Na Mwandishi Wetu
RAIS wa Moro United, Ismail Rage ameunga mkono kauli ya Naibu Waziri Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Ali Juma Shamuhuna kuwa wachezaji wa timu ya soka ya Taifa (Taifa Stars), hawafundishiki, wamechoka.
Akizungumza Dar es Salaam juzi, Rage aliyepata kuwa Katibu Mkuu wa Chama cha Mpira wa Miguu Tanzania (FAT), ambayo sasa ni Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), alisema kwa muda mrefu lawama kuhusiana na kudorora kwa soka zimeelekezwa kwa viongozi bila kuwatazama na wachezaji.
"Kila siku tunasema viongozi ni chanzo cha kushuka kwa soka, hilo nalikubali limesemwa sana, lakini tutazame na wachezaji wetu nao.
"Wachezaji hawapo makini, hawajui wanalotakiwa kufanya, wapo tu, matatizo yanaanzia na kwa wachezaji, Naibu Waziri Kiongozi yupo sahihi kabisa.
"Kauli yake imenifurahisha na namuunga mkono kwa aliyozungumza, wachezaji wetu ni matatizo makubwa," alisema Rage ambaye pia amepata kuwa Makamu wa Pili wa Rais wa TFF.
Juzi Shamuhuna alikaririwa na gazeti hili akisema wachezaji wa Taifa Stars hawafundishiki na kwamba hata wakija makocha maarufu kutoka Brazili, Ufaransa na kwingineko hawawezi kuibadili ikafanya maajabu, badala yake alishauri waanze kuandaliwa vijana mapema kwa ajili ya timu hiyo.
"Unaweza ukawaletea kocha kutoka Brazili, Ufaransa, lakini wachezaji hawa hata ABC za mpira hawazijui, mtawalaumu bure makocha wa kigeni," alikaririwa Shamuhuna.
Alisema inahitajika mipango ya muda mrefu kuanzia timu za vijana na kwamba hilo likifanyika itakuwa rahisi kwa makocha kutoka nje kukuta wachezaji wameiva.
Kocha mpya wa Taifa Stars, Mbrazili, Marcio Maximo aliwasili Dar es Salaam juzi na kusema Watanzania wasitarajie miujiza kwa sababu soka inahitaji maandalizi.