Rais Jakaya Kikwete, leo atalihutubia Taifa kwa kuzungumza na Wazee wa Mkoa wa Mwanza.
Mazungumzo kati ya Rais na Wazee hao, yatafanyika saa 10:00 jioni katika ukumbi wa Chuo cha Benki Kuu (BoT), Jijini Mwanza.
Taarifa ya Ikulu Jijini Dar es Salaam ilisema, hotuba hiyo ni mwendelezo wa utaratibu wake aliojiwekea wa kuzungumza na wananchi kila mwisho wa mwezi.
Taarifa ilifafanua kuwa, mazungumzo hayo yatarushwa moja kwa moja na kituo cha Televisheni cha Star TV na Radio Tanzania Dar es Salaam (RTD).
Katika hatua nyingine, akiwa mkoani Mwanza, Rais atakitumia kipindi cha kuanzia Agosti Mosi hadi 6, mwaka huu kwa mapumziko mafupi.
Taarifa ilifafanua kuwa, pamoja na kuwa katika mapumziko, Rais atakuwa na ratiba nyepesi ya kutembelea Kiwanda cha Kusindika Minofu ya Samaki na Kiwanda cha Nguo cha Mwatex.
Ilisema Agosti 7, mwaka huu, Rais ataondoka mkoani Mwanza na kwenda mkoani Arusha ambako siku inayofuata, atakuwa mgeni rasmi katika maadhimisho ya Wakulima yaani Nane Nane.
Ilifafanua kwamba, kuanzia Agosti 9, mwaka huu, Rais Kikwete ataanza ziara ya kikazi mkoani Mara kukagua shughuli mbalimbali za maendeleo.