Na Prosper Kwigize, Kibondo
HALMASHAURI ya wilaya ya Kibondo imeiagiza idara ya maji wilayani humo kuhakikisha huduma ya maji inapatikana katika kipindi cha wiki mbili zijazo kabla baraza la madiwani halijawachukulia hatua za nidhamu.
Agizo hilo lilitolewa jana wakati wa kikao cha baraza la madiwani, kufuatia kutokuwepo kwa huduma ya maji mjini Kibondo kwa kipindi cha zaidi ya mwezi mmoja bila sababu zinazoeleweka.
Akitoa tamko hilo, mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya hiyo, Simon Kanguye, alisema idara ya maji imekosa sababu ya msingi ya kuwakosesha maji wananchi na kwamba ipo haja ya kuwachukulia hatua wakuu wa idara hiyo, kwa mujibu wa taratibu za utumishi wa umma.
Baraza limemtaka mhandisi wa maji wilaya na meneja wa Mamlaka ya Maji Mjini, kuhakikisha mashine zilizopo zinafanya kazi na kuondoa tatizo hilo la ukosefu maji.
Baraza la madiwani limesikitishwa na kitendo cha idara hiyo kutotoa huduma ya maji licha ya kununuliwa kwa mashine mpya za kusukuma maji zilizogharimu mamilioni ya shilingi.
Wakati huo huo, mganga wa wilaya ya Kibondo ametakiwa kuhakikisha vyombo vya mawasiliano vilivyoko kwenye zahanati na vituo vya afya vinafanya kazi ili kuhakikisha mawasiliano yanakuwepo kwa ajili ya kusaidia wagonjwa vijijini.
Baraza la madiwani limempa mganga huyo mwezi mmoja kuhakikisha redio zilizonunuliwa na halmashauri zinafanya kazi na endapo agizo hilo halitatekelezwa halmashauri itawawajibisha wahusika.
Imeelezwa kuwa licha ya kununuliwa kwa ‘radio Call’ hizo na kufungwa katika zahanati na vituo vya afya, baadhi ya zana hizo hazijafanya kazi kutokana na kinachodaiwa na mganga huyo kuwa mbovu kabla hazijafanya kazi iliyolengwa.