Serikali imewaagiza viongozi wake kushirikiana na vyombo vya habari ili kuwawezesha wananchi kufahamu kazi zinazofanywa na Serikali yao.
Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Mawasiliano Ofisi ya Rais Ikulu, Balozi Peter Kalaghe wakati akifunga mafunzo ya siku tano kwa Maafisa Mawasiliano wa Wizara mbalimbali katika Chuo Kikuu Kishiriki cha Habari na Mawasiliano.
Kadhalika, Balozi Kalaghe amewataka mabosi hao kuacha tabia ya kuvikimbia vyombo vya habari na kujipanga upya ili kwenda sambamba na kasi iliyopo.
Amesema kutokana na ukuaji wa teknologia ya habari duniani kote, Serikali imeamua kuvitumia vyombo hivyo kikamilifu na kwa kuanzia imeanza kutoa mafunzo kwa maafisa hao ili wawe kiungo muhimu kati ya Serikali na wananchi.
’’Wakati umefika kwa mabosi kuacha tabia ya kutofanya kazi na vyombo vya habari, kinachotakiwa sasa ni kujipanga upya ili tuweze kuwapatia habari wananchi juu ya nini Serikali yao inafanya,’’ akasema.
Aidha, Balozi Kalaghe amewaambia maafisa hao kuwa Ikulu inaamini mafunzo hayo yaliyowachukua siku tano, yatawafanya wabadilike na kuwa watu wapya katika utendaji wa kazi zao na kuachana na utendaji waliouzoea wa kuogopa kutoa habari hata kama wamepewa uwezo huo.
Pamoja na hayo, akasema Serikali kwa kutambua ina wajibu wa kutangaza sera zake ndani na nje ya nchi itaendelea kutoa mafunzo zaidi kwa maafisa wake kutoka ngazi ya Wizara hadi Mikoa.
Kwa mujibu wa Mratibu wa Mafunzo hayo, Afisa katika Kurugenzi ya Mawasiliano Ofisi ya Rais Ikulu Bi. Asha Mtwangi, mafunzo hayo yamefadhiliwa na Shirika la Kimataifa la UNDP na yana lengo la kuoboresha utawala bora katika wizara zote.
Wakati wa mafunzo hayo, maafisa hao waliweza kutembelea vyombo vya habari, taasisi na mashirika kadhaa ili kujionea njia mbalimbali zinazotumika katika uotoaji habari kwa wananchi