'Wauzwa' na mtoa habari kama kuku mdondo eneo la tukio
Na Subira Mtandi, Morogoro
JESHI la Polisi Mkoa wa Morogoro, linashikilia watu watatu akiwamo askari wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), askari wa Jeshi la Polisi na mfanyabiashara kwa tuhuma za kutaka kufanya wizi wa kutumia silaha.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jana, Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Morogoro, Bw. Thobias Andengenye, alisema tukio hilo lilitokea Julai 26 mwaka huu saa 4 asubuhi katika maeneo ya Sangasanga Njia Tatu barabara kuu iendayo Iringa.
Kamanda Andengenye aliwataja watu hao kuwa ni mfanyabiashara Amani Athumani (37) ambaye ni mkazi wa Sultani Area, Askari wa JWTZ Pangawe ambaye pia ni dereva, MT 5991 Koplo Maige Robert (39) na askari polisi wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) E 9939 KonsteboAmoud Said (33).
Kamanda Andengenye alisema waliwanasa watu hao kutokana na mtego ulioweka na Jeshi hilo baada ya kupata taarifa kutoka kwa raia mwema, kuwa kuna watu wana bunduki aina ya SMG na wanatafuta kazi ya uhalifu ambayo itawaingizia fedha nyingi.
Alisema baada ya kupata taarifa hiyo, Polisi ilimpandikiza mtu ambaye ni askari, na walimtaka ajifanye kuwa Mhasibu wa SACCOS ya Kilombero na anakuja kuchukua sh. milioni 100 CRDB.
Alisema baada ya kukamilisha kila kitu, mtu huyo aliwapigia simu watu hao na kuwaambia kuwa amefanikiwa kupata sh. milioni 42 tu, na muda huo anaondoka na wakitaka kujua gari wanalosafiria, watakapofika Sangasanga Njia Tatu, watapaki na kufungua boneti ya gari lao.
Alisema wakati huo, Koplo Maige alikuwa ameshakwenda kazini kwake na kuomba ruhusa kuwa amepata dharura na anataka kusafiri, aliporuhusiwa walikwenda kutafuta usafiri yeye na mwenzake.
Kamanda Andengenye alisema walikuwa wakitumia gari aina ya Toyota Chaser namba T 706 AJU mali ya Konstebo Said, ndipo wakaanza safari hadi Sangasanga Njia Tatu na kulikuta gari hilo limefunguliwa boneti, wakapaki gari lao na kumfuata mtu huyo, ili waweze kuzichukua 'fedha' hizo.
Kamanda alisema kabla hawajakaa sawa, walivamiwa na gari la Polisi lililokuwa na askari ambalo lilikuwa limefichwa karibu na eneo hilo la tukio na watu hao wakatiwa mbaroni.
Alisema walipowapekua waliwakuta na risasi za bunduki aina ya shotgun, kisu cha kukunja chenye mpini mweusi na manati moja.
Awali watu hao walielewana na mtoa taarifa huyo, kuwa wawe na bunduki, kwani kwa kutokuwa nayo ingeonekana kuwa waliibiwa kizembe, hivyo walimhakikishia kuwa watakuwa na bunduki, lakini badala yake hawakwenda nayo.
Hivyo, alisema walikuwa na manati ili baada ya kuchuka fedha hizo wapige kioo cha gari kwa kutumia manati hayo na kisha waache risasi na kisu kwenye gari ili askari wakija wajue aliibiwa na watu waliokuwa na silaha.
Alisema baada ya kukamatwa, Konstebo Said alipohojiwa, alisema yeye alikodishwa na wenzake, ili awapeleke shamba maeneo ya Melela.
Polisi bado inaendelea na uchunguzi zaidi wa tukio hilo, ili waweze kuwafikisha watu hao mahakamani.