali kwa kutowathamini wakulima.
Akiongea na Mtandao wa HabariTanzania.com kwa niaba ya wakulima hao, Bw. Chrisostom Noel mkazi wa kijiji cha Biturana amesema wao kama wakulima wanasikitishwa na kitendo cha wilaya kutothamini mchango wao katika taifa na kuwanyima nafasi ya kuadhimisha nanenane kiwilaya
Mratibu wa sherehe hizo wilaya Bw.Julius Chalya ambaye ni Afisa kilimo wilaya Amemwambia mwandishi wa HabariTanzania.com ofisini kwake kuwa sherehe hizo zinaadhimishwa katika kila kata na si kiwilaya, hata hivyo amekiri kutuma wawakilishi katika maadhimisho kimkoa wilayani Kasulu..
Naye Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya Bw Simon Kanguye alipouliuzwa kuhusu sababu za kutofanyika maadhimisho hayo amesema awali ilipangwa kufanyika kiwilaya mijini Kibondo lakini baadaye alipata taarifa kuwa kila kata itajitegemea.
Kwa upande wao chama cha wafanyabiashara, wenyeviwanda na wakulima TCCIA wilayani Kibondo wameelezea kusikitishwa kwao kwa kutoshirikishwa kwa lolote juu ya sherehe hizo na kuongeza kuwa wamekuwa na wakati mgumu sana kutafuta mawasiliano na DED (mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya) bila mafanikio.
Katibu wa TCCIA wilaya Bw. Robert Ntendeli akiongea na waandishi wa Habari katika ofisi za kata ya Kibondo mjini amesema hadi majira ya saa sita mchana hakufanikiwa kumuona afisa mtendaji wa kata hiyo Sylvester Katunzi ili kujua kulikoni kwa kile kilichoelezwa kuwa yuko katika mapumziko ya nane nane.
Hata hivyo Bw. Ntendelei amebainisha kuwa alifanya mawasiliano na mkuu wa wilaya ya Kibondo luteni kanali John Mzurikwao ambaye alijibu kuwa sikukuu ipo na shughuli zote ziko chini ya ofisi ya mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya.
Pamoja na majibu yaliyotolewa na viongozi hao wa ngazi ya juu wilayani Kibondo uchunguzi uliofanywa katika baadhi ya kata umebainisha kuwa hakuna maadhimisho yanayofanyika katani.
Juhudi za kumpata mkurugenzi wa halmashauri kujibu hoja hiyo hazikuzaa matunda na mwandishi wa HabariTanzania.com anaendelea kumtafuta ili kujua undani wa kuwanyima heshima na haki yao ya msingi wakulima wilayani hapa.