Wazazi wameshauliwa kupunguza kasi ya kuzaa na badala yake wajiwekee mikakati endelevu ya kuwatunza watoto walionao ili kuondoa tatizo la watoto wa mitaani na ajira kwa watoto wao.
Rai hiyo imetolewa mwishoni mwa wiki na mwalimu wa taaluma wa shule ya sekondari ya wasichana Boni Consilii Mabamba Bw. Phares Peter wakati akihojiwa na mwandishi wa habari hii.
Mwalimu Peter amesema tatizo la kuongezeka kwa watoto wa mitaani pamoja na watoto wanaoajiriwa ni matokeo ya wazazi kutopanga uzazi na kushindwa kabisa kuwalea watoto wao.
Amebainisha kuwa baadhi ya watoto hushinikizwa na wazazi kuacha shule na kuingia katika ajira kama sehemu ya wazazi hao kukwepa majukumu ya malezi na baadhi yao huuchukua ujira wa watoto hao.
Aidha kwa upande mwingine mwalimu wa taaluma wa shule hiyo amezitaka serikali za vijiji hadi ngazi ya wilaya kushirikiana na taasisi nyingine kutoa elimu kwa wazazi na kukomesha kabisa tatizo la wazazi kutelekeza watoto.