MFANYABIASHARA maarufu wa Zanzibar, Mohammed Raza, amesema vigogo wanaoingiza dawa za kulevya Zanzibar bado hawajaguswa, na kwamba wanaokamatwa ni watumiaji wadogo wadogo (mateja).
Raza alisema hayo alipokutana na Mkuu wa Jeshi la Kujenga Uchumi Zanzibar (JKU) na kukabidhi zawadi za askari wa kikosi hicho waliomuokoa na familia yake, baada ya kuvamiwa na majambazi Julai 12 mwaka huu nyumbani kwake Kibweni, nje kidogo ya mji wa Zanzibar.
Raza alisema kwamba, tatizo la dawa za kulevya ni kubwa Zanzibar na kuna haja kwa jamii hivi sasa kuvunja ukimya na kuwafichua wanaoingiza dawa hizo kutoka nje ya Zanzibar.
Aliahidi kwamba, kuanzia hivi sasa yuko tayari kutoa zawadi ya sh milioni 10 kwa mwananchi atakayefichua jina la mfanyabiashara mkubwa anayejishirikisha na dawa za kulevya Zanzibar.
“Lazima tuwe na tabia ya kutoa habari za vigogo wa dawa za kulevya, kuanzia sasa niko tayari kumzawadia sh milioni 10, mtu atakayemfichua mfanyabiashara mkubwa wa dawa ya kulevya,” aliahidi Raza.
Mfanyabiashara huyo ambaye aliwahi kuwa Mshauri wa Rais mstaafu wa Zanzibar, Dk. Salimin Amour Juma, alisema kinachojitokeza Zanzibar hivi sasa ni kukamatwa watumiaji wadogo wadogo, maarufu kama mateja, na kuachwa wale wakubwa ambao ndio hasa wanaoziingiza.
“Taarifa zinazotolewa lazima ziwe za wafanyabiashara wakubwa, hivi sasa wanaokamatwa ni vidagaa na machangu na mapapa bado hawajakamatwa,” alisema Raza.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mkuu wa JKU, Kanali Makame Mabrouk, alisema zawadi za mfanyabiashara huyo zitaongeza ari ya askari wake katika kulinda usalama wa nchi, raia na wawekezaji vitega uchumi.
Aliahidi kwamba kikosi hicho kitaendelea kushirikiana na vikosi vya ulinzi vya Jamhuri ya Muungano na vile vya Zanzibar, ili kuhakikisha Zanzibar inabaki kuwa na amani na inatawalika.
Akizungumzia kauli ya Raza, jana Naibu Mkurugenzi wa Haki za Binadamu na Mawasiliano ya Umma wa CUF, Salim Bimani, alisema ahadi hiyo ni changamoto kwa wananchi, lakini akasema tatizo kubwa ni kukosekana kwa nia njema kati ya wananchi na vyombo vya dola.
Alidai dawa za kulevya zinapitishiwa uwanja wa ndege na bandarini, ambako kuna vyombo vya ulinzi, vikiwamo vikosi, lakini bado ‘unga’ unapenya na kuwaathiri vijana wengi.
‘“Unga’ unauzwa mitaani, na wanaotumia wanajulikana, tatizo ni kwamba wananchi wamepoteza nia njema na vyombo husika vya ulinzi na usalama,” alisema Bimani.
Hivi karibuni, Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Sultan Mohammed Mugheiry, alisema idadi ya vijana wanaoathirika kwa matumizi ya dawa za kulevya imekuwa ikiongezeka mwaka hadi mwaka.
Alisema wastani wa watu 1,000 Zanzibar hukumbwa na ugonjwa wa akili, ambapo wengi wao ni waathirika wa matumizi ya dawa hatari za kulevya.
Habari zaidi zinasema kwamba, mbwa walioletwa Zanzibar kutoka Afrika Kusini kunusa dawa za kulevya, hawapelekwi bandarini wala uwanja wa ndege kunusa mizigo, baada ya wananchi wengi kupinga kutokana na imani za kidini.
Mbwa hao wanadaiwa kuwa hula kilo tano za nyama kila siku, lakini wanashindwa kufanya kazi ingawa uwezo wao ni mkubwa