KITUO cha Uwekezaji Tanzania (TIC), kimesema kukosekana kwa watawala wengi Watanzania katika hoteli za kitalii nchini, kunasababishwa na kutokuwapo vyuo vinavyozalisha wataalamu hao.
Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mtendaji wa TIC, Emmanuel ole Naiko, alisema waligundua tatizo hilo baada ya kuwauliza wamiliki hao sababu za kutokuwapo mameneja wazalendo katika hoteli zao.
Ole Naiko alisema kwamba, wengi wa wamiliki wa hoteli hizo walikuwa wakiilalamikia sekta hii nchini kwa kutokuwapo Watanzania wenye uwezo na sifa za kushika nafasi hizo.
“Wawekezaji hao walijitetea kwa kusema kuwa wafanyakazi wengi wanaofanya kazi katika hoteli zao ni wale wasiokuwa na sifa za kuwa mameneja,” alisema Ole Naiko.
Aliongeza kuwa, wamiliki hao waliwalalamikia wafanyakazi wengine kughushi wasifu wao, kuonyesha wana uwezo wa kufanya kazi hizo, lakini wanapofika kwenye kazi wanakuta hawazimudu.
Alieleza kuwa wamiliki wa hoteli hizo wamesema kuwa, Watanzania wenye uwezo wa kufanya kazi hiyo si waaminifu, na kwamba wengi wao ni wezi.
Kuhusu malalamiko ya ubaguzi au kuwapo machangudoa, Ole Naiko alisema wenye hoteli walieleza kwamba tatizo ni kubwa, ambapo machangudoa wamekuwa wakipenya bila kutambulika, hadi wanapowagongea milango wageni na kuwaghasi.
Ili kudhibiti hali hiyo, imeshauriwa kwamba wageni wote wanaoingia watozwe kiingilio, lakini pia ziwekwe kamera maalum, kudhibiti mienendo ya wageni wote katika hoteli, ili kuwaondoa machangudoa hao.
Tatizo jingine la viongozi wazalendo, ni tabia yao ya kuhamahama. Mwekezaji wa Hoteli ya New Africa alisema mwanzo alikuwa na wafanyakazi 300, lakini baada ya miaka 10 wamebaki 35 tu.
Whitesands walisema walianza na wafanyakazi wazalendo 200, lakini sasa wamebaki 25, kutokana na wafanyakazi hao kuamua kuhamahama.
Kutokana na tatizo hilo, Serikali ya Tanzania, kwa msaada wa Ufaransa, inajiandaa kujenga chuo cha utalii baada ya mwaka mmoja, ili kuongeza wataalamu kwenye fani hiyo.