Na Eva Musiba, Mwanza
NAIBU Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo, Emmanuel Nchimbi ametoa mwito kwa vyombo vya habari kuandika habari zenye kujenga utamaduni wa Mtanzania ili uheshimiwe na kulindwa kwa ajili ya vizazi vijavyo.
Aliyasema hayo juzi alipokuwa anatembelea vituo vya redio, televisheni na kampuni ya uchapaji magazeti ya CPPC ya jijini Mwanza.
Pia Naibu Waziri alikutana na waandishi wa habari wa mkoa wa Mwanza ambapo katibu wa chama cha waandishi wa habari mkoa, Jacob Kambili alisema kuwa kuna umuhimu wa serikali kuangalia uwezekano wa kurudisha utaratibu uliokuwepo wa maofisa habari wa mikoa.
Alisema malalamiko yanayotolewa na wadau mbalimbali wa habari juu ya baadhi ya waandishi, ambao ni wa kujitegemea, kutoaandika habari wakati wa ziara za viongozi yatamalizika tu pindi kutakapokuwa na maofisa hao, watakaokuwa waratibu wakuu.
Kambili alibainisha kuwa tatizo hilo linatokana na viongozi kumwita mwandishi mmoja mmoja, ambapo wakati mwingine sera ya gazeti inamhitaji kuandika habari sera inavyotaka na hivyo kulazimika baadhi ya habari kutoonekana.
Dk. Nchimbi aliwataka viongozi hao kuwa na ushirikiano na chama cha waandishi mkoa huu ili kupunguza malalamiko yanayojitokeza dhidi ya baadhi ya waandishi.
Naibu Waziri anaendelea na ziara katika mikoa ya kanda ya ziwa.