Bibi kizee anayekadiriwa kuwa na umri wa kati ya miaka 70 na 74 amegongwa na gari wakati alipokuwa akivuka barabara akiwa mbioni kwenda kumwona Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Bwana Jakaya Kikwete aliyekuwa anatembelea maeneo hayo.
Tukio hilo la kusikitisha lilitokea dakika chache kabla ya msafara wa Rais Jakaya Kikwete kuingia katika kiwanda cha nguo cha Urafiki, Jijini.
Bibi huyo aliyekuwa akitokea kwenye maghorofa ya Urafiki aligongwa wakati akiwa katikati ya barabara kwenye michoro ya zebra mbele ya lango kuu la kiwanda hicho.
Alasiri iliyokuwa maeneo hayo ilishuhudia gari aina ya Isuzu Journey lenye namba T 330 ALN lililokuwa likitokea Ubungo kuelekea Manzese, likimzoa bibi wa watu na kumtupilia mbali.
Alasiri ilishuhudia gari hilo likimgonga bibi kizee huyo na kumpaisha mita kadhaa mbele kisha kupaparamia tuta na kutokomea ili kukwepa kudakwa na polisi.
Habari zaidi zinasema bibi huyo alikuwa anaelekea kiwandani hapo kusubiri kumwona Rais Kikwete aliyekuwa anakaribia kufika eneo hilo.
Katika hatua nyingine baadhi ya wafanyakazi wa kiwanda cha nguo cha Urafiki waliokuwa wamepania kumpasulia dukuduku lao Rais Jakaya Kikwete walijikuta wakigonga mwamba.
Wafanyakazi hao walikuwa wamepanga kumweleza matatizo yao Rais ikiwa ni pamoja na mgogoro uliokomaa kiwandani hapo.
Rais alitembelea kiwanda hicho na kujionea hali halisi ya shughuli zinazofanywa humo ambapo pia aliwasisitiza wawekezaji hao kununua pamba za ndani na kuuza nguo nje ya nchi.
Hadi Rais anaondoka kiwandani hapo wafanyakazi hao walikuwa bado langoni wakisubiri upenyo ili waweze kuongea naye, bahati ambayo hawakuipata.
Na huko Tegeta, Rais Kikwete alipokelewa na mabango kutoka kwa wafanyabiashara wa soko la zamani la Tegeta yaliyokuwa na ujumbe wa kupinga kuhama katika soko hilo.
Mabango hayo yaliyokuwa yamebeba ujumbe wa kupinga kuhamishwa katika soko la zamani na kuelekea katika soko jipya yalikuwa yakisomeka hivi:
’’Tunapinga kuhamishiwa katika soko jipya,’’Sokoni Tegeta rushwa inanuka’’.
Kana kwamba hiyo haitoshi, Rais pia alikumbana na mabango ya wachimba kokoto wa Kunduchi ambayo yalikuwa yakipinga amri ya kuwahamisha katika machimbo hayo.
Hata hivyo, Rais Kikwete hakuwalazia damu, akaamua kuwapasha hapo hapo na kuwataka kushusha mabango yao chini.