PAMOJA na kauli zake nzito, vitisho na kujidai kwingi, imeelezwa kwamba, Kiongozi wa genge la kigaidi la Al - Qaeda, Osama bin Laden ni mwoga, pengine kuliko mtu yeyote.
Wapiganaji wenzake, Mujahidina, wamekuwa wakimcheka nchini Afghanistan, kutokana na kukithiri kwa woga wake, kiasi cha kujifungia mbali au hata kukimbia na kushtuka kupita kiasi mashambulizi yanapofanywa na adui zao.
“Osama akisikia milipuko, alikuwa anaruka juu, anakimbia mbali sana. Bado nakumbuka kwamba mimi, kaka zangu wakubwa na wadogo, tulikuwa tunacheka,” Hutaifa Azzam, rafiki wa siku nyingi wa Osama aliiambia CNN.
Azzam ni mtoto wa mlezi wa Osama katika Uislamu wa siasa kali, Abdullah Azzam. Baba huyo na Osama, kwa pamoja waliunda kundi la Mujahidina, ambalo baadaye lilikuja kuwa Al - Qaeda.
Abdullah aliuawa mwaka 1989 pamoja na kaka wawili wa Hutaifa, na kifo chao kilitokana na bomu linalodhaniwa kupigwa na jamaa wa karibu wa Osama, wenye asili ya Misri.
Ukweli wote huo kuhusu Osama na mambo mengine, unatarajiwa kuonyeshwa Agosti 23 mwaka huu, katika makala maalumu iliyoandaliwa na mtaalamu wa uchambuzi wa masuala ya ugaidi. Kimeandikwa pia kitabu: ‘The Osama bin Laden I know’.
Rafiki wa Osama, wanamwelezea kama mtu aliyepoteza mamilioni ya fedha na sasa anaishi kwa shida, akiwa amejiweka tayari kwa maisha ya jihad, akijaribu kupambana na mataifa ya Magharibi.
Katika maelezo mengine ya makala hiyo, mtu aliyesoma shule na Osama enzi hizo kisha wakaja kuwa wapiganaji katika Al - Qaeda, Khaled Batarfi, ana haya ya kusema:
“Kwa pamoja tuliangalia sinema za Cowboy, karate…picha nzuri nzuri na action kama za kina Bruce Lee na wacheza kung fu.”
Hata hivyo, imedhihirika sasa, si wote katika familia ya Osama, wanaopenda maisha ya kuwa wakitafutwa kila wakati, na hiyo ilibainika baada ya yeye kutangaza vita dhidi ya Marekani.
Bergen alisema kwamba, mtoto wa Osama mwenye umri wa kati ya miaka 20, Omar, alisikitishwa mno na mashambulizi ya Septemba 11 nchini Marekani, akaikimbia Afghanistan kwenda kuishi Saudi Arabia, ilipokuwa wazi kwamba Rais George W. Bush angeipiga Afghanistan.
“Omar, kimsingi alimwambia baba yake (Osama), ‘mashambulizi haya ni upuuzi, hayatusaidii chochote, tazama sasa tunaandamwa na kipigo.’” Baada ya kusema hayo, alinawa mikono, akaondoka akakimbilia Saudia.
Osama amekuwa akionekana kwenye mikanda ya video au sauti yake kwenye redio, akitishia kuipiga Marekani na washirika wake. Hata hivyo, kwa sasa hajulikani alipo, hata Bush hajui yuko wapi, na wengine wanadhani labda ameshafariki dunia.
Wakuu wa Pakistan wanadai kwamba yuko kwenye mapango yasiyofikika kirahisi kati ya mpaka wake na Afghanistan, akiwa amebakiwa na wasaidizi wachache. Mara ya mwisho alionekana wa akitumia mkongojo, nywele zikiwa mvi nyingi, kuonyesha umri unakwenda. Kuna kipindi alionekana vilimani akiwa amepanda punda.